Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Salum Mohammed Shaafi

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Chonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. SALUM MOHAMMED SHAAFI: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nitumie fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kunijalia leo kuwepo katika Bunge hili Tukufu. Pia nitumie fursa hii kuwashukuru wale wote waliosababisha kwa namna moja ama nyingine nami kuwa Mbunge wa kuchaguliwa Pemba. Nawashukuru sana wananchi wangu wa Chonga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja kujadili hotuba ya Mheshimiwa Rais. Miongoni mwa mambo aliyoyajadili Mheshimiwa Rais ni suala zima la kudumisha Muungano. Muungano huu umeunganisha nchi mbili; ulikuwa ni Muungano uliounganisha Tanzania Bara na Tanzania Visiwani Zanzibar.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Wanzanzibar, sisi Watanzania tunahitaji Muungano wa haki, usawa na wa kuheshimiana. Naomba ifahamike sisi Zanzibar tunayo Mahakama Kuu ambayo ina mamlaka ya kusikiliza kesi zinazohusu masuala ya Zanzibar. Nilikuwa najiuliza maswali na kupata ukakasi mkubwa sana iweje leo kesi inayopaswa kusikilizwa Zanzibar ihamishiwe Tanzania Bara? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukirudi tuna kesi kadhaa, natolea mfano kesi ya uamsho. Hili dai liko mahakamani linaendelea, sipendi kuingilia Mhimili wa Mahakama, lakini najiuliza sasa ni takribani miaka nane, kesi hii bado iko kwenye upelelezi, bado haijakamilika ushahidi wake. Je, hakukuwa na mamlaka kwa Mahakama Kuu ya Zanzibar kusikiliza kesi hii mpaka iletwe Tanzania Bara? Hebu tunaomba Serikali mtuambie nini shida watu hawa hadi leo; tunahitaji tuwatendee haki Wazanzibari wale.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie fursa hii kumwomba Rais huyu, Rais msikivu, Rais mtetea wanyonge, Rais anayesema aombewe, nimwombe Mheshimiwa Rais; kama walivyoachiwa wale Waethiopia na hawa Wazanzibari na wao tuwaachie. Kama walivyoachiwa Waethiopia wale, Wazanzibari hawa na wao Mheshimiwa Rais awahurumie, atumie nafasi yake ya Urais kuhakikisha Wazanzibari hawa na wao tunawatendea haki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende katika suala la mchakato wa Katiba Mpya, ni sehemu ambayo Mheshimiwa Rais aligusia. Katiba hii tutakapoipata tutatatua changamoto na matatizo mbalimbali yanayotuhusu Wazanzibari na yanayotuhusu Watanzania.

Leo najiuliza, iweje referee anachezesha ndani ya uwanja halafu yeye huyo huyo anakuwa ndiye mchezaji wa mpira, anakuwa ndio muamuzi; kweli tutakuwa tuna Tume huru? Tunahitaji Tume huru ili tuwaaminishe Watanzania chaguzi hizi zinavyofanywa ni uchaguzi huru na haki.

Mheshimiwa Naibu Spika, humu leo sote kila mmoja anafahamu ni namna gani alivyoingia humu. Sote tunajuana humu; waliongia kushoto wanajua, waliongia kulia wanajua, kila mmoja na siri yake. Uchaguzi ulikuwa ni uchaguzi wa shida, ulikuwa ni uchaguzi mtihani. Leo humu wengine ukiwauliza, aah kwani bado mimi ni Mbunge? Ni mtihani mtupu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme Taifa hili tunasema tuliombee, hatuwezi Mungu akatupa mafanikio makubwa kama dhuluma inatawala ndani ya nchi hii. Dhuluma ni adui wa haki. Tutakuwa tunadhulumu lakini mafanikio hatuyapati.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa, Kanuni.

MHE. SALUM MOHAMMED SHAAFI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. SALUM MOHAMMED SHAAFI: Naomba niendelee kusema. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante. Mheshimiwa uliyekuwa unataka kutoa taarifa uniwie radhi, sikuona uko upande gani, kwa hiyo kengele imeshagonga.