Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Shamsia Aziz Mtamba

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Mtwara Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ili nami niweze kuchangia katika Mpango huu wa Maendeleo wa Taifa. Awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya nzuri na leo hii nikaweza kusimama katika Bunge hili, lakini pia nitoe shukrani zangu za dhati kabisa kwa wapiga kura wangu wa Jimbo la Mtwara Vijijini kwa heshima kubwa ambayo wamenipa na leo hii nikaweza kurudi tena katika Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, gesi inayotumika kuzalisha umeme Kinyerezi inatoka Mtwara katika Kijiji cha Msimbati, inapitia Madimba ndipo inaposafirishwa kuelekea Kinyerezi. Kwa mshangao mkubwa sana sehemu ambako inatoka gesi asilia, Msimbati, miundombinu ya barabara ni mibovu mno. Barabara ni mbovu haipitiki kabisa hasa kipindi hiki cha masika. Hivyo, niiombe Serikali katika Mpango huu wa Maendeleo irekebishe barabara hii muhimu ambayo inaleta uchumi wa Taifa, ijengwe kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wanaoishi katika eneo ambalo inatoka gesi wana mazingira duni sana. Hivyo, niiombe Serikali iwaangalie wananchi hawa kwa kuwawekea mazingira ya kuwaboreshea afya bora, elimu pamoja na uchumi kiujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wetu wa Mtwara na Kusini kwa ujumla Mwenyezi Mungu ametujalia tuna korosho nzuri na bora kabisa, lakini pia tuna gesi asilia, lakini pia tuna bandari kubwa ambayo ina kina krefu. Kwa masikitiko makubwa sana Bandari hii ya Mtwara haifanyi kazi ipasavyo ukilinganisha na Serikali ilivyotumia pesa nyingi kuwekeza katika Bandari hii ya Mtwara; haifanyi kazi, hii inanyima maendeleo kwa Taifa na maendeleo kwa watu wa Kusini kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi mwenyewe ni shahidi. Nikiwa natoka Mtwara naelekea Dar-es-Salaam natumia barabara, lakini napishana na malori njiani ambayo yamebeba simenti pamoja na korosho. Mizigo hii ingeweza kupitia katika bandari yetu ya Mtwara, lakini inatumia barabara. Hii inaleta uharibifu mkubwa wa barabara na inaipa Serikali jukumu kubwa la kuikarabati barabara hii mara kwa mara. Sasa niishauri Serikali katika Mpango huu ione umuhimu mkubwa sana wa kuitumia Bandari ya Mtwara ambayo italeta maendeleo kwa watu wa Kusini, lakini pia kwa Taifa kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka ya nyuma tulikuwa tunaziona meli nyingi zikifika katika bandari yetu ya Mtwara na vijana wengi wa Mtwara waliweza kupata ajira…

(Hapa kengele ililia)

MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuni… eeh, si nimesikia kengele?

MWENYEKITI: Ni kengele ya kwanza Mheshimiwa, bado ya pili.

MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe Serikali na niishauri kwa ajili ya Taifa kwa ujumla, ione umuhimu wa kuwekeza katika Bandari hii ya Mtwara ili iweze kufanya kazi ipasavyo. Bandari hii ingeweza kupata mizigo mingi kutoka Songea, Makambako, lakini pia na sehemu nyinginezo, wangeweza kuitumia bandari hii, leo hii hali ya maisha ya watu wa Mtwara yamekuwa magumu kwelikweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wengi walikuwa wanajipatia ajira katika bandari hii, lakini cha kushangaza bandari hii imetupwa kabisa, imesahaulika kabisa wakati bandari hii ina kina kirefu cha kupokea meli zaidi hata ya 15 au 20. Kwa hiyo, niiombe Serikali ione umuhimu wa kuitumia bandari hii. Ahsante sana. (Makofi)