Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nami nitumie nafasi hii kukishukuru sana Chama changu cha Mapinduzi na wananchi wa Jimbo la Korogwe Vijijini kwa kura nyingi na za heshima walizotoa kwa chama chetu na kuniwezesha nami kuwa mwakilishi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma vizuri mapendekezo ya Mpango, nimesoma vizuri mpango huu, naipongeza Serikali kwa kazi kubwa na hatua kubwa ambayo tumepiga mpaka sasa. Ila nilipokuwa nasoma Mapendekezo ya Mpango huu wa Awamu ya Tatu kwenye ukurasa wa 87 nimekutana na vipaumbele pale viko vitano. Ukisoma kuanzia kipaumbele cha kwanza, cha pili na cha tatu, huoni namna ambavyo unaweza ukaikwepa sekta ya kilimo kwenye kuendeleza na kukuza uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri sana Serikali, kwenye suala la kilimo, tunayo mambo mengi sana ya kufanya na mengi yameshazungumzwa, mimi naomba nizungumzie sana eneo la soko. Ni lazima Serikali ijitahidi kuweka uhakika wa masoko kwa wakulima wetu wanaolima kwenye nchi yetu hii. Tukiweka uhakika wa masoko tutasaidia viwanda vyetu, tutatengeneza ajira, tutaongeza pato kwa wale wakulima wanaolima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi tulikuwa tunamwuliza Waziri Mkuu kuhusu mkakati tulionao kwenye mazao ya kimkakati, nikatoa mfano wa zao la mkonge. Wananchi wameitikia na wanalima sana, lakini tusipokuwa na uhakika wa soko kwa ajili ya mazao haya, mwisho wa siku wananchi watakuja kuishia kupata hasara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya njia ya kuweka uhakika wa soko ni kutengeneza viwanda na kushawishi wawekezaji kuwekeza kwenye sekta ya viwanda. Tunavyo viwanda kwa mfano kwenye zao la mkonge, tulikuwa na viwanda vya magunia, sasa hivi havifanyi kazi vizuri. Asubuhi kuna mtu amezungumza hapa kwamba wale wawekezaji ikiwezekana wanyang’anywe lakini ni lazima tujiulize hivi viwanda vya magunia vilikwama wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mahitaji ya magunia ni makubwa sana, lakini uzalishaji wa magunia ni mdogo, kwa nini? Ni gharama za uzalishaji. Siyo hivyo tu, pia magunia yetu yanakumbana na ushindani kutoka kwenye magunia yanayozalishwa kwa kutumia mazao mengine na bidhaa nyingine kama jute. Ukiangalia India na Bangladesh, wao wana subsidy kwenye jute na wanajitahidi sana kuwekea mfumo mzuri wa kununua mazao yale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia East Africa Community, Sheria za Ushuru wa Forodha zinatoa nafuu ya kodi kwa bidhaa ambazo zinaingia kwa ajili ya kuchukua mazao na kutoa bidhaa na kuzipeleka nje kwa ajili ya ku-export. Haya yote ukiangalia yanafanya magunia ya jute yanakuwa na bei rahisi wakati magunia yanayozalishwa na mkonge yanakuwa na bei kubwa. Ukienda kwenye ushindani hatuwezi kupata faida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze jambo linguine, tumejiwekea malengo, tumepiga hatua kidogo kwenye umwagiliaji na tumejiwekea malengo mpaka 2025 tufike hekta 1,200,000. Naiomba Serikali, lazima tuangalie miradi mikubwa ya umwagiliaji itakayotusaidia kuweza kuhudumia eneo kubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mheshimiwa Naibu Waziri wa Kilimo tulikuwa nao Tanga, Bwawa la Mkomazi, mradi mmoja tu una uwezo wa kuhudumia hekta zaidi ya 6,000, lakini kwa zaidi ya miaka 10 wananchi wamekaa na matumaini wanasubiria miradi hiyo haitekelezwi. Naomba tuweke nguvu kwenye maeneo ya namna hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni la miundombinu. Kilimo kinafanyika vijijini, lakini miundombinu ni mibovu sana. Leo tunasema tuongeze uzalishaji kwa kuongeza maeneo ya kulima, lakini Mheshimiwa Naibu Waziri wa Kilimo na Waziri wa Kilimo wanajua, kwenye chai peke yake kwa mwaka, zaidi ya kilo milioni nne tunazipoteza, zinachelewa kufika kiwandani kwa sababu ya miundominu na zinapotea. Thamani yake ni karibu shilingi bilioni 2.8 kwa sababu ya miundombinu. Naungana na Mheshimiwa Nditiye, tunahitaji kuwa na nguvu na mkakati wa ziada kwenye suala la miundombinu, kutafuta fedha kuiongezea TARURA ili wananchi wetu wapate uhakika wa kupeleka mazao kwenye masoko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na ninaunga mkono hoja. (Makofi)