Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama walivyo Wabunge wenzangu kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama kwenye Bunge hili, naomba nichukue fursa hii kukishukuru Chama cha Mapinduzi kwa kunipatia nafasi ya kuwa mwakilishi wa Jimbo la Kibaha Vijijini. Kwa namna ya peke kabisa niwashukuru wananchi wa Jimbo la Kibaha Vijijini kumpatia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kura za kutosha, kunipatia mimi Mbunge wa Chama cha Mapinduzi kura za kutosha na kuwapa Waheshimiwa Madiwani wa kata mbalimbali katika jimbo langu kura za kutosha. Nawaahidi kutoa ushirikiano wa kutosha kwao na nitajitahidi kuwatumikia kwa kadri ya uwezo Mwenyezi Mungu atakavyonijalia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na muda kuwa mchache, naomba nijielekeze kwenye hoja chache ambazo nimezisoma katika hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoitoa tarehe 13 Novemba, 2021 wakati anafungua Bunge hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, najielekeza kwenye ukurasa wa 13 wa hotuba hiyo. Katika hotuba hiyo Mheshimiwa Rais alijaribu kuonesha hisia zake na kuonesha ni namna gani na sekta zipi anaamini kwamba zitalifikisha Taifa hili kwenye uchumi mkubwa na kuwaondoa Watanzania kwenye umaskini na kuwafanya wawe wanaishi maisha mazuri na salama kabisa.

Katika maeneo hayo, naomba nichangie kwenye sekta mbili; kilimo na ufugaji. Hawa wakulima ambao tunawazungumza kwenye Bunge hili, ukiangalia kwa haraka haraka katika Wabunge wote tuliopo hapa tunao wakulima wa kawaida kabisa na wafugaji wadogo kabisa ambao wako kwenye mazingira ya vijijini kabisa ambao ndiyo tunatakiwa tuwaelekezee nguvu zetu kuhakikisha kwamba wanafuga na walima katika mazingira yaliyo bora.

Naomba nieleze kwamba katika jimbo langu na nafikiri na kwenye majimbo mengine, makundi haya mawili ni rafiki lakini ndiyo makundi ambayo yanagombana kila siku. Ukikaa unasikia mkulima amevunjika mkono kapigwa bakora na mfugaji, ukikaa mfugaji kaumizwa yaani ni vita siku hadi siku.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina ushauri kidogo katika suala hili, kwa kuwa hawa ni wakulima na wafugaji ambao tunawategemea kwa ajili ya kukuza kilimo na mifugo yao, nafikiri tungetumia maeneo yetu yaliyotunzwa kuwaondoa wafugaji walio katikati ya vijiji ambavyo vinalima kwenda kukaa kwenye maeneo ambayo yanafaa kwa ajili ya shughuli za ufugaji na wakasaidiwa mbinu mbalimbali wakafuga vizuri na hatimaye mifugo hiyo ikawasaidia. Kwa mfano, kule kwetu Kibaha Vijijini, tunayo maeneo ya Kwale yaliyokuwa yanamilikiwa na watu wa kilimo, tunayo maeneo ya NARCO ni msitu mkubwa sana katika Jimbo la Chalinze, ni vizuri wafugaji wa maeneo yale ya karibu wangehamishiwa kwenye maeneo yale wakawekewa miundombinu ili waweze kufuga vizuri na waondoke kukaa katikati ya wakulima waachwe wale wakulima wadogo nao wanaohangaika kulima kilimo kisichokuwa na tija angalau waambulie kupata chakula kidogo ambacho wanakilima kwa kutumia nguvu zao kwa jembe la mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Sika, sambamba na hilo, najielekeza katika ukurasa wa 19 ambapo Mheshimiwa Rais amejaribu pia kuonyesha ili uweze kukuza uchumi wa nchi hii au kuwaendeleza Watanzania hawa ni lazima tuwekeze nguvu kwenye viwanda. Nashukuru sana kwamba Mkoa wa Pwani unatekeleza na unatambuliwa kwamba umefanya kazi kubwa ya kujenga viwanda vingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka Serikali ijaribu kulifikiria jambo moja, wanafahamu matatizo yanayowakuta watumishi kwenye viwanda vile? Wanajua mishahara ya wafanyakazi wanaofanya kazi kwenye viwanda hivi ambavyo wawekezaji wetu wamewekeza?

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali ingewezekana hata kwa kuanzia na Mkoa wa Pwani watengeneze timu maalum wapite kule, waangalie mishahara ya wafanyakazi hawa ambayo wanalipwa kwenye viwanda vile vya uwekezaji. Pia waangalie mazingira wanayoyafanyia kazi, wana mazingira magumu sana kiasi ambacho huwezi kuamini hali ile inaweza ikatokea kwa wafanyakazi wale ambao wako kwenye maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hayo lipo jambo lingine la ujenzi wa miundombinu. Nashukuru kwenye Mkoa wetu wa Pwani, kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi 2025 inatajwa barabara mkakati na nzuri kabisa inayoweza kwenda kutoa huduma nzuri kabisa inayoanzia Bagamoyo pale Makofia, inapita Mlandizi, inakwenda kwa kaka yangu Mheshimiwa Jafo, mpaka inatokea Kimara Misale huko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni vizuri barabara hii ishughulikiwe kwa haraka zaidi. Wananchi wamekaa kwa muda mrefu wakisubiri matengenezo barabara hii, naiomba Serikali ifike kwenye maeneo yale ikiwezekana iwaeleze wale ambao wanaathirika na mradi huu mara utakapokuwa unaanza utekelezaji wake wawape taarifa sahihi, bado wananchi hawaelewi na wanashangaa. Pamoja na kwamba tumeeleza vya kutosha kwenye Ilani lakini bado wanapata shida ya kuamini kwa sababu ni barabara iliyotajwa kwenye Ilani hii na hata ile iliyopita. Niiombe Serikali kipindi ambacho tunajiandaa kwenda kufanya utekelezaji wa barabara hii na nina imani kwamba kwa uwezo wa Serikali iliyopo na kwa jinsi inavyojipanga kutekeleza miradi hii itakwenda kuitekeleza, basi itenge muda sasa iende ikazungumze na wananchi wa maeneo yanayoanzia Bagamoyo na kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, naunga mkono hoja. (Makofi)