Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Stella Ikupa Alex

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi ya kuweza kuchangia hotuba hii ya Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Kabla sijaendelea naomba niunge mkono hoja hii iliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote naomba nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa upendeleo mkubwa alionipatia na kuweza kuingia tena ndani ya Bunge hili ambalo mimi ni mara yangu ya pili, Bunge la Kumi na Mbili. Pia naomba nitumie nafasi hii kukishukuru sana Chama changu cha Mapinduzi kwa kuweza kutenga nafasi maalum kwa kundi la watu wenye ulemavu, nafasi ambazo zilikiwezesha chama kunichagua mimi kuwa Mbunge wa Bunge hili la Kumi na Mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba nitumie nafasi hii kuwashukuru sana akinamama wa Mkoa wa Dar es Salaam kwa jinsi ambavyo wameendelea kuniamini, pia akina mama wa UWT, Baraza Kuu ambao wameniwezesha tena kuingia ndani ya Bunge hili niweze kuwakilisha wanawake, watu wenye ulemavu pamoja na Watanzania wote kwa ujumla. Ahsanteni sana akinamama, nawaahidi ya kwamba sitawaangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nitumie nafasi hii kuishukuru sana familia yangu, lakini pia watumishi wa Mungu ambao wamekuwa wakiniombea mchana na usiku, maombi ambayo yameniwezesha kutekeleza majukumu yangu ipasavyo kila iitwapo leo. Naomba niendelee kutumia nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais John Pombe Joseph Magufuli, jembe letu, tingatinga kwa ushindi mkubwa ambao ameupata katika uchaguzi uliopita.

Mheshimiwa Naibu Spika, najaribu kuwaza kwa sauti, hivi Watanzania tungekuwa ni watu wa aina gani na kwa kweli niseme hata shetani angeweza akatushangaa kumnyima kura Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa hospitali hizi alizotujengea, lakini kwa umeme huu aliotuletea, barabara na pia kwa jinsi ambavyo alihakikisha kwamba kizazi chetu kinasimama imara kwa kukomesha dawa za kulevya. Kwa jinsi ambavyo ameweza kusimamia vitendo vya rushwa na kutokomeza kabisa rushwa ndani ya Taifa letu. Hakika shetani angeweza kutushangaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yako mambo mengi ambayo Mheshimiwa Rais ameyafanya, lakini katika hotuba zake, nimesoma hotuba yake vizuri, nimeirudia tena hotuba yake ya mwaka 2015 na ya 2020. Hotuba hizi zimejieleza vizuri na zinaonesha kabisa ni kwa jinsi gani Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli amedhamiria kulitoa Taifa letu kutoka sehemu moja na kulipeleka sehemu nyingine lakini pia ameweza kuonesha kwa vitendo katika awamu yake ya miaka mitano.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunamshukuru sana tukiwa kama Watanzania, lakini pia kwa kundi la watu wenye ulemavu hatuna budi kuendelea kumshukuru sana Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa jinsi ambavyo ameendelea kuyasimamia masuala ya watu wenye ulemavu na kuhakikisha kwamba kundi la watu wenye ulemavu na lenyewe linapata heshima katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nishauri mambo mawili kwa upande wa kundi la watu wenye ulemavu na hasa kwenye eneo la matibabu. Wakati wa kampeni niliweza kutafuta kura pia kwenye kundi la watu wenye ulemavu na changamoto mojawapo ambayo waliiongelea ilikuwa ni changamoto ya matobabu ambapo hapo kabla kulikuwa na utaratibu ambao ulikuwa unatumika, utaratibu wa utambulisho. Yaani mtu mwenye ulemavu anapoumwa yule ambaye hana uwezo, basi anaenda kwa mtendaji wa Kijiji ama Mwenyekiti wa Kijiji na hatimaye anaweza kutibiwa. Waliweza kuniambia kwamba utaratibu huu sasa hivi hauko vizuri sana, kwa hiyo suala la matibabu kwao inakuwa ni changamoto. Niiombe Serikali sana iweze kuuhuisha utaratibu huu wakati tunasubiri sasa ule mfumo wa Bima ya Afya kwa watu wote ili sasa kundi hili la watu wenye ulemavu liweze kunufaika na utaratibu wa matibabu kwa wale ambao hawana uwezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba nitumie nafasi hii kuweza kuishauri Serikali na kuiomba na kuungana na Wabunge wenzangu waliotangulia kwenye eneo la TARURA.

Tumeona kwamba mabadiliko ya tabianchi yameendelea kutuathiri sana na hivyo mvua za mara kwa mara zimekuwa zikiathiri miundombinu yetu. Kwa hiyo, niiombe Serikali iweze kuipa nguvu kubwa TARURA ili sasa hii miundombinu yetu iweze kuwa vizuri wakati wote. Mara nyingi tunapokuwa tunawasiliana na TARURA kama Wabunge wanalalamikia changamoto ya bajeti, kwa hiyo niiombe sana Serikali iweze kuliangalia hili na kulipa kipaumbele ili sasa miundombinu yetu iweze kuwa vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tuendelee kumwombea Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ili aendelee kuliongoza Taifa letu na Mwenyezi Mungu aendelee kumpa hekima na maarifa ya kuliongoza Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi. (Makofi)