Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Regina Ndege Qwaray

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa nafasi hii ili nami niweze kuchangia katika Mpango wa Taifa wa Miaka Mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kumpongeza Waziri wa Fedha kwa taarifa yake nzuri aliyoianda. Pia niipongeze Kamati ya Bajeti kwa kuandaa vizuri taarifa yao. Kwa namna ya pekee pia, niipongeze Serikali hii ya Awamu ya Tano kwa kazi kubwa inayofanya kuhakikisha Tanzania inazidi kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijikite katika sekta ya kilimo. Kilimo ni msingi wa uchumi wa viwanda na uti wa mgongo wa Taifa letu. Wananchi wengi wa Tanzania tunategemea kilimo ili kujikwamua kiuchumi, hasa wananchi wa vijijini wanategemea kilimo kujipatia mahitaji yao. Mwananchi wa kijijini anategemea kilimo kusomesha mtoto, kupata mahitaji yake ya msingi ikiwemo afya, yaani kilimo ndiyo kila kitu kwake. Pamoja na hayo yote bado wanakumbana na changamoto nyingi ikiwemo soko kwa maana kwamba baada ya mavuno, wananchi hawana soko la uhakika. Wanavuna lakini mwisho wa siku mazao yao hayapati soko kama inavyotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kilimo wanacholima kwanza kinakuwa hakina tija. Wanatumia vitendea kazi vilivyopitwa na muda. Akina mama wengi wa kijijini wanajihusisha sana na kilimo lakini hawana vitendea kazi vinavyowarahisishia kufanya kilimo kile kuwa chepesi zaidi. Hivyo inakuwa vigumu sana kupata tija au kupata manufaa kupitia kilimo. Wamama hao leo wanahangaika kutumia jembe la mkono katika kilimo, hawawezi kulima mashamba makubwa hivyo, wameishia kulima mashamba madogo madogo ambayo sasa mazao wanayoyapata ndio hayohayo wanatumia katika chakula na katika mahitaji mengine, mwisho wa siku wanaendelea kudhoofika kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo bado naendelea kushauri Serikali kuona ni namna gani watainua sekta hii ya kilimo ili wananchi wetu wa vijijini waweze kujikwamua kiuchumi. Kwanza nishauri Serikali iwekeze katika utafiti wa mbegu tunazozitumia. Mbegu zetu nyingi tunazotumia zinatoka nje ya nchi, asilimia kubwa mbegu za mahindi na mbogamboga hazizalishwi hapa nchini hivyo, husababisha wananchi kutumia gharama kubwa kupata mbegu na kutumia mbegu ambazo sio bora katika kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nashauri Serikali ifundishe wakulima wetu kuhifadhi na kusindika mazao ili waweze kuuza bidhaa badala ya malighafi. Pia nishauri pia Serikali kujenga mabwawa ya kuvunia maji ili kuboresha scheme za umwagiliaji. Mfano, katika Wilaya ya Babati kuna Vijiji vya Shauri Moyo, Masware, Kisangaji, Bonde la Kiru, Madunga, Narkash, vyote vinategemea kilimo cha umwagiliaji, lakini hawana uwezo mkubwa au teknolojia ya kutosha kuvuna maji ili waweze kuendesha kilimo cha umwagiliaji katika maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima wengi hawana elimu ya kutosha. Hawaelewi ardhi yao wanayoitumia ni mazao gani hasa yanastawi, hivyo wanastawisha mazao ambayo wakati mwingine hayaendani na maeneo yao. Maafisa Ugani katika maeneo yetu bado ni wachache sana. Niishauri Serikali kuongeza Maafisa Ugani katika kila kijiji ili waweze kuwaelimisha wananchi wajue ni mazao gani yanastahili kustawishwa katika maeneo yao, lakini pia waweze kutoa shamba darasa. Yale mafunzo ya shamba darasa yanasaidia wananchi kuona kwa vitendo ili waweze kuzalisha mazao yale yanayoendana na maeneo yao na pia yaweze kuwaletea tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri pia vyuo vya kilimo viboreshwe. Vyuo vyetu vya kilimo haviendi kulingana na ukuaji wa teknolojia. Bado tunatumia mbinu zile za zamani katika kuwapa mafunzo wale wataalam wa kilimo ambao wana kazi ya kwenda kuwaelimisha wakulima hawa, ili waweze kuzalisha mazao kwa kiwango kikubwa. Mfano, Chuo cha Sokoine nashauri Serikali ione ni kwa namna gani kiendelee kubaki na kutoa taaluma inayohusiana na kilimo, uvuvi badala ya kujikita katika kutoa fani ya ualimu. Kama inavyotambulika ni Chuo cha Kilimo, kibaki katika kutoa fani ya kilimo badala ya kujishughulisha na fani nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, katika Mkoa wetu wa Manyara, tunaomba Chuo Kikuu cha Sokoine kuanzisha shamba darasa katika mkoa wetu, ili wananchi wa mkoa ule waweze kufaidika na mafunzo ya kilimo na mwisho waweze kulima kilimo chenye tija na kufaidika na kilimo hatimaye kuleta maendeleo na mapinduzi katika viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi hii na naunga mkono hoja. (Makofi)