Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Kassim Majaliwa Majaliwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu Mwingi wa Rehema kwa kutujaalia afya njema tunapoelekea kuhitimisha hoja ya kujadili Hotuba ya Mheshimiwa, Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoitoa wakati wa ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, tarehe 13 Novemba, 2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, natumia fursa hii pia kukushukuru na kukupongeza wewe binafsi pamoja na Mheshimiwa Spika kwa namna ambavyo mmesimamia vyema mjadala huu uliotuchukua siku 4. Hali kadhalika napenda kuungana na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kumshukuru Mheshimiwa, Dkt. John Pombe Magufuli Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutoa hotuba yake nzuri aliyoitoa wakati wa kuzindua Bunge la Kumi na Mbili la Jamhuri ya Muungnao wa Tanzania siku hiyo ya tarehe 13 Novemba, 2020. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jumla ya Waheshimiwa Wabunge 169 wamechangia mjadala huu. Hivyo natumia nafasi hii kuwashukuru na kuwapongeza sana Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia mjadala huu na kuunga mkono maeneo mbalimbali yaliyobainishwa katika hotuba ile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia michango ya Waheshimiwa Wabunge, kwanza nakiri kupokea salamu za pongezi, salamu za shukrani kwa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. Nami nawahakikishia kwamba nitazifikisha baada ya kufunga hotuba hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, michango ya Waheshimiwa Wabunge itasaidia sana Serikali kutekeleza kwa ufanisi maelekezo ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020 - 2025 sambamba na Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Miaka Mitano kutoka mwaka 2021/2022 - 2025/2026 ambao utawasilishwa kwenye mkutano huu na Waziri wa Fedha na Mipango kuanzia wiki ijayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa upande wake itaendelea kushirikiana na Waheshimiwa Wabunge sambamba na kutekeleza ushauri na michango mizuri waliyoitoa wakati wa kuchangia hoja hii. Nitumie fursa hii pia kuwashukuru sana Waheshimiwa Mawaziri kwa kutoa maelezo ya ziada na ufafanuzi mzuri kwenye sekta zote zilizochangiwa na kushauriwa kuelekea kwenye utekelezaji mzuri. Maeneo yote yaliyoshauriwa ni muhimu ambapo Serikali haina budi kuyazingatia katika utekelezaji wa mipango na vipaumbele vyake kwa kipindi kijacho.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tulivyoona wakati wa mjadala huu, masuala na hoja nyingi zimetolewa maelezo na ufafanuzi wa kina kutoka kwa Waheshimiwa Mawaziri ambao wamemaliza muda mfupi uliopita. Niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kuwa Serikali itazingatia maelekezo na ahadi za Mheshimiwa Rais katika kupanga vipaumbele vyake vya mpango wa bajeti katika kipindi chote hiki cha miaka mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuibuliwa kwa hoja nyingi kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge wakati wa mjadala wa Hotuba ya Mheshimiwa Rais ni kielelezo tosha kwamba hotuba hiyo imegusa maeneo muhimu na yenye maslahi ya moja kwa moja kwa wananchi wetu. Miongoni mwa maeneo yaliyosisitizwa na Waheshimiwa Wabunge ni kuimarishwa kwa sekta za miundombinu na usafiri na usafirishaji ambapo taasisi zetu za TARURA na TANROADS nazo pia imeshauriwa namna ya kuziboresha. Sekta ya maji imeguswa, elimu na ujuzi nayo imesisitizwa, uongezaji thamani kwenye bidhaa zetu hususan za kilimo nayo pia imeguswa, uzalishaji mali, masoko, nishati, afya na huduma za kifedha na shughuli za kiuchumi uwekezaji ukiwemo na ujenzi wa viwanda nazo zimeguswa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo yote hayo yamefafanuliwa kinagaubaga kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais ambayo hoja yake tunaihitimisha leo. Kadhalika wakati nawasilisha hoja hii, nililiarifu Bunge lako Tukufu kuwa tayari utekelezaji wa maelekezo na ahadi za Mheshimiwa Rais ulishaanza mara tu alipowasilisha hotuba yake siku ya tarehe 13 Novemba, 2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwenye wiki ijayo tutapata nafasi ya kuchangia hoja ya Waziri wa Fedha na Mipango ambayo nitasheheneza mjadala ninaohitimisha leo. Kama ambavyo unafahamu maandalizi ya bajeti kwa mwaka wa fedha 2021/2022 yanaendelea. Hivyo basi, kutokana na ukweli kuwa maeneo hayo ya vipaumbele yanahitaji kupangiwa fedha za bajeti kwa ajili ya utekelezaji wake, kupitia mijadala na hoja zote mbili, hotuba yangu ya kuhitimisha Mkutano huu wa Bunge nitatoa mwelekeo wa namna ambavyo tutakwenda kutekeleza yale yote ambayo yameshauriwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa maelekezo kwa Wizara na taasisi nyingine za Serikali kuhakikisha kwamba vipaumbele hivyo vinapangiwa fedha kwenye bajeti ya mwaka 