Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. John Michael Sallu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Handeni Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. JOHN M. SALLU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Namshukuru Mwenyezi Mungu, namshukuru Mwenyekiti wa Chama chetu cha Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, nashukuru Chama chetu cha Mapinduzi, nashukuru wananchi wa Handeni Vijijini na wadau wote walionifanya niwepo hapa ili kuwatumikia wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli napongeza sana juhudi zilizofanywa katika kuandaa Mpango huu. Namshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Mpango kwa kuandaa Mpango mkakati utakaotutoa sehemu moja kwenda sehemu nyingine. Ndugu zangu si dhambi kushukuru na kupongeza juhudi zilizofanywa katika kuanzisha miradi mikubwa katika nchi hii ambapo ni msingi mkubwa wa maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa uchache wa muda, nitaanzia na bwawa kubwa la Stigler’s Gorge. Bwawa hili la Mwalimu Nyerere litazalisha umeme wa maji megawatt 2,115 ambapo ndiyo rahisi duniani kote. Kwa hiyo, utachagiza maendeleo makubwa kwa viwanda vyetu vikubwa, vya kati na vidogo. Hivyo, itatusaidia sana sisi wananchi wa Handeni Vijijini kuongeza thamani ya mazao yetu kwani sisi ni wakulima wazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na kuanzisha viwanda hivyo ambavyo tayari vimeshaanza na tuna mikakati ya kuvutia wawekezaji, vilevile maji na barabara ni muhimu. Ili mazao hayo yaweze kufika kwenye viwanda, ndugu zangu lazima tufanye mpango mkakati bajeti ya TARURA iongezeke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile viwanda vinaendana na maji. Naomba Wizara yetu ya Maji tukitoka hapa tuwe na mpango mkakati ili tuongeze pesa ili wananchi wetu wa vijijini wapate maji safi na salama na kuweza kuendesha mitambo hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni upanuzi mkubwa wa bandari zetu. Bandari zetu zimepanuliwa sasa lazima tutafute mbinu chochezi ziweze kufanya kazi zituingizie pato. Kwa mfano, wananchi wa Mkoa wa Tanga tumeshuhudia meli kubwa ya mita 200 ambayo ilibeba tani 55,000 za Clinker kwa ajili ya kwenda Rwanda. Meli hiyo iliondoka pale Tanga ikiwa tupu, sasa lazima tutafute mbinu chochezi ili bandari zetu ziweze kubeba mizigo kuingiza na kutoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Wizara ya Madini iweze kusaidia wachimbaji wetu wadogo wa chuma na madini ya viwandani kwani Handeni Vijijini tuna madini ya chuma na madini ya viwandani kwa wingi sana. Wachimbaji wadogo wamejitahidi, pale tuna takribani tani zaidi 50,000 imelala pale chini ambapo waliingia mkataba na Dangote lakini kwa bahati mbaya haijachukuliwa. Kama tungeweka mbinu chochezi basi tani hizo zingeondoka na meli hiyo na bandari yetu ingefanya kazi, Halmashauri ingepata siyo chini ya shilingi milioni 600, bandari yenyewe ingepata mapato siyo chini ya dola milioni 150 kwa sababu mzigo huo wa tani takribani 50,000 gharama yake ununuzi (FOB) huwa ni dola milioni 4. Kwa hiyo, ndugu zangu naomba tutafute namna chochezi Wizara ya Madini ikitusaidia ili tuweze kuwahudumia wachimbaji wetu hawa wadogo tuweze kuhamasisha uingizaji wa pesa kwa kutumia bandari yetu ya Tanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)