Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Asia Abdulkarim Halamga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Mpango huu wa Maendeleo wa mwaka 2021/2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nachukua nafasi hii kuendelea kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kazi kubwa na nzuri ambazo anazifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kumpongeza Waziri wa Mipango pamoja na timu yake yote, bila kusahau Kamati ya Bajeti kwa hotuba yao nzuri waliyotuletea. Naomba nijikite kuchangia katika eneo la kilimo na hasa kilimo cha ngano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Manyara kupitia Wilaya ya Hanang ni miongoni mwa sehemu inayolima ngano kwa asilimia kubwa. Nikichukua takwimu za Serikali ambazo zimetumia fedha ya kwenda kununua ngano katika msimu uliopita, Serikali ilitumia zaidi ya shilingi trilioni 1.3 kwa ajili ya kununua zao hili la ngano na kuliingiza nchini. Nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitaweza kuipongeza Wizara ya Kilimo kwa kuamua sasa Wilaya ya Hanang kuwa kitovu cha kilimo hiki cha ngano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha kwamba sasa zao hili na kilimo hiki katika Mkoa wa Manyara, hususan Wilaya ya Hanang, tunaomba sasa Serikali ichukue hatua ya kuleta mbegu kwa wakati na kwa haraka kama ambavyo imetufanyia kwa sasa kutuletea tani 22 kwa ajili ya mbegu. Naiomba sasa Serikali kupitia mnunuzi ambaye iliamua awe Bakhresa kuja kununua ngano hizi za wakulima zaidi ya tani
477.8 ili wakulima hao waweze kukidhi kilimo chao kwa wakati na tuweze kwenda sambamba na uchumi wa viwanda kupitia malighafi watakazozitengeneza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Hanang ina ekari zaidi ya 100,000 ya kilimo cha ngano. Pamoja na ekari hizi, ekari 40,000 ziko kwa mwekezaji anayeitwa Ngano Limited. Tunaomba sasa, kwa sababu Serikali imeamua Hanang iwe kitovu cha ukulima cha ngano ili kuweza kukidhi mahitaji ya ndani ya nchi, mwekezaji huyu wa Ngano Limited mikataba yake iweze kuangaliwa kwa sababu anamiliki ekari zaidi ya 40,000 lakini halimi kiwango hicho cha ekari 40,000 na ekari hizo zilikuwa ni pori.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Hanang wanatamani kweli kulima ngano ili kukidhi haja ya Serikali, lakini tunaiomba Serikali kupitia Wizara ya Kilimo, iweze kumsaidia mwekezaji huyu mkataba wake, kwa sababu eneo alilonalo ni kubwa na limekuwa ni pori. Kama tumeamua kweli kuwekeza katika ngano, basi ikiwezekana shamba hilo liletwe katika halmashauri, halmashauri ilimiliki kwa maana ya Serikali au wananchi waweze kugaiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwekezaji huyu anamiliki eneo la Gidamocha, Sechet pamoja na Murjanda. Wananchi wanapoingia kulima hata kidogo tu, mwekezaji huyu anakwenda kuweka mazao sumu, mazao ya wananchi yanakufa, lakini pia halimi eneo hili la ekari 40; na lengo la Serikali ni kuhakikisha tunafikia…

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukuza uchumi, naipongeza Wizara ya Habari, Sanaa na Utamaduni kwa kazi kubwa ambayo inafanya, lakini naomba sasa Wizara ifike mahali iweze kuwasaidia wasanii wetu. Kwa sababu ni ukweli usiopingika, wasanii wanaingiza mapato. Vijana pamoja na ninyi wazee humu ndani mnapenda burudani, basi ifike sasa, Wizara iweze kuona ni namna gani inaweza kuwasaidia vijana hawa ku-promote kazi zao na hasa kimataifa ili wasanii hawa waweze kukubalika Kimataifa kama ambavyo Nigeria na nchi nyingine zinavyofanya. Wasanii wetu wana uwezo mkubwa wa kuliingizia Taifa letu pato kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania Mungu ametubariki sana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ajili ya muda, ndiyo nilikuwa nimeanza. Naunga mkono hoja. Naendelea kumshukuru Mwenyekiti wetu na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa huruma ya Serikali na hata leo Serikali hii kwa huruma yake, ina hadi watu ambao walifukuzwa kwenye vyama vyao, lakini Serikali kwa sababu imezingatia maslahi ya Watanzania imeweza kuwaweka humu ndani ili kuendelea kuchukua michango yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nasema tena, naunga mkono hoja. (Makofi)