Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nitumie fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, lakini nimshukuru Mheshimiwa Rais ambaye ni Mjumbe namba moja wa Chama Cha Mapinduzi na wajumbe wengine kwa kupendekeza jina langu kurudi kwenye kinyang’anyiro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikishukuru sana Chama changu Cha Mapinduzi kwa sababu ndicho chama kinachotekeleza ilani na mambo yanakwenda vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilimsikia dada yangu Mheshimiwa Halima akipongeza watu mkawa hamumuelewi. Amesema Awamu ya Tano yapo yanayofanyia mazuri, ndicho alichosema, msipate shida sana, wataelewa tu, wamekuja na wataendelea kuja wala msipate shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, rasimu hii ya Mpango iliyoletwa kuna mambo ambayo at least nataka niishauri Serikali. Ukisoma maelezo ya rasimu ya Mpango wa 2021 na ile yenyewe ya 2021-2026, kwenye suala la kilimo ambalo tumelizungumza na mimi nagusa sana kilimo kwa sababu asilimia 98 ya jimbo langu ni wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Waziri wa Mipango, tunapokwenda kuileta bajeti yenyewe ya mpango kabisa Wizara yetu ya Kilimo ambayo ukisoma Bajeti ya mwaka 2019/2020 ilitengewa asilimia moja tu ya bajeti kuu. Kilimo ambacho kwa maelezo yenyewe ya mpango yanasema kinaajiri watu zaidi ya asilimia 65, sasa reflection yake Watanzania wanaotegemea kilimo ni wengi bajeti inayokwenda kwenye kilimo ni ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukienda kusoma hotuba ya Mheshimiwa Rais ambayo amekielezea kilimo kwa mapana yake sana ukurasa ule wa 13 ameelezea vizuri sana. Nami hapa nataka Waziri wa Kilimo anisikilize vizuri sana. Mwaka 2017/2018 waliondoa fedha ya export levy ambayo ilikuwa inawapelekea wakulima pembejeo. Rais kwenye ukurasa huu wa 13 ametoa maneno ambayo nadhani Wizara ya Kilimo wana kitu cha kufanya na nataka ninukuu ili yawe mwongozo kwa Wizara. Mheshimiwa Rais anasema; “Kwa msingi huo, kwenye kilimo tunakusudia kuongeza tija na kukifanya kilimo chetu kuwa cha kibiashara. Lengo ni kujihakikishia usalama wa chakula, upatikanaji wa malighafi za viwandani na pia kupata ziada ya kuuza nje. Ili kufanikisha hayo tutahakikisha pembejeo na zana bora za kilimo ikiwemo mbegu, mbolea na viuatilifu vinapatikana.” (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa Wizara wanatakiwa waende kwenye extra mileage na ndiyo maana tunataka mpango u-reflect na bajeti zao. Mheshimiwa Rais ameshaonesha dira hii kubwa, hii dira iwafanye watu wa kilimo sasa, kwa wakulima wetu tatizo la pembejeo tuone limekwisha, wakulima wetu tuone suala la dawa limekwisha. Rais amekwenda mbali mpaka matrekta, matrekta haya ya wakulima yanaishia mijini tu. Ukienda vijijini hakuna mtu anajua trekta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Wizara ya Kilimo waende mbali zaidi. Hii nchi ina ardhi ya kutosha. Wakulima hawa wanapaswa sasa waache kutumia jembe la mkono. Tunapokwenda kwenye uchumi wa kati wa viwanda ni lazima twende mbali ambako wakulima tutawasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye kilimo hiki zao la korosho ndiyo zao pekee duniani lenye makato makubwa na mengi kuliko zao lingine. Sasa Wizara hapa wana jambo la kutusaidia. Kwenye korosho peke yake mapato yanafika 745, ukiacha hayo ambayo wanayaona kwenye mjengeko wa bei wa 226, lakini ukienda ukaangalia export levy, ukaenda ukaangalia ndani kuna waendesha maghala shilingi 38. Jumla ya makato tu kwenye korosho ni zaidi ya 745, hakuna zao lolote Tanzania ambalo lina makato makubwa kama korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima wafike mahali waone kwamba wakulima hawa wa korosho waende kwenye makato wanayoyakata kwenye pamba, alizeti, mahindi kuliko mzigo huu mkubwa. Tutaendelea kulalamika bei ya korosho ni ndogo kumbe makato makubwa wanayachakata Serikali. Tuone namna ya kuendelea kuyapunguza makato ya wakulima hawa kwa sababu yamekuwa mzigo mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, Mheshimiwa Rais alivyokuja kwenye kampeni alishatuahidi watu wa kusini, kuna barabara ile ya kutoka Mtwara – Nanyamba – Tandahimba – Newala na ipo ndani ya Ilani ya Chama Cha Mapinduzi. Tuone sasa tunapokwenda kwenye bajeti barabara hizi zinatengewa fedha za kutosha ili tunapofika 2025, story ya barabara kwa eneo lile iwe imekwisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la maji; tumekuwa kwenye tatizo la maji kwa muda mrefu sana. Kuna wakati amekuja Makamu wa Rais akatuahidi tungepata fedha za Mradi wa Maji wa Makonde. Badala yake tumerudi hapa miaka mitano Mradi wa Makonde umesogezwa umekuja kwenye miji 28. Tuone sasa Serikali inatenga fedha kwa ajili ya Mradi wa Maji wa Makonde.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.