Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Esther Edwin Maleko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. ESTHER E. MALEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kuzungumza katika Bunge hili, nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, niwashukuru sana Chama changu Cha Mapinduzi kwa kunipa nafasi kwa kuteuliwa kugombea. Zaidi niwashukuru akinamama wa Kilimanjaro kwa imani kubwa waliyonipa, wakanipa kura za kishindo na mimi nikaweza kuwa Mbunge wao na kuja kuwawakilisha katika Bunge hili Tukufu. Pia nisiwasahau wazazi wangu, mume wangu, watoto wangu, ndugu jamaa na marafiki, kwa namna walivyonisaidia kwa maombi na kwa ushauri mpaka leo niko hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja kuchangia katika hotuba ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa wakati anafunga Bunge la Kumi na Moja, lakini wakati anafungua Bunge la Kumi na Mbili Novemba 13. Katika hotuba yake Mheshimiwa Rais ambayo imetoa dira, mwelekeo na mustakabali wa Taifa, Mheshimiwa Rais alisema katika ukurasa wa 10 kwamba wataongeza jitihada za kuwasaidia wananchi kiuchumi kwa kuwapa mikopo ambayo haina riba au yenye riba kidogo. Naomba basi niende moja kwa moja kuishauri Serikali yangu sikivu, ifanye utaratibu wa namna gani hiyo mikopo ambayo inatolewa na halmashauri 4% kwa wanawake, 4% kwa vijana na 2% kwa wenye walemavu, iangalie basi ni namna gani mikopo hiyo inaweza kuongezwa. Zaidi ya hapo iangaliwe ni namna gani mikopo hiyo haitatolewa kwa masharti ya kupewa kwa vikundi, ikatolewe kwa mtu mmoja mmoja kwa sababu ni wanawake wengi ambao wanahitaji mikopo hiyo lakini wakati mwingine wanakosa kwa sababu ya masharti ambayo yamewekwa kwamba ni lazima mkakope kwa vikundi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu najua Serikali yangu ni sikivu naamini itazingatia suala hilo na kwasababu akinamama wa Kilimanjaro wengi ni wakulima, lakini wengi ni wafanyabiashara wakipatiwa fursa hiyo adhimu wataweza kukwamua familia zao. Kama unavyofahamu mwanamke ndiye anayeinua uchumi wa familia, hivyo mwanamke akiguswa familia itaguswa lakini pia na Taifa litakuwa limeguswa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nisiache kulisema hili pia, kule kwetu Kilimanjaro akinamama wengi wanauza ndizi lakini ndizi haina bei kabisa inapopelekwa sokoni. Mwanamke anapopeleka ndizi sokoni anaenda kuiuza kwa shilingi elfu moja na wakati mwingine wanunuzi wanamkopa, anaweza kukaa na hiyo ndizi ikaiva kwa hiyo hivyo inabidi aitoe kwa wale wanunuzi ambao wao wakienda kuiuza wanaenda kuiuza kwa zaidi ya shilingi elfu ishirini na tano. Basi tuone ni namna gani tunaweza kuwapatia akinamama hawa elimu ya namna gani wanaweza kuchakata ndizi hizo na wakaweza kupata kipato zaidi na siyo kuonewa kwa namna ambavyo wanaonewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hali ya hewa ya Kilimanjaro tunaweza kulima kilimo cha mbogamboga, kilimo cha bustani. Naiomba Serikali yangu Tukufu iweze kuongeza bajeti kwenye Wizara ya Kilimo ili sasa wanawake hawa ambao ni wakulima wapate elimu bora juu ya kilimo hicho wanacholima kwenye matunda, kwenye mbogamboga na tukaende kuongeza pato la Taifa. Kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais amesema leo Tanzania iko nafasi ya 20 kidunia kwa kuzalisha mazao haya, lakini imeingiza zaidi ya dola milioni 412 kwa mwaka 2015; mwaka 2018/2019 imeingiza zaidi ya dola milioni 779. Je, hatuoni…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Muda wako umeisha Mheshimiwa.

MHE. ESTHER E. MALEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)