Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia mipango hii ya maendeleo ambayo ni muhimu sana kwa Taifa letu. Niwashukuru pia wale wote ambao wameweza kutambua juhudi za Serikali katika kuleta maendeleo katika Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kueleza kwamba asilimia 75 mpaka 80 ya Watanzania wanaishi kijijini na ni maskini. Tushukuru Serikali kwa kutuingiza kwenye uchumi wa kati ila pia tuiombe iongeze fursa, kazi ya Serikali ni kuandaa mazingira mazuri ya biashara ili watu waweze kupata kipato na pato la Taifa liweze kukua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo pia nimshukuru dada yangu, Mheshimiwa Balozi Dkt. Pindi Chana, amezungumzia changamoto ya bei ya mbolea. Ni kweli; kwa mfano kule kwetu Ludewa mfuko mmoja wastani unauzwa kati ya 56,000 mpaka 65,000 na kwa ekari moja mkulima anatumia mifuko siyo chini ya minne ambapo mavuno yake anapata sanasana roba kumi. Sasa akija kuuza hizi roba kumi, roba moja shilingi 40,000, kwa hiyo anapata mapato ya shilingi 400,000 wakati amewekeza gharama zaidi ya shilingi 400,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tuangalie namna sasa, nashukuru Mheshimiwa Waziri wa Kilimo amekaa na wataalam wa kilimo na kuweka mikakati. Hii ni ishara njema na nimwombe yale ambayo ameahidi aweze kuyatekeleza kwa sababu Wabunge wengi humu tunatokea maeneo ambapo wananchi wetu ni wakulima na wanategemea hasa jembe la mkono. Kwa hiyo naamini atawatoa jembe la mkono wakulima wale ambao asilimia kubwa wako vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na vituo vya utafiti, lakini vituo hivi vijengewe uwezo zaidi ili viweze kutoa taarifa nzuri na taarifa hizi zisibaki kwenye makabrasha, wawashirikishe wataalam wa kilimo kwenye halmashauri zetu, zinaweza kusaidia katika kuongeza tija. Vile vile kwenye ile mikoa yetu ambayo inajishughulisha na kilimo kungekuwa na vituo ambavyo vinafanya uchunguzi wa udongo, zile maabara. Kwa sababu mwananchi anaweza akawa anatumia mbolea ambayo saa nyingine haihitajiki kwenye udongo wa eneo husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulivyokuwa kwenye Mkutano wa RCC Njombe, watu wa madini waliwasilisha taarifa kwamba Wilaya ya Ludewa ina leseni 104 za madini ambazo hazitumiki zimekuwa zikihuishwa tu. Kwa hiyo waliomba kwamba kwa kuwa eneo hili linaweza kutoa ajira nyingi kwa Watanzania na Wanamkoa wa Njombe na kanda nzima ile ya nyanda za juu; leseni hizi ziweze kufutwa, maeneo haya yagawiwe kwa wachimbaji wadogo ili waweze kuongeza kipato chao na kipato cha Taifa kiongezeke. Namshukuru Mheshimiwa Waziri, aliahidi kwamba atalishughulikia na atafanya ziara Ludewa; nimshukuru sana. Wananchi wa Ludewa wanamsubiri kwa hamu kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile wanaomba kwenye eneo la makaa ya mawe pale kuna leseni kubwa mbili ambazo zote zimeshikiliwa na Serikali. Sasa si halmashauri mapato pale ni hafifu sana, milioni 800 na sisi tulitamani Mheshimiwa Waziri wa Madini angetumegea kidogo halmashauri pale tuweze kuwekeza kwenye uchimbaji ili pato letu la halmashauri liinuke, tuweze kuhudumia wananchi. Tukihudumia vizuri wananchi maana yake watakuwa na kipato kizuri watafungua biashara na Serikali itapata mapato kupitia kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa Sheria ya Kodi ya Mapato, TRA. Kuna kodi moja inaitwa Capital Gain Tax; mwananchi anavyonunua au kuuza ardhi hii kodi inatozwa kwa mujibu wa Sheria ya Mapato ya Mwaka 2004. Kodi hii siyo rafiki, wananchi wengi ambao wananunua ardhi wanashindwa kuhamisha umiliki wa viwanja vyao. Kwa hiyo naomba iangaliwe vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)