Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Prof. Kitila Alexander Mkumbo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ubungo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (UWEKEZAJI): Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa nafasi hii na nawashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa maoni yao mazuri sana kuhusu Sekta ya Uwekezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijajibu baadhi ya hoja, naomba niseme mambo mawili ya kihistoria. Moja, naomba nichukue nafasi hii kukipongeza sana Chama cha Mapinduzi kwa kuadhimisha miaka 44 tangu kilipozaliwa na ukijumlisha na wazazi wake, miaka 60 leo mambo ambayo yanakifanya kuwa chama kikongwe kabisa Barani Afrika. Historia ya leo inakiweka Chama cha Mapinduzi kuwa chama ambacho kimekaa madarakani kwa muda mrefu kuliko vyama vyote Afrika. Mwaka juzi kulikuwa na chama ambacho kilikuwa kimekizidi sitaki kusema nchi gani lakini kimeondolewa madarakani kwa hiyo kimebaki Chama cha Mapinduzi na nakipongeza sana kwa historia hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, Bunge hili zimeshatolewa hotuba hapa za kufungua Bunge na hotuba za wakuu wa nchi zaidi ya 20 lakini zipo hotuba tano ambazo ni za kihistoria ikiwemo hizi hotuba mbili ambazo tunazijadili leo. Kwa ruhusa yako kwa haraka sana, hotuba ya kwanza ya kihistoria ambayo inajulikana katika nchi hii ndani ya Bunge hili ni hotuba ya Desemba, 1962 iliyotolewa na Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere. Hotuba hiyo ndiyo iliyozaa Jamhuri ya Tanganyika. Lengo lake kubwa ilikuwa ni kujenga Umoja wa Kitaifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya pili ni ya tarehe 25 Aprili, 1964 iliyotolewa katika Bunge hili. Lengo la hotuba hiyo Mwalimu alitumia kuomba ridhaa ya Bunge kuridhia Mkataba wa Muungano kati ya Tanganyika na Zanzibar. Hotuba hiyo ndiyo iliyozaa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya tatu muhimu ya kihistoria katika nchi hii ya tarehe 29 Julai 1985. Hotuba hii aliitumia Mwalimu Nyerere kuaga…

WABUNGE FULANI: Uwekezaji.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (UWEKEZAJI): Tulia wawekezaji unakuja. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya nne ni ya tarehe 20 Novemba, 2015 iliyotolewa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. Hotuba hii lengo lake kubwa ilikuwa ni kujenga msingi wa kupambana na ufisadi na kuimarisha maadili ya utumishi wa umma na matokeo yake wote tumeyaona. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya tano ya kihistoria ni iliyotolewa tarehe 13 Novemba, 2020. Lengo lake kubwa ni kulinda na kuendeleza status ya nchi ya uchumi wa kati. Hotuba hii imetoa mwelekeo wa kiuchumi wa nchi na imejengwa katika uwekezaji kama njia ya kukuza uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nichukue hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kunipa nafasi kuwa sehemu ya Serikali yake ili kutekeleza maono makubwa ambayo yapo ndani ya hotuba hii ya tarehe 13 Novemba, 2020. Lengo kubwa ambalo Mheshimiwa Rais ametuelekeza na ambalo tunalisimamia kwa bidii na kwa maoni ambayo Waheshimiwa Wabunge wameyatoa ni mambo matatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza tuhamasishe uwekezaji wa ndani nan je ya nchi. Katika kuhamasisha uwekezaji Waheshimiwa Wabunge wanairudia ile kauli ya Mheshimiwa Rais, tunapozungumzia uwekezaji sio lazima moja, iwe kutka nje, lakini sio lazima uwe bilionea. Unatumia nafasi yako ndogo uliyonayo unaweka akiba, unapata mtaji, unawekeza