2021/2022. Kwa msingi huo, nitumie fursa hii kurudia tena kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwamba maoni na hoja zenu zitazingatiwa wakati wote kwa utekelezaji wa vipaumbele vya Serikali. Vilevile kwa ile miradi inayoendelea kutekelezwa nchini katika sekta za uzalishaji mali ikiwemo kilimo mifugo, maliasili, madini na sekta za huduma ya jamii kama vile elimu na afya zitakamilishwa kama ilivyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu imekuwa ikifanya juhudi kubwa katika kuandaa mpango pamoja na mipango ya bajeti na kwa ajili ya utekelezaji wa vipaumbele mbalimbali vya Serikali vyenye lengo la kuwaletea maendeleo wananchi. Hata hivyo, awali tulikuwa na changamoto ya baadhi ya viongozi na watendaji kutowajibika na kusababisha kudorora katika kuwahudumia wananchi ipasavyo. Katika kukabiliana na changamoto hiyo, Serikali ya Awamu ya Tano ilijikita katika kuhakikisha inarejesha nidhamu katika utumishi wa umma kwa kuweka mkazo katika misingi ya uadilifu, uwajibikaji, kutoa huduma kwa wakati na kuchukua hatua za haraka dhidi ya watumishi wote wanaokwenda kinyume na misingi ya utendaji wa kazi ndani ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nyote mtakubaliana nami kwamba kuimarishwa kwa nidhamu ya viongozi na watendaji Serikalini imekuwa chachu ya kufikiwa kwa malengo mengi tuliyojiwekea. Aidha, baada ya kufuatilia kwa karibu michango ya Waheshimiwa Wabunge, nami napenda kusisitiza masuala machache kwa viongozi na watendaji wa Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja, ni suala la utoaji wa taarifa kwa umma kwa wakati kuhusu miradi na shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na Serikali. Katika hili, nirejee kauli ya Mheshimiwa Rais mpendwa aliyoitoa tarehe 4 Juni, 2018 wakati akizindua Awamu ya Pili ya Programu ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo Nchini (ASDP II) kwamba viongozi na watendaji wa Serikali wanao wajibu wa kueleza kwa kina mambo yanayotekelezwa na Serikali kila wanapopata nafasi ya kufanya hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sote ni mashuhuda kwamba yako mambo mengi ya kujivunia yametekelezwa na yanaendelea kutekelezwa na Serikali yetu. Kwa msingi huo, Watanzania wanayo haki ya kuhabarishwa na kufahamu mipango na mikakati mbalimbali ya Serikali katika kuwaletea maendeleo wananchi wetu. Nitoe wito kwa viongozi na watendaji kwenye ngazi mbalimbali kuzingatia eneo hilo la mawasiliano kwa umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo napenda kulisisitiza ni viongozi na watendaji kuwafikia wananchi kwenye maeneo yao kusikiliza kero zao na kuzitafutia ufumbuzi. Katika ziara zangu zote nimekuwa nikisisitiza kuwa viongozi na watendaji wawafuate wananchi kwenye maeneo yao, wawasikilize na kuwahudumia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwakumbushe tu viongozi na watendaji wote kwamba tunao wajibu mkubwa kwa wananchi kutokana na dhamana waliotupatia, hivyo, tunapaswa kuwajibika kwao badala ya kusubiri ziara za viongozi wakuu wa kitaifa. Natumia fursa hii kuwaambia viongozi na watendaji wote wa Serikali kuwa tutapima utendaji wenu kwa namna mnavyotatua kero za wananchi kwenye maeneo yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa upande wetu itahakikisha inachukua hatua dhidi ya wote watakaokiuka sheria, kanuni na taratibu za kazi na kwamwe hatutamvumilia mtumishi mzembe na mwenye kufanya kazi kwa mazoea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyoeleza awali, hotuba yangu ya kuhitimisha mkutano huu itajumuisha mijadala yote miwili; huu ambao tunahitimisha leo na ule wa Mpango wa Wizara ya Fedha ambao utaanza kujadiliwa kuanzia Jumatatu. Nimalizie maelezo yangu kwa kuwasihi Waheshimiwa Wabunge kwamba tunao wajibu wa kuishauri Serikali sambamba na kuwaongoza wananchi katika kusimamia utekelezaji wa ahadi na maelekezo ya Mheshimiwa Rais yaliyomo katika hotuba yake ya kuzindua Bunge la Kumi na Mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande mwingine, niwaombe Waheshimiwa Wabunge wenzangu kuimarisha ushirikiano wa wananchi na mamlaka mbalimbali za Serikali hususan Serikali za Mitaa kwa lengo la kuhakikisha kwamba wanaunga mkono Serikali na hivyo kufanikisha utekelezaji wa vipaumbele mbalimbali kwenye bajeti ya mwaka 2021/2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, niseme ni kwamba nimevutiwa sana na michango ya Waheshimiwa Wabunge wakati wote wa kuchangia hoja hii. Nimepokea ushauri wenu kama ambavyo nilieleza wakati tunawasilisha hoja hii na sasa narudia kwamba tutaendelea kushirikiana katika kuboresha yale yote ambayo mmechangia kwenye hoja hii ya kujadili hotuba ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo aliitoa tarehe 13 Novemba, 2020 wakati akifungua Bunge la Kumi na Mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa kutoa hoja. (Makofi)