Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye Mpango wa Tatu wa Taifa.

Niseme tu kwenye maelekezo yako umeni-preempt, nilitaka niongelee eneo la elimu. Wadau wengi wamezungumzia suala la mitaala yetu ya elimu kwamba tuna sababu ya kuangalia kama kweli elimu ambayo tunaenda nayo inaendana na mazingira yetu halisia. Tumesema sana lakini ukiangalia kwenye vyuo vyetu tafiti nyingi zinafanyika lakini haziendi kutatua changamoto za wananchi. Maana yake wakati mwingine juhudi kubwa zinafanyika kwenye taasisi zetu za elimu lakini yale yanayopikwa kule hayajafiki kwa walaji ambao ni wananchi katika kutatua changamoto zao kwenye upande wa kilimo, mifugo na masuala mengine ya kijamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe ufike sasa wakati elimu ile tunayoifundisha isiwe inaowatoa wanafunzi au watu wetu kwenye maisha yao yale ya kawaida, bali iende kuimarisha maisha ya watu yale ya kawaida. Twende tukawasaidie wafugaji wafuge kisasa, hatimaye wapate tija. Siyo kama mtoto akienda shule…

MWENYEKITI: Upande huu kuna kelele sana, naomba tumsikilize Mheshimiwa.

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Sio tukipeleka watoto wetu shule, tunawatenganisha na zile shughuli za asili ambazo tumekuwa tukizifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka wakati nasoma shule ya msingi tulikuwa na Afisa wa Kilimo, alikuwa anafundisha kwa vitendo kwa wanafunzi na kwa wanakijiji, naye alikuwa anashika jembe la mkono, alikuwa anashika plau la kuvuta na ng’ombe na katika mazingira yaleyale ambayo watu wapo tuangalie elimu yetu kama inatuelekeza upande huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia hata kwenye Vyuo vyetu vya VETA mambo tunayofundisha ni yaleyale ya kila siku; je, tunaangalia mabadiliko ya maisha ya sasa? Je, tuna-address yale mambo ya msingi ambayo yatatuletea tija? Ukiangalia nchi yetu ina mifugo wengi, tunalima sana, lakini hapo tija inakosekana kwa sababu hatupeleki sayansi kwenye maeneo husika ili tuzalishe kwa tija ili hatimaye tunavyoongea Tanzania ya viwanda tubadilike kutoka kwenye kilimo, tuzalishe tupate mazao ya viwandani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo kinatumia ardhi, ardhi haiongezeki, Watanzania tunaongezeka. Baada ya muda kama elimu haiwezi kutusaidia waangalie ni namna gani baada ya muda kwa sababu ardhi tuliyonayo haiongezeki lakini sisi tunaongezeka. Kama haiwezi kututoa kwenye eneo hilo kuhakikisha kwamba elimu yetu inatatua changamoto za msingi na mabadiliko ya kila wakati jinsi tunavyoongezeka na ardhi haiongezeki tukatatua hiyo changamoto ya msingi kwamba baadaye tutakuwa hatuna ardhi ya kutosha, hatuna maeneo ya kufuga mifugo, hatuna maeneo ya kulima. Je, elimu yetu itatutoaje kwenye changamoto hiyo? Lazima tujielekeze huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niongelee suala la ufugaji, hasa eneo la usindikaji wa bidhaa zinazotokana na mifugo. Tuna mifugo mingi sana lakini ukiangalia malori barabarani ukiona yamebeba mifugo, mingi tunasafirisha nchi za jirani. Tunasafirisha nyama, ngozi na mazao mengine. Hatuwezi kupata tija bila kuliangalia hilo eneo kwa makini. Ni lazima tujiwekeze kwenye kuboresha mifugo yetu. Tujiwekeze kwenye kuhakikisha kwamba tunakuwa na machinjio kwenye maeneo yale ambayo kuna mifugo wengi. Hatimaye tu- process vizuri tukatafute masoko nje badala ya kusafirisha mifugo ambayo iko hai. Hiyo inatupotezea na tunapoteza fedha nyingi kwenye eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kidogo suala la miundombinu; hii imeongelewa sana. Hakuna namna tunaweza kupata maendeleo bila kuboresha eneo la miundombinu. Kazi kubwa imefanyika lakini bado tunayo kazi kubwa ya kuifanya. Lazima tutoke hapa tukiwa na jawabu. Kwa sababu ukiwa umelima, una mifugo, bila kuwa na uhakika wa kusafirisha na huduma nyingine za kijamii zinakuwa ni changamoto kubwa. Maeneo mengi barabara kwa sasa hazipitiki kwa sababu ya mvua. Lile suala la TARURA kutokuwa na bajeti ya kutosha, hilo eneo bila kuli-address hatuwezi kutoka, lazima tuje na jawabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yametolewa mapendekezo mengi. Tuache kwenda kama kawaida, lazima tuje na ubunifu kuhakikisha kwamba kwenye eneo hili tunapata fedha za kutosha na siyo kuchukua kwenye upande wa TANROADS. Nao wana majukumu makubwa ambayo ni ya msingi, hivyo, tuje na njia mbadala ya kupata fedha ilituboreshe TARURA ipate fedha za kutosha ili hatimaye watu wapate huduma za usafiri ulio…

MWENYEKITI: Sasa hapa tulipo Mheshimiwa Engineer ni mahali ambapo utuambie sasa tuzipataje hizo fedha? Yaani utoe mapendekezo.

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachosema, lazima tuwekeze kwenye maeneo yetu mkakati. Yameongelewa, eneo la upimaji wa ardhi ambalo nalo nataka niongelee ardhi peke yake, ni sleeping giant ambaye hatujavuna chochote kutoka huko. Ukiangalia kwenye eneo hilo hilo la upande wa ardhi, biashara za upangishaji wa nyumba hazijasimamiwa vizuri. Maeneo hayo kuna mapato ambayo yangeweza kupatikana kuhakikisha kwamba tunapata fedha za kutosha. Tuangalie namna ya kuhakikisha kila tulichonacho tunaweza kukitumia vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukipima ardhi yote kila mtu akalipa kodi tukahakikisha kwamba biashara zote zinazofanyika za ardhi; za kuuza ardhi, za kupangisha nyumba na nyumba zote zikalipa kodi ile stahiki, tukisimamia maeneo hayo tunapata mapato ya kutosha.

Tuangalie namna ya kuhakikisha kwamba tunapata fedha ili tuwekeze kwenye miundombinu ili hatimaye tuweze kufanya shughuli za uzalishaji kwa urahisi. Miundombinu inayopitika kwa urahisi ndiyo itakayotutoa kwenye mkwamo tulionao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa hivi maeneo mengi wananchi wanakwama kwenda hospitali, wananchi wanakwama kufanya shughuli za kimaendeleo kwa sababu barabara zimekatika na hii kila wakati inakula uchumi wa nchi, lazima tuje na jawabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niongelee kidogo eneo la umeme; kazi kubwa imefanyika, vimebaki vijiji vichache. Hata hivyo, ukiangalia kuna baadhi ya maeneo umeme umepita juu, kiasi kwamba wananchi wale wakishushiwa gharama sidhani kama ni kubwa sana, itatusaidia katika kuchochea uchumi kwa kujenga viwanda vidogo na vya kati ili wananchi waweze kufanya shughuli za maendeleo kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)