Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu hotuba ya Mheshimiwa Rais akifungua rasmi Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dodoma, tarehe 13 Novemba, 2020 naomba kutoa mchango wangu wa maandishi baada ya kubaini kwamba wachangiaji wamekuwa wengi na naomba niseme kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesoma hotuba zote mbili ya mwaka 2015 na ya 2020; kama Mheshimiwa Rais alivyotuasa Wabunge kwamba lengo la kufanya hivyo ni ili tuweze kupima utekelezaji wa vipaumbele alivyokuwa navyo Mheshimiwa Rais katika kipindi cha miaka mitano ya kwanza ya Serikali ya Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka mitano ya kwanza ya Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, ni dhahili kwamba Mheshimiwa Rais amewafanyia Watanzania kazi nzuri mno na ni utendaji uliotukuka ambao umekiinua chama chetu (CCM) na hata kutubeba Wabunge tulioshinda katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 28, 2020 na kuwepo Bungeni leo hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa Ilani ulikuwa wa ufanisi mkubwa kila sekta; kwanza, utawala bora. Tumeweza kuwa nchi ya kwanza Afrika katika kupiga vita rushwa. Pia tumekuwa nchi ya 28 kati ya 136 duniani katika matumizi mazuri ya fedha za umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, uchumi umekuwa kwa 7% na kufanya pato ghafi kupanda toka shilingi trilioni 94.349 2015 hadi kufikia shilingi trilioni 139.9 mwaka 2019 na Taifa kupanda chati kiuchumi na kuwa Taifa la uchumi wa kati 2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, umeme wa REA toka vijiji takribani 2000 mwaka 2015 na kufikia vijiji 9000 mwaka 2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, nne, upatikanaji wa maji safi na salama kuongezeka kutoka 47% mwaka 2015 hadi 70.1% mwaka 2020 kwa vijijini na kwa mjini toka 74% hadi 84%.

Mheshimiwa Naibu Spika, tano, barabara za lami zimejengwa, madaraja yamejengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sita, watoto wetu wameendelea kupatiwa elimu bila malipo darasa la kwanza hadi kidato cha nne. Kila sekta Serikali imefanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, saba, miradi mkakati imeendelea kutekelezwa, mfano Bwawa la Mwalimu Nyerere lenye uwezo wa kuzalisha umeme megawati 2115 linaendelea kujengwa na mradi unaendelea vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa reli ya kisasa ya SGR unaendelea vizuri na section ya Dar es Salaam/Morogoro itamalizika mwaka huu wa 2021.

Mheshimiwa Naibu Spika, ATCL; ndege zimenunuliwa nane na zinaruka; tatu ziko njiani; kwa kifupi mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Tano kipindi cha kwanza cha miaka mitano (2015 – 2020) ni makubwa sana na pongezi na shukrani nyingi zimuendee Mheshimiwa Rais John Pombe Joseph Magufuli kwa uongozi uliotukuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya Mheshimiwa Rais ya Novemba 13, 2020, kimsingi kwenye hotuba hii ameweka dira kwa Taifa kwamba ni mambo gani amepanga kutekeleza na ameweka wazi kwamba itakuwa ni utekelezaji Ilani ya Uchaguzi yenye kurasa 303 na ahadi alizotoa majukwaani wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, yako mengi ya kuboresha maisha ya Watanzania lakini naomba kuchangia kwenye mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara; zitajengwa barabara za lami zenye urefu wa kilometa 2500 na lengo ni kufikia kilometa 6006 kuunganisha Wilaya na Mikoa yote nchini. Nashauri utekelezaji uanze na ahadi za Mheshimiwa Rais alizozitoa hadharani kwa mdomo wake na mbele ya wapiga kura wengi ukizingatia kwamba pia mikutano yake ilikuwa na watu wengi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule Meru aliahidi kujenga kwa kiwango cha lami barabara ya Malula Kibaoni kwenda King’ori; Maruvango, Leguriki hadi Ngarenanyuki na mpaka Oldonyosambu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kilimo; kwenye hotuba ya Rais kilimo kitaboreshwa na kubadilishwa sura kiwe kilimo cha biashara ili kuongeza uzalishaji. Nashauri Wizara ya Kilimo iongeze nguvu kwenye miundombinu ya umwagiliaji ili tuondokane na kilimo cha kutegemea hali ya hewa ambapo mvua zikikosekana basi wakulima wanapata hasara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu eleimu; elimu itaendelea kuboreshwa na mpango ni kujenga shule za sayansi za wasichana moja kila Mkoa. Huu mpango mzuri na kule Meru kuna shule ya wasichana ilibuniwa na aliyekuwa Mbunge wetu kwa tiketi ya CCM Marehemu Jeremiah Solomon Sumari ambaye alitangulia mbele ya haki Januari, 2012 kabla ndoto yake haijatimia.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kwa Serikali ni shule hiyo ijengwe maana ilishaanza tayari na eneo la ujenzi lipo. Nilikwenda kutembelea mradi huo nikaridhika na kuamua kwamba nitaishawishi Serikali iendelee na mradi huo kumuenzi ndugu yetu huyo ambaye mema yake sasa yanaingia kwenye Dira ya Maendeleo ya Taifa 2021 – 2025.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.