Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Regina Ndege Qwaray

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi uliyonipa. Nami niungane na wenzangu kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa nafasi aliyonijalia hadi siku ya leo nimeweza kuwepo hapa Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee pia nikishukuru chama changu kwa kuniteua na kunipendekeza katika ngazi zote na hatimaye leo niko hapa. Pia niwashukuru kwa namna ya pekee sana akina mama wa Mkoa wa Manyara kwa imani kubwa waliyoonesha juu yangu na kuniona natosha kuwa mwakilishi wao katika Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee niishukuru pia familia yangu; mume wangu na watoto wangu ambao wamekuwa bega kwa bega na mimi muda wote wa mchakato na hata sasa wamekuwa wavumilivu kipindi chote ambacho niko katika majukumu yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee, niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi kubwa iliyoifanya kwa miaka mitano ya kuhakikisha Tanzania inasonga mbele kimaendeleo. Pia nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli, kwa hotuba nzuri iliyosheheni matumaini kwa Watanzania ambayo inaonesha dira kwa nchi yetu. Kwa namna ya pekee, tunamwomba Mwenyezi Mungu aendelee kumjalia afya njema, busara na hekima ili yale yote aliyoahidi na aliyoyasema katika hotuba yake yaweze kutekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijikite katika kipengele cha elimu. Kwanza niipongeze sana Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi ambayo imeona ni vyema kuwa na Watanzania wenye elimu na kuhakikisha kila mtoto wa Kitanzania ambaye ana umri wa kwenda shule anaweza kwenda shule na kupata elimu bure kuanzia darasa la awali mpaka kidato cha nne; si kazi rahisi. Ndugu zangu, Tanzania imesonga mbele. Ukiangalia miaka ya nyuma waliokuwa wanapata elimu walikuwa wachache sana lakini leo kila Mtanzania ana uhakika wa kupata elimu na anasoma bure. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na jitihada zote za Serikali bado tuna changamoto ndogo ndogo ambazo Serikali yetu inapaswa ione kwa jicho pevu kwamba bado tuna miundombinu mibovu, madarasa ni machache msongamano ni mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tuna upungufu mkubwa wa madawati na wataalam kwa maana kwamba walimu ni wachache. Kuna shule ambazo wanafunzi ni wengi darasani, unaweza kuwa na wanafunzi 200 lakini walimu ni wachache sana. Kwa hiyo, uwiano kati ya mwalimu na mwanafunzi bado haujazingatiwa. Hii inabidi Serikali iangalie uwiano huo ili utendaji kazi kati ya ufundishaji na ujifunzaji uwe mrahisi na wanafunzi wetu waweze kufanya vizuri huko madarasani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nashauri Wizara hii ya Elimu iangalie upya mtaala wa elimu unaotumika. Elimu yetu inayotolewa kwa sasa haimuandai mwanafunzi kwenda kusimama mwenyewe na kujitegemea. Kwa hiyo, napendekeza Wizara ione namna gani elimu inayotolewa kwa sasa inaweza kumuandaa mwanafunzi ili aweze kujitegemea. Kwa maana ya kuboresha vyuo vya ufundi, wanafunzi wapate ujuzi wa kutosha ili waweze kujianzishia maisha kwa maana ya kuwa na ujuzi wa kwenda kujitegemea na kuanzisha ujasiriamali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo basi nashauri Serikali iboreshe vyuo vya ufundi vilivyopo, lakini ihakikishe inaanzisha vyuo vya ufundi katika kila wilaya vikiwa na taaluma na ujuzi ambapo kila mwanafunzi anaweza kupata ujuzi tofauti tofauti. Kwa hiyo, wanafunzi wetu wanapomaliza kidato cha nne ni vyema akaamua kujichagulia kuingia kidato cha tano na cha sita ama kwenda kwenye vyuo vya ufundi kujipatia ujuzi hatimaye aweze kujitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo Wizara ya Elimu inapaswa sasa kuanzisha au kusimamia kuwepo na kitabu kimoja cha kiada. Kwa maana kwamba tuwe na kitabu kimoja cha kiada kuanzia shule za msingi za Serikali pamoja na shule za msingi za binafsi. Hii itasaidia kuwa na uniformity katika elimu badala ya kuwa na vitabu tofauti vya kiada mwisho wa siku wanafunzi wanafanya mtihani unaofanana lakini wakiwa wanawezeshwa kwa kutumia vitabu tofauti tofauti. Angalizo kwa Serikali pia iangalie vitabu vinavyotumika katika shule za private viwe na ithibati za Kamishna wa Elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)