Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, kabla sijachangia nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa nguvu na uhai kuwepo katika Bunge hili. Kipekee, niwashukuru wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa ambao wameniamini tena kwa mara nyingine na kunipa kura nyingi za kishindo ambazo zimenirudisha katika jengo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikichangia kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais, kwa kweli niseme ukisikia na ukisoma vizuri kwenye hotuba hii, hotuba hii imejaa matumaini na neema kubwa sana kwa Watanzania. Mimi nachosema wasaidizi wake ambao Mheshimiwa Rais amewaamini, niombe wachukue hatua ambazo zitaibeba hotuba hii na kuifanyia kazi. Kwa nini nasema hivyo? Mara nyingi wakati mwingine viongozi wetu wanaongea mambo mazuri na makubwa lakini yanaishia kwenye vitabu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kwanza niongelee upande wa kilimo, tunaongelea Tanzania ya viwanda. Wazalishaji wakubwa wako vijijini, lazima tuwekeze nguvu kubwa kwa wakulima wa hali ya chini na ili tuweze kufanikiwa lazima tuandae miundombinu mizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge wamekuwa wakichangia kuhusu TARURA, ni ukweli usiopingika kuwa mtandao wa barabara nyingi sana uko kule kwa wananchi wa hali ya chini na ndiyo wazalishaji wakubwa. Mimi nashindwa kuelewa, kwa nini hili jambo tumeshauri muda mrefu toka Bunge lililopita lakini bado halijatatuliwa naomba Serikali ilione hili jambo ni la muhimu. Tunaongelea Tanzania ya viwanda, hatuwezi tukafanikiwa kwenye viwanda vyetu kama hatutaboresha miundombinu mizuri kwa wananchi wetu wa hali ya chini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kwa mfano kule vijijini, mimi niongelee kwa mfano Kyerwa, barabara hali ni mbaya lakini haohao ndiyo wazalishaji wakubwa. Ukienda kwa Mkoa wa Kagera, ndizi zinazotoka Kagera ndizo zinalisha nusu ya Tanzania. Tusipoboresha mazingira haya yawe mazuri huyu mkulima akaweza kusafirisha mazao yake vizuri, hatutaweza kufanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini siyo hilo tu; malighafi nyingi tunategemea zitoke kwa hawa wananchi wa hali ya chini. Tusipoboresha haya mazingira mazuri, tukaweka miundombinu mizuri, tutaishia kuchukua malighafi kule nje kuwanufaisha watu wa nje badala ya kutumia malighafi ambazo zinazalishwa hapa kwetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe sana Mawaziri ambao wanahusika suala la TARURA walitilie mkazo.niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge, suala hili ni kwa faida yetu sote. Tuombe sana Wizara inayohusika na TARURA itengewe pesa, kama haitatengewa pesa sisi ndiyo tunaopitisha bajeti, haiwezekani tukae tunazungumza mambo hayafanyiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine, nimekuwa nikishangaa, ukienda kwenye vyuo vyetu, kwa mfano kile Chuo cha NIT, tuna wataalam ambao wanaweza wakatengenezwa pale kusimamia miradi yetu mikubwa. Leo hii tunao Mradi wa SGR, mradi huu unajengwa na watu kutoka nje lakini Serikali imejipanga vipi kuandaa wataalam ili hawa waliojenga huu mradi wakishaondoka tupate wataalam wetu?

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiwasikiliza wale watu wa NIT wanakwambia mtaalam mmoja kwenda kusoma nje anatumia zaidi ya milioni 200, lakini wao kumuandaa mtaalam huyohuyo wanatumia milioni 25, lakini unakuta chuo hichohicho Serikali bado haijawekeza nguvu. Sasa hili na lenyewe lazima tuliangalie, vinginevyo hii miradi mwisho wa siku itakosa wataalam wetu wa kusimamia. Jambo ambalo unalisimamia wewe mwenyewe hata kama mradi ni wako unakuwa na ule uzalendo. Haya masuala ya miradi kusimamiwa na watu wengine, tunakwenda kutafuta wataalam nje, hili jambo halijakaa sawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais kwenye hotuba yake amezungumzia miradi mingi ya maji. Kwa kweli tuseme ule ukweli, miradi mingi ya maji bado haijafanikiwa. Unakuta hapa wamedonoa kidogo, hapa wamegusa kidogo. Niiombe sana Serikali tusianze kufanya usanifu miradi mipya, tukamilishe ile miradi ya zamani ndiyo tuanze na mingine. Hili suala la kushika hapa kidogo tuonekana tuna miradi mingi ambayo haina manufaa hatutaweza kufika mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano Kyerwa tuna mradi wa maji wa vijiji hamsini na zaidi, mradi huu ukikamilika naamini utanufaisha wananchi zaidi ya laki mbili. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali, tunapoanzisha miradi hasa hii ya maji basi ikamilike kuliko tunagusa kidogo, Serikali inaonekana tuna miradi mingi sana lakini mwisho wa siku hatuikamilishi. Kwa hiyo, niombe hili na lenyewe tuliangalie. Tutakapokuwa tumehakikisha hawa wananchi wetu wamepata maji, nina uhakika hata uzalishaji utakuwa mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine ambacho napenda kukiongelea ni barabara zetu kuu, kwa kweli ni jambo ambalo linasikitisha. Ukienda kwa mfano mpakani kwetu na Uganda ni aibu. Kule kwetu unaweza ukafikiri ni uchochoro kule kwao ni Ulaya. Hizi barabara ambazo zinaunganisha nchi na nchi niombe sana tuweze kuzikamilisha ili na sisi tuonekane ni sehemu ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru. (Makofi)