Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa siku hii ya leo kuchangia Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano na Mwaka Mmoja. Kwanza napenda kutumia fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kuniwezesha kurudi tena kwa awamu ya pili, lakini nawashukuru wapiga kura wangu ambao hawakufanya ajizi, wameona yale niliyoyafanya wakaamua kunichagua tena. Pia nitakuwa ni mchoyo wa fadhila bila kukishukuru Chama Cha Mapinduzi. Nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii kuwawakilisha wananchi wa Jimbo la Tunduru Kusini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mpango nitachangia mambo mawili, jambo la kwanza ni suala la elimu. Kwanza niipongeze Serikali ya Chama Cha Mapinduzi ikiongozwa na Rais wetu, jemedari, Mheshimiwa Dkt. Pombe Joseph Magufuli, kwa kazi kubwa aliyoifanya kwenye Sekta ya Elimu. Naamini wengi tumeona mafanikio yaliyotokana na Sekta ya Elimu, tumetoka kwenye kuongeza shule za sekondari, kuongeza wanafunzi katika shule za msingi, vyuo pamoja na majengo na ukarabati wa miundombinu katika shule za sekondari na vyuo vikuu vilivyopo hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala hili la elimu bure napenda tuone namna mpango unavyoweza kusaidia shule za kata. Naamini wengi tuliotoka kwenye majimbo ya vijijini wanafunzi wengi wanasoma kwenye shule za kata. Ongezeko la wanafunzi kwenye shule za msingi limesababisha shule za kata ziwe na watoto wengi. Sasa miundombinu iliyopo kwenye shule hizi si rafiki sana ukilinganisha na shule zile ambazo zinahudumiwa na Wizara ya Elimu kama shule zile 89 ambazo zinafanyiwa ukarabati. Ndiyo maana hata ufaulu wake umekuwa wa kiasi kidogo sana ingawa zinajitahidi na watoto walio wengi kutoka vijijini wanasoma kwenye shule hizi. Naomba mpango ungeweka badala ya sasa kuendelea kukarabati naamini shule katika miaka mitano zimekarabatiwa zile kongwe, basi Serikali iangalie shule hizi za kata kuweza kuziongezea miundombinu ili zilingane na shule nyingine ambazo ziko katika mazingira mazuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia shule hizi nyingi wanasoma watoto wa maskini ambao wamejitahidi kujenga mabweni lakini watoto wanakwenda na vyakula shuleni. Naomba Serikali kupitia Mpango wa Miaka Mitano ijayo ijitahidi kuongeza ruzuku kwenye shule za kata ili watoto wanaosoma kwenye maeneo yale ambao wanatoka katika mazingira magumu kwenye kata zetu waweze angalau na wao kupata chakula kwenye shule hizi za kata ili kuwafanya watoto hawa waweze kufaulu vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini watoto hawa kwa mazingira tunayoyaona wanafaulu katika mazingira magumu sana na ndiyo maana utakuta private school wanafaulu vizuri zaidi kwa sababu wako kwenye mazingira mazuri, wanalala mahali pazuri, Walimu wengi wa sayansi, Walimu wa masomo mengine wako wengi na maabara za kutosha. Naomba mpango uangalie namna ya kuimarisha shule zetu za sekondari za kata ili miundombinu ya maabara, madarasa, mabweni, hata chakula Serikali iweze kutoa ruzuku kwenye shule hizi za kata waweze watoto wetu kusoma katika mazingira mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, napenda nichangie sana suala la barabara. Ukizungumzia barabara ukweli tunaishukuru Serikali, Mtwara Corridor, barabara kutoka Mtwara sasa imefika mpaka Nyasa. Tunaishukuru sana Serikali kwa kitendo hiki cha kutujali watu wa kusini kuhakikisha barabara hizi zimekamilika na sasa unapiga lami kutoka Mtwara mpaka unafika Ziwa Nyasa na baadaye unapanda meli kwenda Malawi unakwenda Mbeya, unakwenda wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shukrani hizi, tunaomba tukumbukwe Mtwara Corridor kwa maana ya Reli ya Kusini. Reli ya Kusini ndiyo solution itakayosaidia kuleta maendeleo Mtwara, Lindi na Mkoa wa Ruvuma. Leo Ruvuma kunapatikana makaa ya mawe Ngaka, yote yanasafirishwa kwa njia ya barabara. Utengenezaji au ukarabati wa Bandari ya Mtwara utakuwa na maana kama Reli ya Kusini itajengwa mpaka kufika Mbambabay ambako makaa ya mawe kutoka Ngaka yatatembea kwa njia ya treni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango kazi ambao unajengwa pale Mchuchuma na Liganga hauna maana kama hatutaweza kujenga Reli ya Kusini ili kusaidia uchukuaji wa mawe pamoja na chuma kutoka kwenye machimbo kwenda Bandarini Mtwara ambako bandari yake sasa inakuzwa kwa kiasi kikubwa ili kuhakikisha kwamba inahudumia huku mikoa ya kusini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na barabara hii ya kutoka Mtwara mpaka Nyasa, kwa kweli kwa upande wa Kusini kupitia Mkoa wa Ruvuma hakuna barabara ya lami kwenda Msumbiji. Tunaomba barabara ya Songea kwenda Ngaka iwe ya lami na barabara hii ya Songea – Mokuru – Mkenda ijengwe kwa lami kwa sababu ndiyo njia pekee itakayosaidia kukuza biashara kutoka Msumbiji kuja Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara moja ya kutoka Mtwara Pachani – Nalasi mpaka Tunduru Mjini, tumeona iko kwenye ilani, tunaomba Serikali ndani ya miaka mitano hii iweze kujengwa kwa kiwango cha lami kwa sababu ndiyo njia pekee ya kuokoa mikoa hii ya kusini, hasa Wilaya ya Namtumbo pamoja na Wilaya ya Tunduru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo kuna barabara moja ambayo ninadhani nayo iingizwe kwenye ilani na iingizwe kwenye mpango ili isaidie watu wa Msumbiji kwa sababu watu wa Tunduru mambo yao mengi yanakwenda na watu wa Msumbiji kwa sababu tunafahamiana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya kutoka Tunduru Azimio mpaka Lukumbule mpaka Makande ambayo inamilikiwa na TANROADS nayo ingeweza kuingizwa kwenye mpango kuhakikisha kwamba barabara ile inajengwa kwa kiwango cha lami ili kuwahudumia wananchi wa Tarafa ya Lukumbule na wa Jimbo la Tunduru Kusini kwa ujumla kwa ajili ya kwenda Msumbiji kupeleka mali na kuchukua mali kutoka Msumbiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuchangia ili niweze kutoa mawazo yangu. (Makofi)