Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA K.n.y. WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa kuhitimisha Hoja niliyoitoa hapo tarehe 8 Februari, 2021. Awali ya yote, nikupe pole wewe mwenyewe pamoja na Mheshimiwa Spika na sote hapa Bungeni kwa ajili ya kuondokewa na mpendwa wetu ambaye tumekuwa naye muda wote hapa Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyotangulia kusema hapo tarehe 8 Februari, 2021 niliwasilisha katika Bunge lako Tukufu Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa wa Miaka Mitano (2021/2022 hadi 2025/ 2026, Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa ya Mwaka 2021/2022 na Mwongozo wa Maandalizi ya Bajeti kwa Mwaka 2021/2022 ambapo Waheshimiwa Wabunge wamepata fursa ya kuyajadili kwa siku takribani tano na kuiwezesha Serikali kupata maoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchukua fursa hii kukushukuru sana wewe binafsi pamoja na Mheshimiwa Spika kwa kuendesha mjadala huu kwa ustadi mkubwa ambao tunauhitimisha hii leo. Aidha, napenda kuchukua fursa hii pia, kuishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti chini ya Mwenyekiti wake Mheshimiwa Sillo Daniel Baran, Mbunge wa Babati Vijijini, kwa maoni na ushauri mzuri walioutoa kwa ajili ya kuboresha mapendekezo haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kutumia fursa hii kuwashukuru sana Waheshimiwa Mawaziri na Manaibu Mawaziri kwa ufafanuzi walioutoa pamoja na michango ambayo wametupenyezea ya kuendelea kuboresha mpango huu, nikitambua mchango wa Naibu Waziri aliyeleta mapendekezo kuongeza masuala yanayoongelea upande wa watu wenye ulemavu. Aidha, niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote kwa michango waliyochangia na hadi sasa imefikia Wabunge 164 waliochangia; kati yao 153 wakiwa wamechangia kwa kuzungumza na 11 wakiwa wamechangia kwa maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba, kusudi la mjadala huu ilikuwa ni Wabunge waweze kutoa maoni yao, ili tuweze kuboresha mapendekezo haya na sisi kwa niaba ya Wizara tuseme tumeyapokea, kwa niaba ya Serikali tuseme tumeyapokea. Yale ambayo moja kwa moja yataenda kuboresha Mpango tutayafanyia kazi kwa namna hiyo na yale ambayo yanahitaji ufafanuzi mengine tutafafanua hapa na mengine tutaleta kwa maandishi kwa kuzingatia kwamba, michango imekuwa mingi san ana michango mingi imekuwa na manufaa makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichangie kwa kufafanua michache tu ile ambayo inahitaji ufafanuzi na ile yote ambayo inaboresha Mpango na mapendekezo haya tutaenda kuitumia kwenye kupendekeza, ili tuweze kuleta tena, kama taratibu za kibunge zinavyosema. Moja ya hoja ambayo ningependa sana kuitolea ufafanuzi ili kuweka kumbukumbu sawa ni ule mjadala uliokuwa unahusisha masuala ya tafsiri ya uchumi wa kati, maana yake na kwa mwananchi mmoja mmoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja ilikuwa inatolewa hoja kana kwamba, kipato kile kilichopimwa ni kidogo sana, lakini lingine ilikuwa inatiliwa mashaka tu dhana yenyewe ya kwamba, tuko uchumi wa kati. Napenda kuliarifu Bunge lako tukufu kwamba, kwanza utaratibu wa kuingia uchumi wa kati ni utaratibu ambao unazingatia vigezo. Tanzania kuingia uchumi wa kati haikutuma maombi kwamba, tunaomba na sisi tuingie tuwe nchi ya kipato cha kati. Hatukufanya application na wala Tanzania kuingia kipato cha kati haikulipia, ni tofauti na utafiti unaweza uka-commission team kwamba, nifanyieni utafiti huu mniletee ripoti; hatukulipia kwamba, tunalipia ili mtufanyie utafiti mtuambie kama tumeshafika uchumi wa kati ama la. