Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Bupe Nelson Mwakang'ata

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia Mpango uliopo mbele yetu. Kwanza kabisa namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uzima. Pia nawashukuru wanawake wa Mkoa wa Rukwa kwa kunichagua tena kwa kura nyingi sana za kishindo, nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kukushukuru wewe na ofisi yako na Wabunge wenzangu wote kwa ujumla wao kwa kunisaidia nilipopata matatizo ya kufiwa na kaka yangu hapa Dodoma, lakini Wabunge hawakuniacha, waliweza kunisaidia mpaka kwenda kuhifadhi mwili huko kwenye nyumba yake ya milele. Nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niingie sasa kwenye mchango wangu. Nachukua nafasi hii kuipongeza sana Serikali kwa kazi kubwa ambayo imefanya. Imeweza kufanya miradi mingi mikubwa ndani ya kipindi cha miaka mitano. Kwa kweli kazi inaonekana, kwanza kabisa imeweza kumtua mama ndoo kichwani kwa asilimia 90, pia imeweza kutengeneza barabara, umeme, mambo ya afya, sisi wanawake mpaka sasa hivi tumepata heshima kubwa sana, tunajifungulia sehemu nzuri. Kwa hiyo, Serikali imefanya mambo mengi mazuri na makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, palipo na mambo mazuri na makubwa hazikosekani changamoto. Mkoa wangu wa Rukwa unakabiliwa na changamoto kubwa sana kwenye Sekta ya Kilimo. Mkoa wa Rukwa ni miongoni mwa mikoa minne ambayo inazalisha kwa wingi sana chakula cha aina nyingi, lakini wakulima wamesahaulika sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima wa Mkoa wa Rukwa wanalima, lakini changamoto kubwa ni masoko. Naomba Serikali yangu Tukufu ya Chama Cha Mapinduzi, iwakumbuke sana wakulima hawa hasa wa mikoa minne ile ambayo inazalisha sana chakula kwa wingi. Kwanza kabisa, kuwatambua wakulima wadogo, wa kati na wakubwa, Serikali iweze kuwatambua na mahali wanapolima. Ikiwatambua, uwezekano wa kuwasaidia kuwapa mikopo itakuwa ni rahisi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia iwaletee wakulima Maafisa Ugani, kwani Maafisa hawa ni changamoto kwenye maeneo yetu. Mimi mwenyewe ni mkulima, lakini sijawahi kumwona Afisa Ugani akinitembelea hata siku moja kwenye shamba langu. Kwa hiyo, wakulima wanajilimia wanavyojua wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile Serikali kama Rais wetu alivyosema kwamba tunakwenda kwenye Tanzania ya Viwanda; tukianzisha viwanda vingi vya pembejeo, nadhani pembejeo pia zitashuka bei na wakulima watapata pembejeo kwa bei nafuu. Naiomba Serikali ijikite sana katika kuanzisha viwanda vya pembejeo ili wakulima nao wapate nafuu ya kupata pembejeo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine naomba kwenye mikoa ambayo inalima sana kwa mfano Rukwa, zingeanzishwa Benki za Kilimo ili wakulima waweze kujikopea wenyewe kwenye hizo benki, walime kilimo chenye tija. Hivi sasa wanahangaika sana, kwa sababu pembejeo zenyewe ni bei kubwa, kwa hiyo, utakuta wanapata shida sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni masoko. Naomba ile taasisiya NFRA ingeweza kuongezwa fedha. Ile inasaidia sana kwa sababu wakulima wakiuza mazao NFRA at least wanapata soko kidogo. Hata hivyo kwa mwaka 2020 kwa mfano kwa Mkoa wa Rukwa tuliambiwa NFRA watanunua milioni 50, matokeo yake walinunua tani 5,000 tu, kwa hiyo ikawa ni changamoto kubwa sana. Mpaka sasa hivi wananchi wale wanapata tabu sana, mahindiyako ndani, hawajauza hata kidogo. Kwa hiyo, naomba Serikali kupitia Wizara ijikite kuongeza fedha kwenye taasisi ile ya NFRA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)