Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Zaytun Seif Swai

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza kabisa naomba nimpongeze Waziri wa Fedha kwa uwasilishaji uliotukuka wa rasimu ya mpango. Mimi binafsi kama Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bajeti pamoja na wenzangu tulipokea mapendekezo yale na tuliyafanyia uchambuzi wa kina. Nashukuru na pia, naipongeza Serikali kwa kuchukua mawazo yet una kuyajumuisha katika rasimu ile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wowote ule unahitaji rasilimali fedha na Waheshimiwa Wabunge hapa wameongea mambo mengi sana ya kimkakati, jinsi gani tutapata fedha kwa ajili ya kuwezesha Mpango wetu utekelezeke kwa kiwango cha juu. Naomba nijikite kwenye suala la udhibiti wa mapato. Mambo yote haya yaliyoongelewa na Wabunge mambo mazuri yatakuwa hayana maana sana kama tutashindwa kudhibiti mapato yetu tutakayoyapata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee suala la GePG, yaani Government Electronic Payment Gateway. GePG ni mfumo wa Serikali wa kukusanya mapato kielektroniki. Naweza kusema kwamba, Serikali imeshindwa kudhibiti mapato yetu kupitia mfumo huu kwa kiasi kikubwa. Ni kweli, mfumo huu umeisaidia Serikali kuongeza mapato yake, lakini vilevile inabidi tuufanyie kazi zaidi kuhakikisha tunadhibiti mapato yetu mpaka mwisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali yetu tumewaamini na tumewaachia sekta binafsi watusaidie kukusanya mapato haya, hususan sekta ya simu, makampuni ya simu na mabenki mbalimbali, lakini inavyoonekana makampuni haya binafsi yamewekeza sana kwenye rasilimali watu pamoja na teknolojia ukilinganisha na wafanyakazi wa Serikali wanaohusika moja kwa moja na mifumo hii. Kwa hiyo, kuna mwanya mkubwa sana hapo wa kupoteza mapato kwa sababu ya tofauti ya kiufahamu wa mifumo hii. Naishauri Serikali iweze kuwekeza kwa rasilimali watu na teknolojia kwenye mifumo hii ili basi tuweze kuitumia mifumo hii kwa ufasaha na ufanisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia niongelee suala la mawasiliano. Naweza kusema kwamba, sekta hii ya mawasiliano ni moja ya sekta ambazo zinachangia kodi kubwa na uchumi wa nchi hii, lakini Serikali yetu sijaona jitihada zake za dhati kuisaidia sekta hii ili iweze kukua zaidi na Serikali iweze kukusanya mapato zaidi kwa sababu mbalimbali, ikiwemo kodi kubwa, tozo mbalimbali na masharti mengi yanayowekewa sekta hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naweza kutolea mfano tu, kuna maeneo mengi ya vijijini, kwa mfano kule Longido kuna Kata ya Nondoto Matale, hata Wilaya ya Meru kuna Kata ya Ngabobo, hakuna mawasiliano ya simu, lakini sekta hii mdhibiti, ndio kazi yake kubwa kuhakikisha kwamba, sehemu mbalimbali zinapata mawasiliano, hususan sehemu za vijijini. Kampuni hizi za simu zinakatwa tozo ya asilimia tatu katika mapato yake inaenda kwenye mfuko unaitwa USCAF (Universal Fund) na lengo kubwa la Mfuko huu ni kuendeleza mawasiliano sehemu za vijijini na mijini. Sasa napenda kujua kwamba, Mfuko huu unafanya kazi gani hasa kama kuna sehemu nyingi tu za nchi hii ambazo hazina mawasiliano ya kutosha? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)