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hilo ni jambo linalozingatia vigezo tena vigezo vyenyewe vimezingatiwa na taasisi kubwa zinazoheshimika duniani, World Bank, IMF na wachumi wote ambao wameitangaza Tanzania kwamba, ni ya uchumi wa kati wala sio washabiki wa CCM. Ni taasisi za wasomi waliobobea na hawajaanza kwa kuitangaza Tanzania, zipo nchi ambazo ziliwahi kufika kule na zimefika kule kwa kuzingatia vigezo. Vigezo vyenyewe hata hapa sisi ukianza kuangalia tangu tumeanza kutekeleza Mpango mpaka tumefika hapa ni vigezo ambavyo tofauti zinaonekana na vigezo hivyo kwa yule ambaye ataifanyia tathmini Tanzania yetu kiungwana, lazima atafikia katika majawabu ya aina hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa wale waliokuwa wanasema kiwango chenyewe kile tulichofika ni kidogo sana, kwanza hawaitendei haki nchi yetu na pili hawamtendei haki Rais wetu, kwa sababu, tulitarajiwa tufike by 2025 tumefika mapema kabla ya muda ule. Tumefika mapema kabla ya muda ule kwa sababu ya ujasiri na uthabiti wa Rais wetu kwamba, kuna mambo ambayo yametekelezwa kwa kasi kubwa na kwa kiwango kikubwa kuliko ambavyo yalikuwa yakitekelezwa kwa muda mrefu tangu tumeweka mpango ule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano ukiangalia vigezo ambavyo huwa vinatumika, pato la mtu mmoja mmoja kufikia wastani wa dola za Kimarekani 1,036; la pili, kupungua kwa utegemezi wa bajeti na kuongeza fedha kwenye matumizi ya huduma za kijamii. Mengine ni kuboreshwa kwa miundombinu katika nchi husika. Ukienda kwenye wastani ambao waliutumia na ndio wakatoa majawabu yale, utaona kwamba, wastani wa pato la mtu mmoja mmoja GNI per capita uliongezeka kutoka Sh.990,462 sawa na dola za kimarekani 980 kwa mwaka 2015 hadi kufikia Sh. 2,577,967 sawa na dola za kimarekani 1,000,080 kwa mwaka 2019, hivyo, kuvuka kigezo kile kilichowekwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni kupungua kwa utegemezi wa kibajeti. Ninyi wenyewe ni mashahidi, kama ninyi mnasema wale watu wamesema tu kama na Benki ya Dunia na IMF imeshakuwa umoja wa vijana na wengine UWT, angalieni ninyi wenyewe utegemezi wa bajeti ulivyopungua. Mwaka 2015/2016 bajeti yetu tuliyokuwanayo ilikuwa takribani trilioni kama 22 hivi, hivi tunavyoongea tumeshavuka trilioni 34 na utegemezi umepungua zaidi, lakini si hayo tu ambayo tunayataja kwa bajeti kwa ujumla wake, nendeni mkaangalie sasa kwenye huduma ambazo wao ndio wanapima ambazo zimetuvusha kwa kiwango kikubwa, nendeni mkaangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye afya, katika miaka mitano takribani trilioni moja imeenda kujenga vituo vya afya vile na imetengeneza wastani wa kila tarafa ina kituo cha afya ambacho kinaweza kikatoa huduma kwa akinamama, kwa watoto, theatre, maabara, pamoja na vitu vingine vyote vya muhimu vinavyotakiwa. Ukienda kwenye umeme zaidi ya vijiji 10,000 vimewaka, ndani ya miaka mitano na zaidi ya trilioni tatu zimekwenda tena ni fedha za bajeti yetu. Ukienda kwenye miundombinu ambayo na yenyewe ni msingi mkubwa wa kujenga uchumi unaojitegemea, zaidi ya trilioni 8.6 zimekwenda kutengeneza miundombinu ya aina hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kwenye utawala bora karibu trilioni moja. Ukienda kwenye usafiri wa majini karibu trilioni moja. Wewe unayepinga kwa nini unaona sifa kuitwa maskini? Yaani wenzako wamekuangalia wakaona wewe