Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Aleksia Asia Kamguna

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. ALEKSIA A. KAMGUNA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi. Pia namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama hapa leo kwa mara ya kwanza katika Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru pia Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuniteua pamoja na vyombo vyote vya Chama cha Mapinduzi hatimaye nimefika hapa katika hili Bunge. Nasema ahsante. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru pia wapiga kura wangu wanawake wa Mkoa wa Morogoro ambao wameniwezesha kuja hapa leo na kuwa msemaji wao. Mwisho naishukuru familia yangu ambayo ilikuwa bega kwa bega na mimi hatimaye nimefikia hapa leo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa heshima na taadhima nimesimama hapa kusema Mheshimiwa Rais tuliyenaye leo sio wa kawaida tumepewa zawadi kutoka kwa Mungu. Kwa maana ukisafiri mataifa mengine wanauliza huyu Rais wenu ni nani na amepata wapi ujasiri wa kufanya haya mambo yote? Naamini ni nguvu za Mungu na pia ameamua kuwakomboa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania ametukomboa kupitia nidhamu ya kazi. Tanzania nidhamu ya kazi ilikuwa imeshuka lakini yeye ameamua kuisimamia nidhamu hasa katika Serikali. Namshukuru sana na kumpongeza, tunamwombea kwa Mungu aendelee na moyo huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wanasema sisi wanawake ni wanyonge lakini ninaamini sisi siyo wanyonge, akina mama ni Taifa kubwa. Mheshimiwa Rais ametupigania kwenye uzazi kutoka vifo 11,000 hadi 3,000, tunamshukuru sana. Hii ni kazi tuliyopewa na Mungu kwamba mwanaume atakula kwa jasho lakini mwanamke atazaa kwa uchungu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwanamke atazaa kwa uchungu lakini ukiliangalia sana katika Taifa letu sasa hivi au katika hili Bara la Afrika mwanamke ana kazi kubwa, yeye anazaa kwa uchungu na bado anakula kwa jasho. Kwa hiyo, ndugu zangu akina mama naomba tusimame kifua mbele hasa Rais wetu kwa jinsi anavyotutetea katika nyanja zote ambazo wenzangu wamezitaja sina budi kuzirudia, upande wa elimu, afya, maji ametutua ndoo, miundombinu na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naomba nijikite katika sehemu moja ya ukurasa wa 39. Naomba ninukuu: “Tutashughulikia pia kero mbalimbali za wananchi ikiwemo migogoro ya ardhi na mirathi.” Mimi naomba nijikite upande wa mirathi. Kwa nini nilisema wanawake ni Taifa kubwa, wanawake tuna nguvu? Anayepata shida katika miradthi ni mwanamke ndiyo maana namzungumzia mwanamke na mtoto. Mwanamke ni nani? Mwanamke ni mama mzazi, ni mlezi, ni daktari, ni mwalimu na ni hakimu kwa wakati mmoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwanamke anapendeza anapoolewa tunamvisha nguo nyeupe, lakini mwanamke huyu siku akifiwa ananyanyasika, hasa wa Kitanzania. Kwa nini huyu mwanamke ananyanyasika kiasi hiki ambapo yawezekana ile mali waliyoichuma wakati mume wake akiwa hai yeye alichuma zaidi kuliko mume wake? Yawezekana alikuwa na kipato kikubwa kuliko mume wake lakini mwanaume akifariki mwanamke yule anakuwa si kitu wala si chochote? (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele imegonga Mheshimiwa, ahsante sana.

MHE. ALEKSIA A. KAMGUNA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tuiangalie hii sheria ili tubadilishe mwanamke aweze kuthaminiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, nashukuru sana. (Makofi)