Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Dr. Oscar Ishengoma Kikoyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muleba kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nichukue nafasi hii kumshukuru Rais wetu Dkt. John Joseph Magufuli. Pili, niunge mkono hotuba mbili zote alizozitoa Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukienda ukurasa wa 12 wa hotuba ya kufungua hili Bunge, Rais alisema: “Nataka Watanzania wote washiriki kikamilifu katika kujenga uchumi wa nchi yao.” Tunapoongelea uchumi jumuishi hii ndiyo falsafa yenyewe ambayo Rais anatuelekeza katika hotuba yake. Hata hivyo, hatuwezi kuwajumuisha Watanzania wote katika kujenga uchumi wa nchi yao kama hatujawawekea miundombinu ya kutosha. Ili kuhakikisha kwamba Watanzania wote wanashiriki katika uchumi wa nchi yao, lazima tuangalie sekta za kimkakati ambazo ni pamoja na kilimo na uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiongelea kilimo, nchi yetu bado inategemea kilimo katika kuzalisha mazao ambayo tunauza nje. Tunayo mikoa ya kimkakati ambayo ni wazalishaji wakubwa wa mazao ya kilimo na biashara. Hatuwezi kuwa na kilimo chenye tija kama tunaendelea na kilimo cha jembe la mkono na cha kutegemea mvua, jua na kiangazi, lazima twende kwenye kilimo cha umwagiliaji maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo langu la Muleba Kusini tunayo miradi miwili ya umwagiliaji maji. Tunao mradi wa Kyamyorwa ambao Serikali yetu Tukufu imeugharamia kushirikiana na wadau wengine, tekeo tayari, mfereji umejengwa, tumebakiza banio. Niiombe Wizara ya Kilimo ikamilishe mradi huu ili wananchi wa Kyamyorwa na Muleba na Mkoa wa Kagera kwa ujumla wake waweze kufaidi na kuendeleza kilimo cha umwagiliaji maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunao mradi mwingine wa Buhangaza ambao umejengwa lakini haujakamilika. Hii miradi imetumia fedha za walipa kodi, niisihi, kuiomba na kuishauri Wizara ya Kilimo, miradi hii ikamilishwe ili iweze kuzalisha kulingana na pesa tulizoziwekeza pale ili wananchi wanufaike na miradi hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Kagera unapakana na nchi nyingi jirani kama Rwanda, Uganda na Burundi. Tukitumia fursa tulizonazo katika Mkoa wa Kagera ambaapo tunalo bonde la Mto Ngono ambalo linafaa kwa ajili ya kilimo na uzalishaji mkubwa wa chakula, tukiweza kuwekeza katika bonde hilo Mkoa wa Kagera unaweza ukawa soko la chakula kwa ajili ya nchi zote zinazozunguka mkoa wa Kagera.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye sekta ya uvuvi. Sekta hii inaajiri vijana wengi na nitajikita katika Ziwa Victoria ambako mimi natoka. Ukiangalia kazi zinazoendelea katika Ziwa Victoria sisi kama Tanzania tunamiliki asilimia 51 ya ziwa lile, wenzetu wanamiliki asilimia 49, Uganda wana asilimia 43, Kenya wana asilimia 6 lakini ukiangalia mauzo nje ya nchi inaonekana sisi tunauza kidogo kuliko wenzetu ambao wanamiliki eneo dogo la Ziwa Victoria. Kwa nini inakuwa hivyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, jana kuna Mbunge hapa alichangia kuhusu sekta ya mifugo, ukiangalia kwa nini hatufanyi vizuri katika mauzo ya nje kama Rais anavyotuambia biashara ni vita, mfumo wa tuzo zinazotozwa kwenye mazao yanayotokana na uvuvi na ukilinganisha na nchi za jirani, sisi tozo zetu ziko juu sana. Niishauri Wizara ya Uvuvi kuhakikisha kwamba tunapitia tozo zote ambazo zinatozwa kwenye mazao ya samaki. Tuhakikishe kwamba zile tozo aidha zinalingana na nchi jirani au kwa kuwa tuna eneo kubwa la ziwa tunaweza tukafanya ujanja tuka under cut tuwe na tozo za chini ili tuweze kuvuna na kuuza nje mazao mengi ya uvuvi. Vinginevyo tutabaki nyuma, tutabaki kulalamika lakini jambo la msingi tupitie tozo kama nilivyoshauri ili tuweze kupata pesa za kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine kwenye sekta ya uvuvi, Wilaya yangu ya Muleba ina visiwa 39 na visiwa 25 vinakaliwa na wavuvi. Ilipokuja hii ya sera ya kukamata wavuvi haramu, siwaungi mkono lakini nawaomba na nishauri Wizara ya Uvuvi, busara itumike tunapokwenda kwenye zoezi la kuwakamata wavuvi haramu. Kinachoendelea sasa imekuwa kama kukomoana na kuna kesi nyingi ambazo zinaendelea watu wanakamatwa, wanafunguliwa kesi na wakati mwingine kesi zenyewe ukiziangalia hazina hata ushahidi wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Bukoba tumejengewa Chuo cha VETA. Nimshukuru Rais wetu na Serikali yetu Tukufu. Nategemea Waziri wa Elimu, kati ya mitaala itakayoendeshwa kwenye Chuo kile cha VETA tuwe na mtaala ambao unawafundisha vijana wetu kutengeneza nyavu na vifaa ambavyo tunavitumia katika sekta nzima ya uvuvi kwa sababu Mkoa wa Kagera na Mikoa ya Kanda ya Ziwa inategemea sana uvuvi katika uchumi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nashukuru sana na naunga hoja mkono hotuba zote mbili na hotuba zote zilizotangulia kabla ya hizo. (Makofi)