Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. ENG. ISACK A. KAMWELWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia Mpango huu wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu Mwingi wa Rehema na upendo hasa kwetu sisi Watanzania, kwa kutufanya tuendelee kudumisha amani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru uongozi wa Chama cha Mapinduzi katika ngazi zote kwa kuendelea kuliteua jina langu ili niingie kugombea. Pia niwashukuru wananchi wenzangu wa Jimbo la Katavi ambao wamenirejesha kwa mara nyingine ya pili katika Bunge hili.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niipongeze sana Wizara ya Fedha kwa Mpango mzuri lakini nitoe ushauri kwa upande wa TRA. Mpango wa Pili wa Maendeleo uliweka makadirio ya kukusanya shilingi trilioni 107 na niipongeze sana TRA wamekusanya zaidi ya asilimia 80. Ni kazi nzuri hongereni sana lakini ni kwa sababu ya usimamizi mzuri wa Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha hiyo katika miaka mitano imefanya kazi kubwa sana lakini ni imani yangu kwamba wangeweza kukusanya Zaidi. Kwa kuzingatia kwamba kwenye Mpango huu wa Tatu unaoanza mwaka 2021 kwenda 2022 matarajio ni kukusanya shilingi trilioni 114 kwa ajili ya kutekeleza mipango ya maendeleo kwa muda wa miaka mitano mingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashauri TRA, ni lazima wadumishe uhusiano kati ya TRA kwa maana ya Serikali na wafanyabiashara. Wabunge wenzangu wamechangia kwamba wafanyabiashara watatu wanakwenda kununua bidhaa moja China lakini makadirio ya TRA yanatofautiana katika yale makontena matatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni rahisi na kwa bahati nzuri Serikali yetu imeshaweka mkongo wa Taifa, teknolojia ya kidigitali tunayo, tunaweza tuka-transfer fedha kwa kutumia teknolojia ya kidigitali. Badala ya wafanyabiashara kutembea na dola mfukoni kwenda China kununua bidhaa, kwa nini tusifanye benki transfer? Tukifanya benki transfer na rekodi zikawepo TRA ukadiriaji hauwezi kuchukua muda, tutakwenda haraka na mlundikano wa makontena ndani ya bandari unaweza usiwepo tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi navyoongea kuna watu wanakimbia mizigo yao kwa sababu analeta mzigo lakini makadirio yanakuwa makubwa kuliko ile fedha aliyonunulia na ile mizigo inaendelea kurundikana bandarini. TRA wanayo sheria baada ya siku 14 wanatakiwa kuweka ule mzigo katika mnada lakini hilo halifanyiki. Niwashauri sana TRA, ili muweze kukusanya fedha nyingi tuwe na mahusiano mazuri. Niombe tu, ikiwezekana hata Bunge litunge sheria kwamba sasa manunuzi ya bidhaa kutoka nje lazima fedha ipelekwe kwa benki transfer badala ya kuweka mfukoni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hii miaka mitano, Mheshimiwa Dkt. John Magufuli, kutoka ndege moja amenunua ndege sasa zimefika kumi na mbiliā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ENG. ISACK A. KAMWELWE: Oooh! Muda umeisha. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. ENG. ISACK A. KWAMWELWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)