Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. ANTHONY P. MAVUNDE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi hii. Kwanza kabisa napenda nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema aliyeniwezesha kusimama siku ya leo. La pili, nakishukuru sana Chama changu Cha Mapinduzi, chini ya Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuniteua kupeperusha bendera ya CCM katika Jimbo la Dodoma Mjini na Wanadodoma wakaniamini na kunichagua tena. Jimbo hili watu wanakwenda msimu mmoja mmoja, mimi nimerudia namshukuru sana Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma hotuba ya Rais, Mheshimiwa Magufuli ya mwaka 2015 na mwaka 2020, inakupa dira, inakupa dhamira na upendo mkubwa ambao Rais wetu anao katika kuipeleka Tanzania kwenye maendeleo. Ni dhahiri kabisa kupitia hotuba hizi, mtu yoyote anaweza akaona Tanzania ilipotoka na inapokwenda, tunakwenda pazuri sana, tumuunge mkono Rais wetu mpendwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitazungumza maeneo mawili ya kipaumbele ambayo Mheshimiwa Rais ameyagusia katika hotuba. La kwanza ni la uunganishaji wa Mifuko ya Uwezeshwaji Wananchi Kiuchumi. Hoja hii ni muhimu sana katika kuwasaidia wajasiriamali wa Tanzania kwa sababu Mifuko hii ilikuwa ni mingi, kila mmoja anatowa mikopo na ruzuku kwa wakati wake, lakini kwa kuunganishwa Mifuko hii maana yake ni kwamba itatoa wigo mkubwa zaidi kwa watu wengi kuweza kupata fursa ya mikopo hii. Imani yangu ni kwamba katika zile ajira milioni nane, ni rahisi sana kuzifikia kupitia katika Mifuko hii na naamini kabisa kwamba, Mifuko hii ikiunganishwa itasaidia pia katika mfumo wa ukopeshwaji, badala ya vikundi iende kwa mtu mmoja mmoja ili Watanzania wengi zaidi waweze kupata fursa hii ya mikopo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo nashauri Serikali kwamba Mifuko hii iende sambamba na program za kukuza ujuzi. Ofisi ya Waziri Mkuu wana programu nzuri sana ya kukuza ujuzi kwa vijana ambayo inaitwa RPL. RPL ni Recognition of Prior Learning, ni mfumo wa urasimishaji ujuzi kwa vijana wenye ujuzi ambao hawajapitia mfumo rasmi na mafunzo ya ufundi yaani wako vijana mtaani wanajua kuchonga vitanda, wanajua kuchomelea, hajawahi kusoma VETA, hajawahi kusoma Don Bosco, Serikali inachokifanya inakwenda kuwajengea uwezo na kuwapa uwezo na kuwapa vyeti vya kuwatambua. Programu hii iendelee na naamini itawagusa vijana wengi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nashauri pamoja na kuunganisha hii Mifuko tusimamie pia ile program ya ODOP (One District One Product) itatusaidia sana kwenye kuimarisha na kukuza shughuli za vijana na akinamama na watu wenye ulemavu katika maeneo tofauti tofauti.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili na la mwisho, mimi ni Mbunge wa Dodoma Mjini na sisi tumepata heshima ya Dodoma kuwa Makao Makuu. Mwanzoni wakati wakati inasemwa watu walijua ni maneno ya utani, lakini Rais Magufuli amefanya kwa vitendo. Nachukua fursa hii pia kulishukuru sana Bunge letu kwa kutunga Sheria Maalum ya Dodoma Capital City Declaration Act ya mwaka 2018 ambayo haiwezi kubadilisha maamuzi ya Makao Makuu mpaka pale itakapoletwa tena Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshuhudia maendeleo makubwa ndani ya muda mfupi, Dodoma imechangamka, uchumi umeongezeka, maisha ya watu yamebadilika. Tunategemea mradi mkubwa wa uwanja mkubwa wa ndege wa Msalato, lakini barabara za mzunguko ambao zitaondoa msongamano katika Jiji la Dodoma. Hii ni kazi kubwa ambayo imefanywa na Rais Magufuli katika eneo la Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali, mwaka 1989 ilitungwa sheria ya Dodoma Special Investment Area ambayo ilikuwa inatoa unafuu kwa wawekezaji wanaokuja kuwekeza Dodoma. Naomba sheria hii ipewe extension kwa sababu ime-expire mwaka 2019 ili kila mtu anayekuja kuwekeza Dodoma, apate unafuu na Dodoma iendelee kujengeka. Naamini kupitia sheria hii Dodoma itakua zaidi na zaidi na ile azma ya Mheshimiwa Rais kuwa Dodoma kuwa ni kati ya majiji bora Afrika itatimia kupitia sheria hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema haya, naunga mkono hoja na nashukuru sana kwa nafasi, tuendelee kumsaidia Rais wetu. (Makofi)