Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Kilumbe Shabani Ng'enda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii, lakini niseme kidogo sisi Wabunge ambao tumeingia kwa mara ya kwanza tunatumia njia mbili hapa kujifunza namna shughuli za Bunge zinavyoendeshwa. Ya kwanza ni hii ya kusoma kwenye Kanuni na nini na nyingine ni kuwaangalia wale wazoefu waliokuja hapa siku nyingi namna wanavyoendesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima niseme kwamba ninayo masikitiko. Wapo baadhi ya wazoefu wanachangia Mpango hapa wanasimama tangu ameanza mpaka anamaliza anakosoa tu halafu hasemi tufanyeje. Nilitaka kusema hilo kwa kweli sioni kama ni jambo jema ambalo sisi tunajifunza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwa maono yangu mimi Serikali ya CCM na inawezekana Serikali ya nchi nyingine yoyote duniani ingependa kuwafanyia wananchi wake kila jambo wanalotaka, kinachozuia kufanya hivyo ni uwezo. Ndiyo maana tuko hapa leo kupitia mipango kuona kupanga ni kuchagua, lipi litangulie lipi lisubiri kutokana na uwezo wetu. Kama tunataka tuongeze zaidi lazima tuseme tunapataje uwezo wa kufanya zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka nishauri kidogo kwenye eneo la ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (Public Private Partnership – PPP). Nimeangalia katika Mpango huu, ni miradi nane tu ambayo imewekwa katika Mpango wa PPP.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wa kwanza ni Kiwanda cha Dawa; mwingine ni Mradi wa Mabasi Yaendayo Kasi; Hoteli ya Nyota Nne; Uwanja wa Mwalimu Nyerere; usambazaji wa gesi asili; Reli ya Standard Gauge Tanga – Arusha – Musoma na Mtwara – Mbambabay; Mwingine ni hosteli ya Chuo cha Biashara Kampasi za Dar es Salaam na Dodoma; na Chuo cha Uhasibu Kampasi ya Dar es Salaam na Mbeya; na wa mwisho ni mradi wa Kiwanda cha Kutengeneza Simu. Hii ndiyo miradi katika mpango mzima wa mwaka ambayo imeingia kwenye PPP.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na PPP ndilo eneo ambalo lingeweza kutusaidia kushirikisha sekta binafsi katika kutekeleza mambo mengi ya Serikali. Kwa mfano leo hii usafiri wa Reli ya Kati kutoka Kigoma kuja Dar es Salaam, wasafiri wanaotakiwa kusafiri kila siku ya treni wanaoondoka ni asilimia 25 tu, asilimia 75 ya wasafiri wote wanabaki kwa ajili ya kukosa mabehewa. Kwa nini katika mpango huu tusingeingiza mabehewa kwenye PPP, wapo Watanzania wafanyabiashara ambao wangeweza kununua mabehewa ya treni yakafungwa. Sasa hivi injini hizi zinakokota mabehewa chini ya uwezo wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekwenda pale Stesheni ya Kigoma zaidi ya mara nne, mara tano. Injini inaondoka imefunga mabehewa nane yenye capacity ya kubeba mabehewa 30, mabehewa hakuna na mabehewa ya mizigo vilevile tatizo. Wakati mwingine yanakosekama mabehewa mpaka yanasababisha mfumuko wa bei ya saruji na bidhaa nyingine za viwandani zinazotoka Dar es Salaam kuja maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nataka niseme, naomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango atakapokuja hapa atueleze namna anavyoweza kuongeza wigo kwenye PPP. Naamini kabisa wapo Watanzania kama watu wanaweza wakanunua mabasi 115 wanashindwaje kununua behewa mbili, tatu au nne za treni akaingia katika utaratibu huu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye sekta ya afya vilevile bado tunaweza tukaingia kwenye utaratibu wa PPP. Nimeangalia sasa hivi kwenye hospitali zetu, tuna wodi za kawaida zile za msongamano na kuna wodi ambazo zimepewa grades; grade one na grade two. Wodi zile kukaa wodini siku moja acha huduma nyingine, unachajiwa kati ya shilingi 25,000 mpaka shilingi 40,000. Hiki ni kiwango cha lodge za kawaida za mjini ambazo mtu anaweza akakaa. Ukiwaambia wafanyabiashara wakujengee majengo hayo kwenye hospitali, watajenga tutaigia kwenye utaratibu wa PPP…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kilumbe, naona hii kengele bwana sijui ina matatizo gani. (Kicheko)

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Ina hiyana, lakini hakuna shida. Ahsante sana. Naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)