Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mahitaji ya A-level kisiwani Ukerewe; Wilaya ya Ukerewe ambayo inaundwa na Visiwa na kwa maana hiyo ki-jiografia iko vibaya lakini tayari Wilaya ina shule za sekondari za Serikali 22 na za binafsi 2. Lakini pamoja na historia ya Wilaya hii kielimu kuwa nzuri hasa kwa kuzalisha vipaji vingi bado hakuna shule ya kidato cha tano na kidato cha sita. Tayari Halmashauri imeandaa shule ya Bukongo sekondari na Pius Msekwa Sekondari kuzipandisha kuwa za high school na tayari kibali kimepatikana. Ninashauri Wizara itoe ushirikiano wa kutosha na kufanikisha uanzishaji wa shule hizi ili kunusuru maisha ya vijana wengi ambao wanamaliza kidato cha Nne na kukosa nafasi ya kuendelea na kidato cha Tano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, posho ya mazingira magumu Ukerewe; kutokana na mazingira ya kijiografia kuwa magumu katika Visiwa vya Ukerewe, walimu wanafanya kazi katika mazingira magumu sana na wakati mwingine wanapopangiwa kuja Ukerewe kwa mara ya kwanza, Serikali haitoi kwa wakati pesa za kujikimu hivyo kuwapa shida sana walimu wetu. Ninashauri Serikali kupitia Wizara hii itoe kwa wakati pesa za nauli na kujikimu kwa walimu wanaopangiwa vituo kwa mara ya kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, itolewe posho ya mazingira magumu kwa watumishi hasa walimu wanaofanya kazi katika Visiwa vya Ukerewe ili iwape motisha katika kukubaliana na changamoto zilizopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upandishaji wa madaraja; Kumekuwa na malalamiko mengi sana toka kwa walimu yanayotokana na ucheleweshaji wa upandishaji madaraja sambamba na mishahara. Ushauri wangu ni kwamba Wizara ilisimamie jambo hili ili madaraja na mishahara vipandishwe kwa wakati kwa walimu wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, usimamizi wa walimu kiutumishi; Serikali kupitia Wizara ya Elimu iangalie upya namna ya muundo wa utumishi kwa walimu. Hali iliyopo sasa kwa walimu kusimamiwa na zaidi ya Wizara moja ni tatizo kwa watu hawa. Hivyo nashauri walimu wawe chini ya usimamizi wa Wizara moja tu badala ya hali ilivyo sasa ili kuongeza ufanisi wa kada hii.