Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Zaytun Seif Swai

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Awali ya yote, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu na vilevile naomba niwashukuru wananchi wangu wa Mkoa wa Arusha hususan kinamama wa Mkoa wa Arusha kwa kuniamini kuwa mwakilishi wao katika Bunge hili. Nawaahidi wananchi wangu hususan kinamama wa Arusha sitawaangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee kabisa, naomba nishukuru familia yangu wakiongozwa na mama yangu mpendwa mama Sifa Swai, mume wangu na mtoto mpenzi Alina. Wote hawa kwa nyakati tofauti wamekuwa wakinishauri vyema jinsi gani ya kuwaongoza wananchi wetu na vilevile wananiongezea busara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie hotuba ya Rais, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze na suala la elimu. Serikali imefanya mambo makubwa sana kwenye awamu zilizopita kwenye suala la elimu na yote haya imeyafanya kwa sababu inatambua umuhimu wa elimu na mchango wake mkubwa katika uchumi wa Taifa letu. Kutokana na umuhimu huu, Rais ameeleza mambo mbalimbali yanayohusiana na elimu katika hotuba yake na majawapo ikiwa ni kuanzisha shule za sayansi za watoto wa kike katika kila mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, binafsi ni mnufaika wa elimu iliyotolewa bure na Serikali katika masomo haya ya sayansi na hisabati. Kwa hiyo, natambua vizuri changamoto wanazozipata watoto wa kike katika masomo haya na naipongeza Serikali kwa kuamua kuanzisha shule hizi ili kutatua changamoto zile. (Makofi)

Mheshimia Naibu Spika, naomba niishauri Serikali, suala la shule za sayansi ni muhimu sana na linatakiwa lichukuliwe kwa umuhimu wake. Shule hizi zinahitaji umakini mkubwa kwenye kuziendesha. Kwa kuanza zinahitaji kuwa na ubora wa hali ya juu, maabara zenye viwango vya juu na walimu wenye uwezo mkubwa wa kuwafundisha wanafunzi hawa. Vilevile shule hizi zinahitaji nyezo mbalimbali kama vitabu na kadhalika. Kwa hiyo, naiomba Serikali isikurupuke kwenye suala hili, iliangalie kwa umakini na tuhakikishe shule hizi zinajengwa kwa umakini wa hali ya juu tukizingatia hayo mambo niliyotaja ili basi lengo la Serikali liweze kutimia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi sote ni mashuhuda, tumeshuhudia jinsi halmashauri zetu zinavyopata shida sasa hivi kujenga madarasa na kutafuta madawati katika shule mbalimbali na wananchi wetu pia wanalalamika kwa sababu michango ni mikubwa kusaidia maendeleo haya. Kwa hiyo, naiomba Serikali suala hili la ujenzi wa shule za sayansi kwa watoto wa kike isilichukulie juu bali ilichukulie kwa umakini na tulianze suala hili mapema tusisubiri mpaka mwisho wa miaka mitano ili tuweze kuzijenga shule hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba vilevile niongelee suala la mikopo ya asilimia 10 inayotolewa kutokana na mapato ya halmashauri. Tumeona jitihada kubwa sana za Serikali inazofanya kuwawezesha wananchi wake kiuchumi kupitia mikopo isiyokuwa na riba na mikopo mingine yenye riba nafuu na vilevile kupitia mifuko na program mbalimbali zilizoanzishwa na Serikali. Mikopo hii ya asilimia 10 inatolewa kulingana na mapato ya halmashauri husika na sisi sote tunajua kwamba halmashauri zote hazilingani kimapato. Kwa hiyo, formula hii haizingatii halmashauri zenye changamoto ya vyanzo vya mapato. Mikopo hii isiwe ni adhabu kwa wanufaika walioko vijijini na sehemu zenye changamoto za mapato. Naiomba Serikali iweze kuangalia formula hii kwa undani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitatolea mfano mdogo tu, hauwezi kulinganisha mapato ya Ilala, Kinondoni na halmashauri za Ngorongoro, Longido au Monduli na sehemu zingine za vijijini. Kwa hiyo, tunaomba Serikali yetu iangalie fomula hii na iweze kugawa mikopo hii kwa usawa. Suala hili pia litapunguza gap lilipo la umaskini wa vijijini na mijini ambapo nadhani ndiyo lengo kubwa la Serikali yetu, tupunguze gap la umaskini lililopo kwa sasa vijijini na mijini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naomba nichangie kwenye sekta ya maji. Nashukuru Mheshimiwa Rais bado anatambua kuna changamoto nyingi za maji, hususan vijijini. Serikali yetu imefanya mambo mengi sana hasa kutekeleza miradi mikubwa ya maji ikiwemo mradi wa shilingi bilioni 520 ulioko Mkoani Arusha. Naomba niishauri Serikali isiwekeze tu kwenye miradi mikubwa kama hii vilevile iangalie vyanzo vingine vya maji ikiwemo uchimbaji wa visima virefu. Nitatolea mfano tu, mradi huu wa shilingi bilioni 520 unapita Wilaya ya Arumeru lakini kuna kata katika Wilaya ya Arumeru kama Kata ya Nduruma haina maji. Kwa hiyo, naomba Serikali iangalie pia vyanzo vingine vya maji ukiachia mbali miradi hii mikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. (Makofi)