Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Ally Mohamed Kassinge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nikushukuru kwa nafasi, lakini pia kwa sababu nachangia kwa mara ya kwanza, nami nitumie fursa hii kuanza kwa kumshukuru Allah Mwenyezi Mungu Subhanah Wataala, lakini pia kuishukuru familia yangu, wapigakura wangu wa Jimbo la Kilwa Kusini, pamoja na Chama changu Chama Cha Mapinduzi kilichonipa dhamana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukrani hizo naanza kuchangia nikianzia na sekta ya viwanda. Sekta ya Viwanda katika nchi yetu ipo malighafi ambayo bado hatujaweza kuitumia na hapa nazungumzia malighafi ya gesi asilia. Katika Wilaya ya Kilwa eneo la Songosongo tunazalisha gesi pale ambayo inatumika kuzalisha umeme au kufua umeme, lakini mabaki yanayotokana na gesi asilia bado hayajaweza kutumika kwa ajili ya viwanda na hapa nazungumzia viwanda vya mbolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri kupitia Mpango huu Kiwanda cha Mbolea Kilwa Masoko kitakachotokana na malighafi ya gesi asilia kiingie katika Mpango huu tunaoenda kuutekeleza kwa ajili ya maendeleo ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, nije kwenye Sekta ya Kilimo; eneo mahususi ambalo tutawasaidia wakulima wetu ni kuhusianisha kilimo pamoja na Sekta ya Viwanda. Mosi, viwanda vya kuwawezesha wakulima wetu kupata mbolea kwa urahisi vianzishwe karibu na maeneo ambayo viwanda hivyo vitawasaidia wakulima kwenye maeneo husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Nyanda za Juu Kusini ambapo kwa kiwango kikubwa wenzetu ndiyo wakulima wakubwa wanaozalisha kwa ajili ya kulisha nchi na ziada mpaka tunaambiwa kwamba kuna chakula au mahindi yamebaki huko yamekosa soko, nashauri kupitia Mpango huu kuanzishwe kiwanda cha mbolea Wilaya ya Wanging’ombe, Mkoani Njombe ambapo tayari wananchi wametoa eneo la kutosha. Kwa kufanya hivyo tutaweza kupunguza changamoto ya pembejeo ya mbolea katika msimu wa kilimo. Wizara ya Kilimo itakuwa inapunguza kazi ya kutoa bei elekezi kwa sababu ya mbolea inayotokana na sekta binafsi, tukianzisha kiwanda pale tutasaidia Mikoa ya Njombe, Mbeya, Iringa, Ruvuma na Katavi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kuna eneo la sekta ya uvuvi, Mpango unaelezea suala zima la uvuvi katika kuanzisha bandari za uvuvi lakini hii iende sambamba na masoko ya samaki. Wilayani Kilwa hususani Kilwa Kivinje ni miongoni mwa maeneo ya uzalishaji mkubwa wa sekta hii ya uvuvi ikiwa ni pamoja na Mafia. Nashauri kupitia Mpango huu tuanzishe bandari za uvuvi Kilwa Masoko na Mafia na tuanzishe soko kubwa la samaki pale Kilwa Masoko kwa sababu nchi jirani na hususani Congo wanakuja kununua samaki tani kwa tani lakini Serikali hatujaweza bado kuratibu eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya mchango huu, naunga mkono Mpango huu na nashauri upitishwe kwa mujibu wa mapendekezo tunayoyatoa Wabunge hapa Bungeni. (Makofi)