umeshaondoka kwenye umaskini, wewe unajisikia bora zaidi wakuone wewe ni maskini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, angalia nchi inayoweza kutoa bilioni 24 kila mwezi kupeleka elimu kwa watoto wake na haijakwama. Angalia nchi inayoweza kutoa takribani bilioni 700 kulipia watoto kwenye elimu ya juu, tunaita mikopo, lakini kimsingi ni bajeti ya Serikali kwa sababu, hawakopi benki hawa ni bajeti ya Serikali. Mambo mengi yamebadilika, hata jana tu simba kushinda kule ni uchumi wa kati, ndio maana hawakuwahi kushinda siku zilizopita, viwango vyao vilikuwa vya kiuchumi wa kati. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachokisisitiza kwamba, vigezo vyote ambavyo nchi ya uchumi wa kipato cha kati inatakiwa kufika, Tanzania imevifikia na tumpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa sababu ya uthabiti wake tumeweza kuyafikia haya na wale wapiga ramli wanaosema hatutaweza, niwaambieni tunasonga mbele haturudi nyuma, tunakwenda Kaanani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni mazoea, mtu aliyezoea sana kuitwa maskini, aliyezoea, bado anahitaji tiba kwenye mindset kuona kwamba, yeye hayuko kwenye umaskini. Ni kama kuku aliyefungwa miguuni muda mrefu, kuku aliyefungwa miguuni muda mrefu hata ukimwondolea kamba anaendelea kuegama hivyohivyo akidhania bado amefungwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wengine wakiambiwa ni wastani wa pato la Taifa limegawanywa kwa uwiano wa wananchi waliopo wanadhani pakigawanywa hivyo kila mtu anapelekewa fedha nyumbani; kwa sababu, tunasema tunagawanya pato, wanadhania wataletewa kila mmoja nyumbani. Si hivyo, huu ni wastani na kama wewe hautashiriki kwenye kuzalisha, kama wewe hautafanya kazi ni dhahiri hautapata hela, kwa sababu, haujazalisha. Wewe ambaye hufanyi kazi na hupati hela ndiye unayetuchelewesha tusiende kwenye takwimu kubwa zaidi ile ambayo tunatakiwa tuifikie. Huo ndio utaratibu na hivyo ndivyo uchumi unavyosema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wengine wanawaza changamoto tu za maisha kwamba, sasa hivi mambo mengi ambayo ni ya kimaendeleo ndio yanatufanya tuwe na matumizi mengi, ndio inafanya wachukulie kwamba, huo ndio ugumu wa maisha. Hebu fikirieni zamani kabla ya changamoto za maendeleo bajeti zilikuwa zinaenda wapi?

Mheshimiwa Naibu Spika, hatukuwa na simu, kwa hiyo, hakukuwepo na mambo ya simu yenyewe, air time, wala MB. Tulikuwa tunakula chakula kilichosagwa kwenye jiwe na mama zetu na dada zetu waliokuwa wanasaga tulikuwa hatuwalipi, tulikuwa hatutumii gharama ya kwenda kulipia mashineni. Tulikuwa hatuna umeme kwa hiyo, tulikuwa hatuunganishi hatuna gharama ya umeme, tulikuwa hatuna TV, hatuna ving’amuzi. Tulikuwa tunachota maji kwenye madimbwi, tulikuwa hatulipii, sasa unatakiwa ulipie na bili ya maji na umeme. Tulikuwa tunalima tu ardhi ina rutuba kwa hiyo, tulikuwa hatutumii mbolea tunatumia samadi, hatutumii mbegu tunaanika tu mbegu zile.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa, sasa hivi hizi changamoto zote ambazo ndio maendeleo yenyewe zimesababisha bajeti constraint, yaani fedha yako ile igawanyike kwenye matumizi mengi, hiyo ndio tunaenda kusema hakuna maendeleo ni maisha mabaya. Ni tafsiri mbaya na wengine waliokuwa wanatafsiri walikiri wenyewe, nilimsikia Mheshimiwa Halima akisema kama bajeti hii imeandikwa na Dkt. Mpango Gwiji wa Uchumi ambaye anatambulika na Benki ya Dunia na IMF na vyuo vyote vya duniani, yeye ni nani hata aseme lingine?

