Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Dr. Amandus Julius Chinguile

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nachingwea

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye Mpango wa Serikali. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia na mimi kuwa mmoja wa Wabunge wa Bunge hili la Kumi na Mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nikishukuru sana Chama changu Cha Mapinduzi kwa kunipa nafasi ya kuwa mgombea na hatimaye kuchaguliwa na wananchi wa Jimbo la Nachingwea kwa kura nyingi za kishindo.

Nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, Mwenyekiti wetu wa chama kwa kazi kubwa aliyoifanya akisaidia na Mheshimiwa Makamu wa Rais na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Wamezunguka nchi nzima kunadi Ilani ya CCM wakishirikiana na viongozi wetu waandamizi wa chama na hatimaye Wabunge wengi tukarudi ndani ya Bunge, wengine kwa mara ya kwanza kwa kishindo kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawashukuru sana. Wengi tumeingia ni kwa matumizi hayo, kwa harakati hizo za viongozi wetu wakuu, lakini zaidi ya hayo kutokana na kazi nzuri iliyofanywa ya kutekeleza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi na comrade wetu, jemdari wetu, Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Pamoja na kazi hiyo nzuri, pamoja na pongezi hizo ambazo nimempatia Mheshimiwa Rais, sasa nijielekeze kuchangia kwenye Mpango huu wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye halmashauri nyingi ikiwemo ile ambako mimi natokea, uchumi wetu ni kilimo. Pamoja na Serikali imeelekeza hapa maelekezo yake kwamba, itawekeza zaidi na kuimarisha upatikanaji wa pembejeo, bado nishauri kuna migogoro mingi ambayo iko kwenye maeneo mengi na hasa wafugaji na wakulima. Nikitolea mfano kwa Jimbo langu la Nachingwea kuna mwingiliano mkubwa baina ya wafugaji na wakulima. Niishauri Serikali tutenge maeneo maalum yatakayowawezesha wafugaji kwenda kukaa kwenye eneo ambalo sasa litakuwa na miundombinu yote kwa maana ya maji na malisho badala ya kufanya ufugaji wa sasa wa kuhamahama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, tunapokuwa tunazungumzia kilimo ni eneo mtambuka, wakulima wetu wengi wanalima kilimo cha kizamani sana, wanatumia jembe la mkono. Kwa kweli katika hili niiombe sana Serikali iwekeze vya kutosha ili wakulima wetu waondokane na kilimo kile cha kizamani, waende sasa kuingia kwenye kilimo cha kisasa. Katika eneo hilo basi tuongeze kwenye rasilimali watu kwa maana ya wale wataalamu wetu wa kilimo waende zaidi kwenye vijiji vyetu, wakatoe elimu zaidi na kuwasaidia wakulima wetu ili waweze kulima kilimo cha kisasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania yetu ni Tajiri, tuna madini, lakini tuna maliasili ya kila namna, Mwenyezi Mungu ametujalia sana. Katika hili yako maeneo ambayo bado hatujayafanyia kazi kwa upande wa madini. Nikitolea mfano kule kwetu eneo la Nditi, Kiegeyi, bado tumeomba vibali, tumeomba leseni ya uchimbaji kwenye maeneo yale, lakini bado Wizara haijatilia mkazo . Nashukuru Mungu nilizungumza na Mheshimiwa Waziri wa Madini akaniahidi atatembelea kule Nachingwea…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Kengele imegonga Mheshimiwa.

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)