Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi jioni hii niwe mchangiaji wa mwisho kwenye hii hotuba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa watu wengi wameshachangia mambo mengi sana, mimi nataka nianze tu na hii sekta ya kilimo. Ni sekta ambayo imechangiwa karibu na Wabunge wote. Yale mambo ambayo nitayazungumza, siwezi kurudia yale ambayo wenzangu tayari ameshayazungumza. Nataka tu nigusie sehemu moja inayohusu mambo ya masoko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba tuna tatizo la utafiti, pembejeo na mambo mengine, lakini soko ni tatizo kubwa zaidi. Kwa sababu wakulima wengi hata wale wadogo wadogo wanaojitahidi kulima, wakihangaika. Nitoe mfano tu, hapa juzi tumesikia kwamba kuna wakulima wa miwa wa Morogoro wamekosa soko, miwa imeungua moto. Leo kuna wakulima Shinyanga wanasema mchele unakosa soko lakini ukienda Mtwara unakuta mchele kilo moja ni Sh.3,000/= mpaka Sh.4,000/=. Tatizo bado Serikali haijajikita kuhakikisha wakulima wetu wanapata uhakika wa kuwa na masoko ya kudumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu wanachangia hapa wanasema wasomi wetu hawako tayari kwenda kwenye kilimo. Jamani, ni msomi gani atakubali kwenda kwenye kilimo akalime heka 10 au 20 za korosho asikie kwamba korosho zimekosa soko? Huyo mkulima ili aweze kujiandaa lazima ataandika andiko, atakwenda benki, atakopa fedha, atafungua shamba la kulima miwa, akihakikishiwa kwamba Kilombero watachukua miwa, inafika mwisho wa msimu, wanakwambia Kilombero wametosheka na miwa, haina soko. Huyo msomi ambaye amechukua fedha kwenye mabenki, amekosa soko, anakwenda kuzilipa vipi pesa alizokopa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni mkulima gani ambaye tangu amezaliwa amemkuta baba yake analima kwa jembe la mkono, shangazi yake analima kwa jembe la mkono, hajatoka; halafu yeye aseme mimi msomi nimetoka SUA naweza kulima kwa jembe hili la mkono litanitoa, litamtoa wapi? Kwa hiyo, tusianze kuwalaumu sana wasomi wetu, lakini lazima tuangalie Serikali imejikita vipi kwenye hili suala la kilimo? (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yuko Waziri mmoja hapa hapa, sikumbuki vizuri, 2015 alisema jembe la mkono linakwenda Makumbusho. Lile jembe mpaka leo halijafika Makumbusho. Lazima tuwe wakweli, bado tuna tatizo kwenye sekta hii ya kilimo. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya kilimo vilevile tuiunganishe na sekta ya miundombinu. Wako wakulima vijijini mazao yao yanaharibika kwa sababu ya miundombinu mibaya kulifikia soko. Leo Serikali, sera yetu inajikita kujenga barabara tunasema tunaunganisha mkoa na mkoa, tunajenga trunk road, tunakwenda regional road, lakini tunasahau ziko barabara zinazotakiwa zihudumie wananchi wetu kupelekea mazao kwenye soko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano tu Wilaya yangu Liwale, sisi ni wakulima wa korosho wazuri sana, lakini kwa sababu hatuna barabara; kutoka Nachingwea kwenda Liwale ni kilomita 124; Nachingwea korosho wanauza 3,000, Liwale wanauza 2,000 kwa sababu hakuna mfanyabishara yuko tayari kukanyaga pale Liwale kufuata korosho. Mnunuzi akinunua korosho kwa bei ya 3,000 akileta mpaka hata Dar es Salaam itakuwa imefika bei zaidi aliyochukua Mtwara au Lindi. Kwa hiyo, bado kuna tatizo la miundombinu. Kwa hiyo ili kilimo chetu kiweze kwenda sambamba na mpango huu lazima kwanza tufanye mageuzi ya kilimo kwamba tulime kisasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile tuhakikishe miundombinu rafiki ya kufikisha mazao haya kwenye viwanda, lakini yapo mazao mengine haya mazao ya msimu, kwa mfano kama nyanya, leo hata ukimwambia mtu afungue kiwanda cha kulima nyanya ambazo zinalimwa miezi miwili, miezi mitatu nyanya hakuna, kile kiwanda anakipeleka wapi, hicho kiwanda anafanya kazi peke yake, maana akishawaajiri watu wanachakata hizo nyanya kwa miezi miwili au mitatu, kiwanda kimefungwa kwa sababu nyanya hakuna. Kwa hiyo ni lazima twende na kilimo cha umwagiliaji. Kama kweli tunajenga kiwanda cha matunda, ni lazima tuhakikishe yule mwenye kiwanda anapata matunda muda wote na anapataje matunda muda wote, ni pale tu tutakapoanza kilimo cha umwagiliaji, lakini hiki kilimo cha kutegemea mvua, hakitatusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunazungumzia mananasi hapa kwa Mheshimiwa Rais mstaafu, kuna mananasi mengi tu, ukienda msimu Chalinze mananasi ni mengi mpaka yanaoza, lakini leo ukifungua kiwanda cha mananasi pale, kitafanya kazi miezi mingapi, miezi miwili au mitatu mananasi yamekwisha, inabidi kiwanda kifungwe na wale uliowaajiri inabidi uwape likizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kuwa na viwanda vya kudumu, ni lazima tuwe na uhakika kwamba tunakuwa na kilimo cha umwagiliaji, kilimo ambacho kitamhakikishia mwenye kiwanda cha matunda kile anapata matunda muda wote. Hili ni jambo ambalo nimeona nilizungumzie kwa namna hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile bado naendelea huko huko kwenye kilimo; tunapokwenda kuzungumzia kilimo cha umwagiliaji, bado ukienda katika skimu za umwagiliaji leo, bado tunatumia mito yaani hatuwezi kuweka skimu za umwagiliaji hapa Dodoma, hakuna mto, ni mpaka uwe pembeni ya mto ndiyo wanatengeneza kile kilimo cha umwagiliaji. Wakati mwingine yanapotokea mafuriko kama haya, ile mifereji yenyewe imevunjika, imeharibika, hakuna kilimo cha umwagiliaji. Naiomba Serikali tafadhali tafadhali, kama kweli tunataka tuisaidie nchi hii, tuwasaidie hawa vijana wa nchi hii, lazima tufanye maamuzi ya kufanya mageuzi ya kilimo, siyo hiki kilimo cha kutegemea mvua wala hiki sio kilimo cha msimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano mwingine, nimefanya kazi kwa Bakharesa miaka zaidi ya 20, wakati ule ngano ilikuwa inauzwa kilo moja Sh.200 nje, ngano ya Tanzania Sh.370. Bakharesa aliamua kwenda kulima ngano Basutu, kilichomkuta alilima mwaka mmoja tu akaacha. Watakuja OSHA hapo, watakuja TFDA, watakuja sijui Ardhi, watakuja watu wa madini, yaani wanakuja kibao. Ile ngano amelima, amevuna, ngano akiagiza India by then ilikuwa 240, ngano alilima Basutu ilifika 400, akaamua kuacha mpaka leo ngano ni shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kweli mpaka leo Bakharesa mimi wakati naondoka mwaka 2014 anasindika tani 1,500 per day, lakini yote hii anaagiza kutoka nje, 100 percent anaagiza kutoka nje. Sasa ni lazima kwanza tujenge mazingira, unajua tatizo lingine linakuja kubwa ni kwamba akionekana mtu anataka kufanya biashara, basi yule anaonekana sijui ameiba hela mahali, sijui anataka kufanyaje, atafuatwa milolongo hapo, itaonekana kama vile hafai, kwanza anaonekana mtu ana hela, hata yule anayekwenda labda anapeleka andiko lake, tayari anaanza kwanza kusachiwa, yaani zile pesa watu wanaanza kugawana kabla hazijafika huko shamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu ulikuwa ni huo tu. Ahsante sana.