Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Justin Lazaro Nyamoga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilolo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi hii. Nimepitia Mpango huu na ningependa kuchangia kwenye mambo machache kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ambalo ningependa kuchangia ni kuhusu mfumo wa kodi hasa kwa wafanyabiashara wa mazao mbalimbali ya misitu na mazao ya mbogamboga. Sheria ya kodi hii inamtaka kila mfanyabiashara mwenye mzunguko unaofikia shilingi milioni 14 basi awe na mashine ya EFD na kwa hiyo, haikuzingatia baadhi ya vitu ambavyo vinawakwaza wafanyabiashara. Nitoe mfano kidogo kwamba, wako watu ambao wanauza mara moja tu, kwa mfano wakulima wa miti ya mbao anachana mbao na anauza anaweza akapata milioni 30 na akapeleka mzigo wake au wafanyabiashara wa mazao wanaonunua kidogokidogo na mzigo unafika kwa kiwango hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuna utaratibu wa mageti ambapo yule mwenye mzigo akifika pale, basi anadaiwa risiti ya mahali alikonunua. Hii inatakiwa kurekebishwa kwa sababu kwa kufanya hivyo inawataka watu wengi sana ambao ni wakulima wa kawaida, watu wengi sana ambao ni wafanyabiashara wa mara moja, huo mzunguko wanaupata kwa haraka na sidhani kama tuko tayari kugawa mashine za EFD kwa wakulima, tuko tayari kugawa mashine za EFD kwa mtu anayechana mbao mara moja tu akauza. Irekebishwe ili iseme wafanyabiashara wa maduka au wafanyabiashara wenye sehemu ya kudumu kwa sababu, ndiko ilikolenga, lakini haiku-specify kwa hiyo, wale wa TRA wanapojaribu ku-execute wanasababisha usumbufu kwa baadhi ya wafanyabiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo ningependa kuzungumza ni ujenzi wa viwanda vya kimkakati. Juzi hapa nilitembelea kiwanda kimoja cha kutengeneza samani na kimejengwa na VETA kiko hapa Dodoma. Nikajiuliza sababu, iliyofanya VETA kujenga kiwanda hapa kwa sababu, ni cha samani; sikuona kama kuna misitu ya kutosha, kuna miti ya kutosha na hiyo ni taasisi ya umma. Ningeshauri viwanda vya kimkakati kama kile, laiti kama kingejengwa mahali kama Kilolo, Mufindi au Mafinga ambako kuna miti ya kutosha maana yake ni kwamba, hata shida ya madawati ingekuwa historia kwa sababu, kingeweza kufanya kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba hizi taasisi za umma, taasisi kama VETA na magereza ambao wanataka kuwekeza kwenye viwanda waangalie mazingira, hasa hivi viwanda vya samani. Sasa kwenye huu Mpango iangaliwe, tunaposema viwanda vya kimkakati basi vijengwe kule ambako mazao hayo yanazalishwa badala ya kuweka mahali kwa sababu ambazo huenda haziwezi kuleta tija kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kuzungumzia ni kuhusu barabara, hasa TARURA, ambalo limezungumzwa na watu wengi. Naunga mkono wale wanaosema kitafutwe chanzo kingine, uundwe Mfuko mwingine wa peke yake na tuangalie kwenye sekta ya mawasiliano, ili tupate fungu la kutosha, tuweze kutatua changamoto ya barabara kwa sababu, baada ya hapo hiyo ndio itakayokuwa mwarobaini wa matatizo tuliyonayo, ili pia TANROADS iweze kubakia na hela za kutosha kwenye Mfuko wake ilionao sasa, kwa sababu, kama tukigawa kwa kiwango kikubwa tutaifilisi TANROADS na itashindwa kufanya kazi tutarudi hapa tena kulalamika. Kwa hiyo, Mfuko mwingine ni muhimu ili kwamba, tusiifilisi TANROADS na TARURA itafutiwe chanzo kingine ambacho kitasababisha pato la Mfuko wa TARURA kuwa stable.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, ningependa kuzungumzia suala zima la ajira kwa vijana na kuweka mazingira wezeshi na rafiki. Watu wengi sana wanamaliza form four wanapata division four na wengine wanapata division zero na hao wengi hatujawawekea utaratibu wowote. Tukiendelea hivi ina maana kwenye vijiji vyetu na kwenye maeneo yetu kuna vijana wengi ambao hawajawekewa mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza vyuo hivi vya ufundi vitakapojengwa, vyuo hivi vya kati, viangalie taaluma maalum kwenye haya maeneo. Ikiwa ni maeneo kama kule kwetu basi ufundi wa kutengeneza samani, ufundi wa aina mbalimbali, lakini pia kufundisha masuala mazima ya kilimo na aina mbalimbali za kilimo zinazolimwa kwenye maeneo husika, ili wale vijana wanaopata division four na wanaopata division zero tusiwaache bila kuweka mpango maalum kwamba, maendeleo yao ya maisha yao yatakuwaje kwa sababu ni wengi na hao watakuja kuwa watu ambao hawana kitu chochote wanachoweza kufanya. Hilo ni janga ambalo kama tusipoliangalia si jambo zuri kwa maendeleo ya Watanzania.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Kengele imegonga, ahsante sana.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante san ana naunga mkono hoja. (Makofi)