Mheshimiwa Naibu Spika, alikuwa anawaambia kwa lugha nyingine kwamba, yale anayoyasema yeye kwenye area hii yapuuzeni haelewi kitu. Ukweli ni haya ambayo yameandikwa kitaalam na ninyi mnatakiwa mwelekee katika mwelekeo wa aina hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hii ya Stieglers Gorge kule ambayo ilikuwa inasemwa, Mwalimu Nyerere Power Station; watu wanaenda kusema tu kwenye asilimia eti ni asilimia 25 tu, hata reli ya kati wanasema eti imeshajengwa tu ni kiwango hiki hapa tu. Fuatilieni hata historia, reli ya kati hii hapa ilijengwa kwa takribani miaka 10. Tena kipindi hicho hakukuwepo na fedha zinazokwenda kwenye elimu bure, hakukuwepo na fedha zinazojenga hospitali nyingi hivi, hakukuwepo na fedha zinazojenga lami kilometa 13,000, hakukuwepo, hata population yenyewe iliyokuwa inahudumiwa na Serikali ilikuwa ndogo tu, lakini leo hii ukianzia kule kilometa 300 za kwanza ni aslimia 90. Hata kile ambacho kinachelewesha ni utaratibu wa kujenga kwa uimara zaidi, lakini mambo yote yameshakamilika mpaka mwisho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda Stieglers Gorge hivyo hivyo, Mwalimu Nyerere Power Station ile, wanasema ni asilimia 25 tu, lakini nendeni mkaangalie fedha iliyowekwa pale ni trilioni 1.9. Kwa hiyo, vingine ni kiutaratibu kwa sababu, hatupimi kwa kumwaga tu fedha, kuna shughuli zinafanywa tena kwa uthabiti mkubwa. Haya ni mambo ambayo napenda nimpongeze sana Mheshimiwa Rais na wale wasioyapongeza haya, watoto wao watakuja kuwasuta kwamba, aliwahi kupita Rais mmoja akiitwa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli alifanya mambo makubwa haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo liliongelewa sana lilikuwa hili jambo la matumizi ya kutumia task force kwenye makusanyo ya mapato. Kwanza Waheshimiwa Wabunge niwaombe sana kwenye hili jambo tunapoliongelea hili la makusanyo tunatakiwa twende kwa tahadhari sana. Mwenzenu nina kumbukumbu nzuri kabisa kwa sababu, niliwahi kuwa Naibu Waziri wa Fedha wakati awamu inapita inamalizikia na Awamu hii ya Tano inaingia; natambua kazi kubwa waliyofanya Serikali ya Awamu ya Tano kwenye mambo ya makusanyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna kipindi tumekipita ambacho ulipa kodi, elimu ya mlipa kodi, uhiari na uzalendo, lilikuwa jambo kubwa na gumu sana kwa watu wetu, kwa walio wengi, hasa wafanyabiashara wakubwa, hasa walipakodi wakubwa. Ukwepaji wa kodi, nendeni mkafuatile Hansard za Bunge lile lililopita, fuatilieni Hansard muone kilio kikubwa kilikuwa wapi? Kilio kikubwa kilikuwa walipa kodi hasa wakubwa hawalipi kodi ipasavyo; walipakodi waliokuwa wanabeba nchi ni watumishi wa umma kwa kiwango kikubwa na walipakodi wadogowadogo na baadhi yao walipa kodi wakubwa waliokuwa waaminifu, kulikuwepo na kiwango kikubwa sana cha ukwepaji wa kodi, kikubwa mno na kulikuwepo na Serikali bubu, Serikali ikipanga namna ya kukusanya kodi kulikuwa na reaction ya Serikali moja bubu; ipo kule tu yenyewe ipo tu, mkipanga bajeti ina-hire ndege inakuja, hii haitatekelezeka, ilikuwa namna hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujasiri wa Rais wetu pamoja na ubunifu wa Waziri wetu katika kumsaidia Rais pamoja na timu yake ya wataalam wakiwepo TRA wamepiga hatua kubwa sana. Sasa, sasa hivi hili jambo linaloanza kujitokeza la kwamba, task force ndio zinakusanya na TRA imeacha majukumu yake, naomba nilihakikishie Bunge lako Tukufu kwamba, TRA bado wanaendelea kukusanya mapato wao wenyewe. Pale ambapo inatokea task force inakusanya kunakuwepo na hatua zinazofuatwa. Moja, kunakuwa na taarifa kwamba, kwa mlipakodi huyu kuna viashiria vya kutokulipa kodi ipasavyo. Baada ya hapo kunatumwa timu ya kwenda kukagua, timu ya kawaida tu ya kwenda kukagua ambayo ni Mamlaka ya Mapato, ni wataalam wao. Wakishakagua wanaambizana, wanaelekezana kwa mujibu wa sheria, sheria zetu mlipakodi mnajadiliana katika yale makadirio, wanakubaliana na wakati mwingine wanasainiana, inatokea hataki kulipa ama inatokea amekata rufaa. Hili lilikuwa linatumika sana miaka kadhaa ile iliyopita.

