Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Agnes Elias Hokororo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa ni mara ya kwanza nianze kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyetujalia uzima. Pili, nitumie fursa hii kuwashukuru sana akina mama wa Mkoa wa Mtwara ambao wameniwezesha kurudi katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais wetu mpendwa, jemedari bingwa, Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa mafanikio makubwa yaliyopatikana katika Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Taifa katika maeneo yote; miundombinu, maji, elimu, afya na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze katika Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa. Mojawapo ya nguzo ya mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa kama ilivyoainishwa kwenye Mpango huo ni ukuaji wa uchumi na maendeleo ya watu.

Naiomba sana Serikali yetu Tukufu, ili kuwajumuisha wananchi wa Kanda ya Kusini, ni muhimu sana Mpango huu wa miaka mitano ukaingiza ujenzi wa reli ya Kusini. Kwa nini naiomba hii? Ujenzi wa reli ya Kusini ulitokana na Mradi wa Mtwara Corridor na mradi huu ulisainiwa na nchi nne; Tanzania, Msumbiji, Malawi na Zambia. Ulisainiwa mwaka 2000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, muasisi wake ni hayati mpendwa wetu Rais Mkapa. Lengo lake lilikuwa kuiwezesha Bandari ya Mtwara. Bandari ya Mtwara imejengwa kwa bilioni 157 lakini juzi swali liliulizwa hapa na Waziri alikiri kwamba Bandari ya Mtwara kwa sasa inafanya kazi chini ya kiwango. Kumbe mradi huu wa Reli ya Kusini ukitekelezwa ina maana Bandari ya Mtwara itafanya kazi ile iliyokusudiwa kwenye huu mradi na miradi ya EPZA ambayo kwa sasa bado haijaanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo naiomba sana Serikali, kwenye huu Mpango wa miaka mitano ioneshe waziwazi ni lini mradi wa ujenzi wa reli ya Kusini utaanza na kukamilika ili kuwajumuisha wananchi wa Mikoa ya Ukanda wa Kusini katika ukuaji wa uchumi na maendeleo yao. Vinginevyo tutakuwa tu tunaendelea kushangilia lakini wananchi wa Ukanda wa Kusini kama maeneo haya muhimu katika ukuzaji wa nchi yetu hayatajumuishwa na wao watakuwa wanaendelea kushuhudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua kabisa kwamba Serikali imeanza kutekeleza sehemu ya Mradi wa Mtwara Corridor, kama vile ujenzi wa barabara ya kutoka Mtwara mpaka Mbambabay umetekelezwa, lakini pamoja na huo ujenzi wa bandari, pamoja na upanuzi wa uwanja wa ndege, lakini pia pamoja na ujenzi wa Daraja la Umoja lile linalounganisha Tanzania na Msumbiji, lile Daraja la Mtambaswala. Sasa mambo haya yote ambayo Serikali ya Awamu ya Tano na zile zingine imeyatekeleza, hii miradi itaendelea kulala kwa sababu shughuli za kiuchumi zinategemea kwa kiasi kikubwa ujenzi wa mradi wa reli ya Kusini. Naamini Serikali yetu Tukufu itaweza kujumuisha Mradi wa Ujenzi wa Reli ya Kusini ili na sisi tuweze kushiriki kikamilifu katika ile dhana ya uchumi jumuishi, uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nijielekeze katika eneo la kilimo. Kama ambavyo mpango umeainisha kwamba asilimia 65 ya Watanzania wanapata riziki yao kwa kutegemea shughuli za kilimo. Lakini tunaona shughuli za kilimo zinachangia asilimia 27 tu ya GDP na asilimia 24 ya total export.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nini kinahitajika katika eneo hili; kwa kuwa wananchi wa Mikoa ya Kusini, hasa Mtwara, asilimia 98 ni wakulima, ili tujumuike pia katika ujenzi wa uchumi huu ambao wote tunauhitaji, naomba sana tujikite katika mapinduzi ya kiteknolojia. Wakulima wetu kwa sasa wanatumia jembe la mkono; kwa nini? Trekta ziko bei juu, milioni 45 mpaka milioni 60. Akinamama ambao wanashiriki kwa asilimia 75 kule mashambani na katika shughuli za kilimo hawawezi kununua trekta, mikopo yetu ya vikundi vya halmashauri...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa. Kengele imeshagonga.

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja. (Makofi)