Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Edwin Enosy Swalle

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupembe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hotuba za Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu leo ni mara yangu ya kwanza kuzungumza ndani ya Bunge lako Tukufu, naona basi ni vema nikatumia nafasi hii pia kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt John Joseph Pombe Magufuli na Mwenyekiti wa Chama chetu cha Mapinduzi na Halmashauri Kuu ya Chama chetu cha CCM kwa kuwa na imani kubwa na kupitisha jina langu kuwa Mbunge wa Bunge hili la Kumi na Mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais wetu amekuwa akiacha alama kila mahali. Ameacha alama kwenye nchi lakini pia ameendelea kuacha alama kubwa kwa sisi vijana wa nchi hii kwa kutuamini na kutupa nafasi. Mheshimiwa Rais ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ufupi sana napenda nitumie kama dakika moja pia kuwashukuru sana familia yangu ya Mzee Enosy na kipekee mke wangu mpenzi Tumaini anayelea wanangu wawili kwa ufasaha mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nijikite kwenye mchango wa hotuba za Mheshimiwa Rais. Nimesoma hotuba mbili za Mheshimiwa Rais, hotuba hizi zina sura mbili sehemu ya kwanza zinaeleza mafanikio makubwa ya miaka mitano iliyopita, lakini sehemu ya pili inaeleza mipango ya Serikali kwa miaka mitano ijayo. Tunavyompongeza Mheshimiwa Rais kwangu mimi nadhani pia ni muhimu sana kuwapongeza Makamu wa Rais, Waziri Mkuu wetu na Mawaziri wote waliopita kwa kazi nzuri waliyoifanya kwa ajili ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sote ni mashahidi, tulishuhudia Waziri Mkuu wetu Mheshimiwa Kassim Majaliwa Kassim, akizunguka hii nchi nzima kusimamia Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Mimi ni kati ya Wabunge ambao niliomba sana Mungu Mheshimiwa Majaliwa aweze kuendelea kuwa Waziri Mkuu na tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais Mwenyezi Mungu alimuonyesha akampa nafasi Mheshimiwa Waziri Mkuu ya kuendelea na utumishi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini maombi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kuendelea kuwa na nafasi ya Waziri Mkuu nilikuwa na sababu maalum. Pamoja na kazi nzuri sana ambayo Serikali imefanya kwa miaka mitano iliyopita na hasa kwenye kipengele cha kilimo, Waziri Mkuu ameshughulika sana kutatua kero za mazao mengi ya kimkakati. Tumemuona Waziri Mkuu akihangaika na zao la korosho katika nchi hii, pamba, mkonge na mazao mengine katika nchi hii. Hata hivyo liko zao moja ambalo katika miaka mitano iliyopita na hiki pengine ni kiporo ambacho naiomba Serikali katika mpango wake wa kuendelea kukuza ajira kwa wananchi wa Tanzania Serikali kupitia Waziri Mkuu awamu hii ya pili ya miaka mitano ya utumishi watazame katika zao la chai ambalo ni zao la kimkakati la Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo langu la Lupembe wananchi walisikiliza hotuba ya Mheshimiwa Rais. Ukiangalia kwenye ukurasa 12 wa hotuba ya Mheshimiwa Rais ya mwezi Novemba 2020, Mheshimiwa Rais aliwaahidi Watanzania pamoja na wananchi wa Jimbo langu la Lupembe kwamba anayo ndoto na angetamani sana wananchi wetu waweze kuwa mabilionea. Wananchi wa Jimbo la Lupembe wako tayari kuwa mabilionea na wamejiandaa kuwa mabilionea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye mchango wangu wa hotuba hii wamenituma kumuomba Mheshimiwa Rais mambo mawili ya msingi sana. Jambo la kwanza wananchi wa Lupembe wanasema pamoja na uchapa kazi, wanamuomba Mheshimiwa Rais awasaidie ahadi ya barabara ya lami kuanzia Kibena - Lupembe - Madeke - Morogoro. Barabara hii ikifunguka hata wewe Naibu ukitoka pale Mbeya utapita Jimbo la Lupembe kuelekea Dar es Salaam, lakini hata Waziri Mkuu mwenyewe anaweza kupitia barabara hii badala ya kupita barabara ya Iringa ambayo ni ndefu na ina milima mikali sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika jambo hili la zao la chai kuna changamoto kubwa sana katika Jimbo la Lupembe. Wananchi wengi wa Jimbo la Lupembe hawalipwi fedha zao na viongozi wengi wa Serikali wamekuja Lupembe wakipewa ahadi na wawekezaji kwamba wangelipa fedha hizi kwa wakati lakini mpaka leo tunavyozungumza Makamu wa Rais amekuja kapewa ahadi hii, Waziri Mkuu amekuja kapewa ahadi hii, Waziri wa Kilimo amekuja kapewa ahadi hii nilikuwa lakini utekelezaji hakuna.

Kwa mujibu wa Sheria yetu ya Makosa ya Jinai, kifungu cha 122 ni kosa kwa mtu kumweleza taarifa za uongo kiongozi wa umma na kwa kuwa wawekezaji hao wamekuwa wakitoa taarifa siyo za kweli kwa viongozi wetu wa Serikali, naiomba Serikali sasa ingewaita wawekezaji hawa waeleze ni kwa nini wasichukuliwe hatua kwa kuiambia Serikali au viongozi wetu taarifa ambazo hawawezi kutekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo la pili naomba niseme kidogo sana kwenye ajira. Naomba sana watu wa TRA waweke mazingira rafiki kwa vijana wetu, wanapofungua biashara wapewe grace period ya kuanza kulipa kodi angalau mwaka mmoja au miaka miwili.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya mchango huo, naunga mkono hoja, ahsante sana kwa nafasi hii. (Makofi)