Mheshimiwa Naibu Spika, ilikuwa mtu akiona anataka kudaiwa kodi anaenda anai-park mahali pale panaitwa appeal, ana-park mahali hapo halafu maisha yanaendelea. Akitoka hapo anaipeleka tribunal ana-park hapo maisha yanaendelea. Sasa inatokea uamuzi umeshafanyika kwamba, anatakiwa alipe ama inatokea pana taarifa zinazoonesha kuna ukwepaji mkubwa, hapo ndipo kwa kukwepa, kwa kuondokana na uwezekano wa kufanya kazi kwa mazoea, kwa kukwepa na kuondokana kwa uwezekano wa vitendo vya rushwa kuweza kutumika katika masuala haya ya ku-bargain rushwa, ya ku-bargain fedha za kodi, timu maalum inapelekwa na Kiingereza chake ndio hiyo inaitwa task force ambayo kiongozi wao anazingatia ile miiko ambayo inatakiwa itumike katika kukusanya kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata Bunge lako tukufu lilikuwa likisisitiza panapokuwepo na operation isiende taasisi moja wala asiende mtu mmoja, ndio tunavyotumia hata kwenye operation zingine, tunatengeneza team ambazo ni multidisplinary ili kuweza kuchangia uzoefu, lakini pia na kuzingatia maadili ya kwenda kufanya jukumu lile pasiwepo na rushwa, pasiwepo na uonevu, lakini pia pawepo umakini mkubwa zaidi katika jambo lile. Hicho ndicho ambacho kimekuwa kikifanyika katika jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais amelisisitiza sana jambo hili kwamba mara zote mfanyabiashara anayefanya kazi zake ama biashara zake ambazo zimenyooka asibughudhiwe, ameshawaambia hata wafanyabiashara wenyewe kwenye vikao vile, ameishaielekeza Wizara, ameshawaelekeza Mamlaka ya Mapato, wazingatie miiko hiyo. Kinachofanyika ni pale panapotokea sasa kuna watu wasiozingatia taratibu wa kulipa kodi, panapotokea watu wanakwepa kodi, panapotokea watu wanafanya njama na njama ziko nyingi sana za kukwepa kodi. Ndio Kamishna wa Mamlaka ya Mapato kwa kutumia sheria inayomruhusu kutengeneza kikosi kazi kama ambayo mnajua, Sura ya 348 ya Sheria ya Utawala wa Kodi inampa mamlaka Kamishna kuunda vikosi na kushirikisha taasisi zingine za umma, Kifungu cha 64 vifungu vidogo mpaka 67 vinampa mamlaka ya kutengeneza vikosi kazi ambavyo vinaweza kwenda kusaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge kwa mazingira haya kwamba tuna miradi tunatekeleza, kuna wengine wasiotutakia mema hata wasingependa tutekeleze, hatuwezi kutekeleza kwa kuomba hela, hatuwezi kuitekeleza kwa kukopa mikopo ya kibiashara halafu tukatekeleza miradi mikubwa ya kiwango hicho, lakini pia hatuwezi tukatekeleza hata hii miradi mingine yote hii tunayoitekeleza bila kuzingatia suala la kulipa kodi. Nitoe rai kwa Waheshimiwa Wabunge pamoja na Watanzania wote tuendelee kujenga uzalendo kwa Taifa letu, maendeleo yetu yatakuja kwa sisi kulipa kodi. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha pamoja na timu yake pamoja na TRA waendelee kufanya kazi kwa kuzingatia maadili pamoja na miongozo ambayo inawaongoza katika kutekeleza majukumu yao hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kutoa rai kwa Watanzania tulipe kodi na kwa wale ambao walizoea kukwepa kodi kuwaachia mzigo watu wengine na kupata mapato hayo ambayo yalitakiwa yakasaidie huduma za jamii wakayageuza yawe ya kwao, niwahakikishie mazingira ya yao kufanya ukwepaji wa aina hiyo yataendelea kuwa magumu tu, kwa mtu anayepanga kufanya biashara kwa kukwepa kodi mazingira hayo yataendelea kuwa magumu tu kwa sababu haturudi tena kule, tunataka tujenge utamaduni wa watu kulipa