unajenga uchumi, unaanza kujitengenezea mazingira kutoka kuwa elfunea kwenda milionea na hatimaye kuwa bilionea. Kwa hiyo niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge ambao ni Wajumbe wa Mabaraza ya Madiwani waende kuhamasisha katika halmashauri zao ili halmashauri zetu zitengeneze mazingira ya uwekezaji, ikiwemo kutenga maeneo ya uwekezajikwa wawekezaji wetu wa ndani, lakini pia wa nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, tumepewa kazi ya kuwezesha wawekezaji ndani ya nchi waliokwisha kuwekesha hapa kwa sababu, balozi mkubwa sana uwekezaji ni yule muwekezaji ambaye tayari yupo ndani ya nchi. Kwa hiyo, naomba sana Waheshimiwa Wabunge tuendelee kuhamasisha halmashauri zetu ili ziweke mazingira mazuri ya kuhudumia wawekezaji ambao wapo. Pale ambapo kuna changamoto za wawekezaji tuzishughulikie kisheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho katika uwekezaji, ni muhimu sana kuwahudumia. Kwamba, pale ambapo mwekezaji ameshaweka, amewezeshwa, kiwanda kipo pale, ni muhimu sana mamlaka zilizopo kuanzia ngazi ya halmashauri wawekezaji hawa wahudumiwe kwa kupatiwa mahitaji muhimu. Tunafanya mawasiliano ya karibu na wenzetu katika Wizara mbalimbali ili kuhakikisha kwamba, huduma muhimu zikiwemo umeme, maji na barabara zinapatikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli, kwa sasa katika nchi yetu huduma za msingi za kufanya uwekezaji mkubwa zipo vizuri ikiwemo katika eneo la miundombinu. Kama ni barabara maeneo yote makubwa yameshaunganishwa kwa mtandao wa barabara za lami. Kama ni usafiri wa majini karibu maziwa yetu yote makubwa ikiwemo na bahari tayari kuna vyombo vya usafiri vya kutosha, lakini pia usafiri wa anga umeimarika sana. Kama ni hali ya kisiasa ambayo ni ya msingi sana katika uwekezaji Tanzania ndio inaongoza kwa utulivu wa kisiasa Afrika. Kwa hiyo kwa kweli Waheshimiwa Wabunge tuendelee kuhamasisha wawekezaji waje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, tupo katika mchakato wa kuifanyia mabadiliko Sheria ya Uwekezaji ili kuiboresha zaidi ikiwemo kuimarisha taasisi yetu ya TIC ambayo Waheshimiwa Wabunge wengi wametoa maoni mazuri namna ya kuiboresha. Pia tunatengeneza mkakati wa kuhamasisha uwekezaji katika ngazi ya kitaifa, lakini pia katika ngazi ya mkoa hadi katika ngazi ya halmashauri na ndio maana tumekuwa tukipita Mheshimiwa Waziri Mkuu akituongoza kwenda kuzindua Miongozo ya Uwekezaji katika ngazi ya mikoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kuwaalika sana Waheshimiwa Wabunge katika mikoa yenu. Pale ambapo tumekuja kuhamasisha na kuzindua miongozo hii naombeni sana mshiriki. Niwapongeze sana Mkoa wa Iringa, tulikuwa huko juzi, imefanyika kazi kubwa na nadhani mikoa mingi inaendelea kuzindua na hivi karibuni tutakwenda kuzindua katika mikoa mingine chini ya uongozi wa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, tumeaswa kila unapopata nafasi ushukuru watu ambao wamefanya tofauti katika maisha yako. Sasa nataka nichukue nafasi hii kwanza kukishukuru sana Chama Cha Mapinduzi kwa fursa kilichonipa ya kugombea nafasi ya ubunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwashukuru sana wananchi wenzangu wa Jimbo la Ubungo kwa kunipa nafasi ya kuwa Mbunge wao, hatimaye tukakomboa Jimbo la Ubungo lililokaa Misri kwa miaka 10 sasa lipo Kaanan, tumetoka Misri sasa tupo Kaanan. Niwapongeze sana, tutashirikiana sana kuhakikisha kwamba, mambo ambayo tumeyaahidi tunayafanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi hii. (Makofi)