Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri mwenye dhamana kwa ajili ya hotuba nzuri au mpango mzuri ambao amewasilisha kwetu. kabla ya kupoteza muda niseme naunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hayo, nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu leo hii nimepokea taarifa kutoka kwa Mkurugenzi kwamba amekubali ombi letu. Lipo ombi maalum ambalo tuliwasilisha kwenye ofisi yake kwa ajili ya kupata eneo la uwekezaji eka 4,000 pale Kwala. Mkurugenzi amenithibitishia kwamba barua tumepokea leo na tumepata eneo hilo. Naishukuru sana Ofisi ya Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na shukrani hizo, mimi nimejaribu kuupitia Mpango lakini pia nimesikiliza vizuri mchango wa Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti na namna ambavyo ameishauri Serikali juu ya kuongeza mapato yatakayoweza kusaidia ku-boost maendeleo ya nchi yetu. Kwenye maeneo hayo, yeye amejaribu kuoanisha uunganishwaji wa bandari ya Bagamoyo na matumizi ya reli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Kibaha vijijini lina reli mbili kubwa na ya tatu inakutana pale Mzenga; tuna reli ya kati, reli ya mwendokasi ambayo kwa wazo hili la Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti kama wataitumia bandari ya Bagamoyo kwa ajili ya kwenda kwenye reli zile maana yake lazima wataimarisha ujenzi wa barabara ya Bagamoyo – Mlandizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo na mimi niithibitishie Serikali maeneo haya ni muhimu kuendelezwa hasa ukizingatia kwamba pale Mlandizi kuna eneo la UFC ambalo limepimwa na Serikali viwanja kadhaa kwa ajili ya uwekezaji. Kwa hiyo, niiombe Serikali iwekeze nguvu kwenye maeneo haya kwa ajili ya kuongeza uchumi wa nchi hii kwa sababu wawekezaji watajenga viwanda katika maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, niipongeze pia Serikali tunao mradi wa bandari kavu pale Kwala na unaenda sambamba na ujenzi wa barabara kutoka pale Vigwaza – Kwala. Katika eneo hilo hilo pia ambapo mradi huo unaendelea ndiko ambako tumepewa eneo la eka 4000 kwa ajili ya kupima viwanja vya uendelezaji. Kwa hiyo, niiombe Serikali katika miradi hii ambayo wameiruhusu kufanyika, ni vizuri tukawekeza kwa haraka kwa sababu wawekezaji wakichukua maeneo hayo watakuwa wanaongeza pato la Taifa hili na kwa kufanya hivyo nchi hii itakuwa imeongeza uchumi na huu mpango ambao umekuja mbele yetu utatekelezeka kwa urahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tunafahamu kwamba Mkoa wa Pwani una viwanda vya kutosha. Katika Jimbo la Kibaha Vijijini tunavyo viwanda mbalimbali kikiwepo kiwanda kimoja ambacho kimetajwa kwenye hotuba hii cha Tan Choice. Kiwanda hiki kinashughulika na suala zima la uvunaji wa mazao ya mifugo, wanachinja ng’ombe 1,000 na mbuzi 1,000 kwa siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kiwanda kile wanakutana na changamoto mbalimbali na moja ya changamoto ni masoko. Niwaombe Serikali wawasaidie watu wale na nishukuru Waziri wa Mifugo alifika pale mwezi uliopita na aliweza kuwaona na walimpa hii changamoto. Kwa hiyo, niwaombe waweze kuwasaidia ile changamoto ambayo waliiwasilisha ili waweze kumaliza tatizo lao lile na waweze kufanyabiashara vya kutosha na kuingiza pesa kwenye nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo pia jambo moja ambalo nataka nilizungumzie, juzi hapa tumesikia Waziri wa TAMISEMI akiwaamuru au akiwaagiza Wakurugenzi baadhi ya vyanzo vya mapato waendelee kukusanya, hapa nataka nijaribu kutoa uzoefu kidogo. Watendaji hawa wa Kata ambao wamerudishiwa kazi hii ya kukusanya mapato ni watendaji ambao wana kazi nyingi kweli kweli. Kwa hiyo, kwa kuwaamini wao kuendelea kufanya na kazi ya ukusanyaji wa mapato tunaendelea kupoteza mapato kwa sababu wanaogopa kuifanya kazi hii na wengi wanadaiwa na wengine wana kesi mbalimbali mahakamani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali kwenye eneo hili, badala ya kuwalundikia mzigo Watendaji wa Kata kukusanya mapato haya hasa kodi za majengo, ardhi, mabango na mambo mengine, ni vizuri sana kama ambavyo wamechangia Wabunge wenzangu tungeweza kutafuta wataalamu maalum wanaoweza kusimamia ukusanyaji wa mapato, tukaiondoa kazi hii mikononi mwa Watendaji wa Kata ili waweze kuzifanya kazi hizo vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu gani watendaji hawa wamekuwa woga sana sasa hivi kwa sababu wana kesi mbalimbali zinawakabili juu ya ukusanyaji huu. Kwa hiyo, wanaweza wakategea wasiifanye kazi hii na mapato haya yasipatikane.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwahiyo ningeomba…

MWENYEKITI: Kengele imegonga Mheshimiwa, ahsante sana.

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)