kodi kwa sababu hiyo ndiyo inayotufanya nchi yetu iweze kujitegemea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Wabunge wenzangu wa CCM Watanzania wengi hawakumchagua Rais kwa sababu ya rangi ya nguo aliyovaa, walimchagua kwa sababu wameona miradi hii iliyotekelezwa haijawahi kutekelezwa kwa kiwango kikubwa cha kiasi hiki. Mtu yeyote akitushauri tuache kujitegemea, mtu yeyote akitushauri tuache kutekeleza miradi, tunatakiwa tuchukulie huyu mtu anataka kutukwamisha kwenye nia yetu hii ya kuwatumikia Watanzania na Ilani yetu tuliyoitengeneza ya mwaka huu ni kubwa kuliko ile ambayo tuliitengeneza kwa wakati ule. Nini kinachowauma wengine huku ni uchache wenu, mmejua tumefanya makubwa tumeingia wengi kwa sababu ya ushindi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu ambalo ningependa nilifafanue kuna hoja ilitolewa kuhusu mfumuko wa bei hii na yenyewe niliona ilikuwa ina misinterpretation ina tafsiri ambazo zinakinzana. La kwanza, mfumuko wa bei siyo bei, inflation rate is just a rate is percentage rate showing how quickly the prices are changing.

WABUNGE FULANI: Kwa Kiswahili.

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA K.n.y. WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mfumuko wa bei ni kile ile kasi ya kile kiwango cha bei zinavyobadilika, siyo bei zenyewe. Ukienda tu ukasema mimi jana nimeenda nikakuta bei imeshakuwa hivi, bei iko hivi, ukilinganisha na ya mwaka jana ama ya mwaka juzi, sijui wengine wanachukuliwa ya mwaka gani, ule si mfumuko wa bei, zile ni bei na bei zingine zinatokana na seasonalities, ni kubadilika kwa majira. Kwa mfano bei ya alizeti wakati wa mavuno na bei ya alizeti wakati ambao siyo wa mavuno, ni vitu tofauti.

Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo unailinganisha tu mavuno ya mwaka jana na mavuno ya mwaka huu yalikuwaje na mmevuna kwa kiwango gani. Kwa mfano mwaka ule uliokuwa na mafuriko makubwa sana umeathiri kilimo, kwa hiyo kuna baadhi ya mazao yanayotokana na kilimo cha aina hiyo kama dengu, maeneo yale yaliyokuwa yanalimwa ikitokea pamekuwa na mafuriko kote hayajatoka vizuri, definitely mwaka kama ule karibu na kilimo kingine kutakuwepo na tofauti ya bei. Ttunachokisemea kama Serikali ni kwamba ile kasi ya kubadilika kwa bei kwa mazao yaliyo mengi na kwa bidhaa zilizo nyingi zinazotumika kwenye viashiria, kwa kipindi chote hicho imekuwa imara. Hicho ndicho tunachopima kwenye mfumuko wa bei na hatufanyi mfumuko wa bei uwe imara kwa kutumia Jeshi wala Polisi, tumetengeneza miundombinu ambayo inafanya ule uimara wa bei katika bidhaa hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, wale waliokuwa wanabeba vitunguu kutoka Manyara kuleta Dodoma kabla ya miaka mitano walikuwa lazima wazungukie Singida waje hapa. Wale waliokuwa wanabeba bidhaa kutoka Mbeya, Njombe, Iringa kuleta Dodoma ilikuwa lazima waende Morogoro ndiyo walete hapa. Kwa kutengeneza miundombinu inayopunguza gharama za uzalishaji na gharama za usafirishaji, kunatengeneza bei ziwe imara, zikishakuwa imara hicho ndicho tunachokipima kwa sababu zinasawazisha kutoka kwenye wingi kwenda kwenye upungufu, hiyo ndiyo mikakati na ndiyo maana tunasema miundombinu hii inaenda kumsaidia mwananchi moja kwa moja kwenye maisha yake. Hili limekuwa likifanyika, kwa hiyo tusije tukachukulia kwa dhana finyu ambayo inawaletea hamaki wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu nimeisikia kengele