Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Nami nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu lakini nikishukuru Chama cha Mapinduzi na wananchi wa Jimbo la Lindi Mjini kuniwezesha kurudi tena katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Waziri, Mheshimiwa Dkt. Mpango kwa kutuletea Mpango wa Miaka Mitano wa Maendeleo ya Taifa. Pamoja na hayo, amefanya kazi nzuri kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita katika kuhakikisha kwamba tunakuza uchumi wa taifa letu. Hakuna asiyejua, kila mmoja anajua kazi kubwa iliyofanywa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nichangie Mpango wa Taifa wa Miaka Mitano. Mpango huu umeweka kipaumbele katika kukuza uchumi wa bahari pamoja na uvuvi. Mwenyezi Mungu ametujaalia nchi yetu tuna bahari na maziwa. Eneo la bahari tuna kilomita za mraba 64,500 lakini upande wa maziwa tuna kilomita za mraba 62. Katika maeneo haya ndiko kunapatikana samaki na ufugaji wa samaki, kilimo cha mwani, uzalishaji wa madini ya chumvi, gesi na mafuta, utalii wa fukwe za bahari pamoja na michezo mbalimbali ya bahari. Katika uwekezaji huu wa blue economy, eneo hili La bahari ni la Muungano, naomba kuishauri Serikali kuhakikisha kwamba tunazipitia sheria pamoja na miongozo na kanuni ili tuweze kufanya kazi vizuri katika kuhakikisha kwamba tunakwenda kutekeleza miradi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Serikali kuhakikisha kwamba tunakwenda kusimamia uchumi huu wa bahari. Tunahitaji kuwa na wataalamu wenye kujua na wenye uzoefu ili tuweze kukuza uchumi huu wa bahari. Niishauri Serikali kupeleka wataalam wetu nje ya nchi kwenda kusoma ili waweze kupata ujuzi mzuri tuweze kuja kutekeleza haya ambayo tunayakusudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hayo, tunahitaji pia uendelezaji wa sekta hii ya bahari uende sambamba na uwekezaji wa miundombinu yake. Tunahitaji kujenga bandari kwa ajili ya shughuli za usafirishaji na uvuvi. Hatuwezi kutumia bandari ya Dar es Salaam, leo inashusha mzigo wa sulphur halafu kesho inashusha samaki, hapana haiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna kila sababu ya kuhakikisha kwamba Serikali yetu inaendelea kujenga bandari zitakazotumika kwa shughuli za uchumi huu wa bahari. Tunaweza kupanua na kujenga bandari kule Bagamoyo lakini tukajenga bandari kule Mkoani Lindi. Kwa kufanya hivyo, tutakuwa tumepanua huduma hii ya bandari na kuendelea na uwekezaji huu wa uchumi wa bahari. Pia tunahitaji meli zinunuliwe ambazo zitakwenda kufanya kazi katika kuhakikisha kwamba uchumi wetu unakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo tungeweza kujenga chuo ambacho kitakwenda kusimamia masuala mazima ya uchumi wa bahari pamoja na uvuvi. Pale Lindi tuna maeneo mengi ya ardhi na tuko tayari kutoa ardhi kwa ajili ya ujenzi wa chuo hiki. Kwa hiyo, naishauri Serikali kujipanga vizuri katika kuhakikisha kwamba tunakwenda kusimamia uchumi huu kwa ajili ya kuongeza kipato cha nchi yetu ili tuweze kuwahudumia wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, rasilimali ya bahari tunayo na rasilimali watu tunayo na Watanzania tuna afya nzuri ya kufanya kazi. Ni sisi Serikali sasa kujipanga katika kuhakikisha kwamba tunakwenda kukuza uchumi huu wa bahari pamoja na uwekezaji kwenye eneo la uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inasikitisha kuona Waziri anapokuja kutoa taarifa yake ya kazi ya kipindi cha mwaka mmoja na kuonyesha kwamba mapato ya Wizara yake yameongezeka kwa kutoza faini, hii siyo sahihi. Tunategemea Mawaziri wasimamie tuone mapato yanaongezeka kupitia miradi ya kimkakati katika kuhakikisha kwamba tunakwenda kukuza uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)