Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa ridhaa yako kwa sababu ni mara yangu ya kwanza kusimama katika Bunge lako hili Tukufu, naomba nitumie fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, lakini pia kukishukuru Chama changu Cha Mapinduzi kwa kunipa ridhaa ya kupeperusha bendera katika Jimbo la Newala Vijijini. Pia nipongeze na kuishukuru familia yangu kwa support wakati wote wa uchaguzi hadi sasa. Kipekee pia niwashukuru wapigakura wa Jimbo la Newala Vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nami nianze kwanza kwa kuunga mkono hoja na hotuba ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa Novemba, 2020 pamoja na ile ya 2015. Ni hotuba ambazo nimepitia zote, hotuba ambazo zina maono, hotuba ambazo kwa namna ya kipekee, hasa ile ya 2015, ilipotekelezwa pamoja na Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ilikifanya Chama Cha Mapinduzi kutembea kifua mbele wakati wa Uchaguzi wa Mwaka 2020. Nina imani hotuba hii ambayo ameitoa 2020 tukiitekeleza hivi inavyotakiwa 2025 itakuwa ni kuteleza kama kwenye ganda la ndizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais amefanya mambo mengi, tumeyaona. Amesimamia vizuri miundombinu katika nchi hii kuanzia afya, barabara, elimu na sekta nyingine zote. Tunampongeza sana kwa kile ambacho amekifanya kwa kusaidiana na wasaidizi wake ambao ni Mawaziri wetu. Hata hivyo, zipo changamoto kadhaa ambazo zikisimamiwa na kutekelezwa ipasavyo nadhani nchi hii itasonga mbele sana zaidi ya hapa ambapo tupo sasa hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Mkoa wa Mtwara wanazalisha kwa kiasi kikubwa zao la korosho, zao ambalo linaipatia nchi hii uchumi na fedha nyingi za kigeni, lakini kuna changamoto ya barabara yetu ya kiuchumi, barabara ambayo inatumika kupitisha zao la korosho kutoka kwenye maeneo ya wakulima kuelekea bandarini. Barabara ile imeshaombewa muda mrefu lakini haikamiliki. Ni barabara ya kutoka Mtwara – Nanyamba – Tandahimba – Newala – Masasi hadi Nachingwea. Barabara ile hadi sasa imekamilishwa kwa kiwango cha lami kwa kilometa 50 tu. Niombe wenzetu wa Ujenzi kuharakisha ukamilishaji wa barabara ile ili mazao ya wakulima yapate kusafirishwa kwa urahisi kuelekea bandarini, lakini pia kuvinusuru vyombo ambavyo vinasafirisha mazao hayo kuelekea bandarini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Newala ambayo ipo Jimbo la Newala Vijijini imehamia mwaka jana katika eneo lake jipya la utawala. Eneo lile halina jengo la utawala na kwenye hotuba tumeelezwa na kusisitizwa suala la utawala bora. Utawala Bora ni pamoja na kuwepo na maeneo ya watumishi kutendea kazi, lakini Halmashauri ya Wilaya ya Newala haina jengo la Utawala. Niombe wahusika na wasimamizi wa masuala ya utawala kwa maana ya TAMISEMI watuangalie kwa jicho la pekee ili watumishi wale wapatiwe jengo la utawala nao wafanye kazi katika mazingira yaliyoboreshwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo la Newala Vijijini kuna changamoto ya maeneo ya kutolea huduma ya afya. Zipo kata 22 lakini ni kata tatu tu ndizo ambazo zina vituo vya afya. Naomba Mheshimiwa anayesimamia afya atuangalie kwa jicho la kipekee tupate vituo vya afya…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Muda wako umekwisha Mheshimiwa, ahsante sana.

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naunga mkono hoja. (Makofi)