imegonga, niende hoja moja ya mwisho wakati namalizia malizia. Lingine ambalo lilijitokeza kwa kiwango kikubwa lilikuwa suala la deni la Taifa. Nishukuru na nipongeze hoja ya Kamati wameleta kiashiria kile walichokisema cha kuangalia mapato, hicho huwa kinatumika tunapoangalia masuala ya ndani, lakini kwenye vigezo vile vinavyotumika ambavyo ni standard na vimewekwa standard ili uweze kulinganisha na maeneo mengine, niwatoe hofu kwamba uchambuzi wa deni la Taifa unatumia model ambayo ni ya Shirika la Fedha la Dunia na viashiria vyote vinaonesha deni ni himilivu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, deni la nje kwa pato la Taifa ukomo wake huwa ni 55%, sisi tuko 17.3%. Thamani ya deni la nje kwa mauzo ya bidhaa na huduma za nje ya nchi ukomo wake huwa ni 240%, sisi tuko 113.2% tu. Uwiano wa malipo ya madeni ya nje kwa mauzo ya bidhaa na huduma nje ya nchi ukomo wake huwa ni 21%, sisi tuko 14% tu na uwiano wa malipo ya madeni ya nje na mapato ya ndani ambapo kwa mwaka huwa ni 23% sisi tuko 13.7%. Kwa hiyo haya mambo yote yanafanyiwa tathmini na pale tunapokwenda kwenye masuala yanayohusu mikopo ya ndani ambapo soko la fedha la ndani bado lina ukwasi wa kutosha huwa tunazingatia kile kigezo ambacho kimewekwa cha ukomo katika masuala haya ya kukopa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwamba hoja zenu zote mlizozitoa tunazizingatia, tumezipokea na majina yenu yote yameingia kwenye hansard (Kumbukumbu Rasmi za Bunge) na sisi tumepokea na zile hoja zenu zitachambuliwa moja baada ya nyingine na zingine zitakwenda kuboresha Mpango na zingine ambazo zinahitaji ufafanuzi ambazo nitakuwa kwa ajili ya muda sijagusa, mtaletewa kwa maandishi ili muweze kuona ni kitu gani ambacho Serikali imekieleza kwenye jambo mlihitaji ufafanuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu hili ndiyo Bunge la kwanza kwa Mpango huu tunaoupanga na kwa awamu hii, niwaombe tuendelee kutoa uongozi, tumsaidie Mheshimiwa Rais. Kwa sisi ambao tumefanya naye kazi, Mheshimiwa Rais wetu uzalendo wake kwa Taifa hili ni wa kiwango cha juu sana na Watanzania wanakiona. Nia yake kwa maisha ya Watanzania ni ya kiwango cha juu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimefuatilia sana hizi siasa, nilikuwa napenda siasa tangu niko shule ya msingi. Afrika hapa kupata Rais ambaye 24 hours na kwa mwaka mzima na kwa awamu nzima anashughulika na maisha ya watu wake tu, tuwe wa kweli its very rare, ni ngumu kupata kitu cha aina hiyo. Kuna marais wako, sitaji nchi hizo, Afrika hapa hapa, wanaongoza nchi wakiwa hoteli huko nchi za Ulaya, yuko hoteli na mke wake huko wanaongoza, wako nje, wa kwetu hata akipata likizo unamwona yuko Chato tu na anaendelea kufanya kazi hapo hapo anashughulika na maisha ya Watanzania. Fedha zote zinakwenda kwenye mambo ya maendeleo.

Kwa hiyo hata hapa ambapo unaona namna hii tulivyofanya hapa, mlivyoona hii miradi na miaka mitano hiyo mpaka tukaweza kuingia kwenye kipato cha kati na tukaweza kutengeneza maendeleo kwa kiwango kikubwa hivyo unaweza ukaona ni commitment ambayo imetokea kwa maaana hiyo na sisi kama viongozi tuendelee kuunga mkono shughuli hizi maendeleo yanapotokea ni yetu sisi sote na sisi tutaingia kwenye record ya kuwa tulichangia pale ambapo tulikuwa na nafasi hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuwa, nimetoa ufafanuzi huu naomba sasa kutoa hoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.