Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Kasalali Emmanuel Mageni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sumve

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa uzima na afya njema na kuniwezesha kufika hapa nilipofika. Kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kuzungumza kwenye Bunge hili, naomba nitumie fursa hii kuwashukuru wananchi wa Jimbo la Sumve kwa ushindi mkubwa waliokipatia Chama Cha Mapinduzi katika uchaguzi uliopita. Nikishukuru Chama Cha Mapinduzi kwa kunipitisha na kunisimamia na kuhakikisha nashinda kwa kishindo katika uchaguzi uliopita.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nijielekeze katika hoja iliyoko Mezani. Katika Nchi ya Tanzania, baada ya mimi kuangalia hizi hotuba, hotuba ya Mheshimiwa Rais ya kulifungua Bunge na nimepitia hotuba ya mwaka 2015 aliyoitoa wakati akilifunga Bunge la Kumi na Moja, nimeona kwamba Nchi yetu ya Tanzania inayo bahati kubwa. Tumempata Rais ambaye anayo maono, tumempata Rais ambaye ana nia ya dhati ya kulitumikia Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Taifa la Tanzania ni moja ya mataifa machache yenye bahati ya kuwapata viongozi wa aina ya Dkt. John Pombe Magufuli. Ukiangalia mipango yote na namna ambavyo Serikali ya Awamu ya Tano imejipanga na ilivyokuwa imejipanga katika kipindi cha kwanza na ilivyojipanga katika kipindi cha pili, unayaona matumaini ya Tanzania itakayokuwa ni nchi yenye uchumi mkubwa. Kwa hiyo ninayo sababu ya msingi ya kujivunia kwamba Watanzania tunaye Rais mwema, mwenye maono na ambaye anataka kutuvusha, anataka twende sehemu ambayo wote tumekuwa tukitamani kufika.

Mheshimiwa Naibu Spika, mambo mengi yamefanywa na Serikali yetu, tunaweza tukazungumza hapa lakini muda usitoshe. Nitajaribu kuzungumza machache ambayo yamefanyika na kushauri nini tufanye vizuri zaidi. Serikali ya Awamu ya Tano katika jambo kubwa ambalo imelifanya ambalo dunia nzima inaona na tunajivunia ni kuhakikisha inasimamia vizuri uzembe, ufisadi na ubadhirifu wa mali za umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali yetu imeweka utaratibu kuanzia Mheshimiwa Rais akisimama, ukiwaona Mawaziri wake wamesimama, wote wanakemea namna yoyote ya uzembe, namna yoyote ya ubadhirifu na ufisadi wa mali za umma. Serikali ya Awamu ya Tano imefanya vizuri sana kwenye jambo hilo; majizi, mafisadi wameshughulikiwa vizuri na kila namna ambayo Serikali imeona inaweza kufanya kuhakikisha mali zetu, mapato yetu tunayoyakusanya yanakuwa salama, Serikali ya Awamu ya Tano imefanya vizuri sana na matunda tumeyaona.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kwenye ukusanyaji wa mapato kupitia TRA na halmashauri zetu, tumefika kiwango cha kuongeza mapato ya mwezi kutoka bilioni 800 mpaka mwezi uliopita tumeweka rekodi ya kukusanya trilioni mbili, mwezi Desemba; Serikali imefanya vizuri sana kwenye hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini yapo mambo ambayo yanahitaji kuangaliwa kwa undani zaidi. Katika kusimamia ubadhirifu wa mali za umma na matumizi mabaya ya fedha za Serikali, Serikali yetu katika kiwango cha Kitaifa, katika taasisi zilizoko karibu na Serikali kama maeneo ya bandari na maeneo mengine tumefanya vizuri sana. Hata hivyo, kwenye maeneo ya chini, kama kwenye Halmashauri za Wilaya kazi kubwa inahitajika kufanyika. Fedha nyingi za matumizi zinazopelekwa kwenye Halmashauri zetu hazitumiki inavyotakiwa. Bado kuna miradi hewa, kuna usimamizi mbovu wa fedha na fedha nyingi zinapotea. Hata viwango vya majengo na miradi inayosimamiwa na Halmashauri zetu hazijafikia viwango vinavyotakiwa. Kwa hiyo, Wizara husika, ambayo ni TAMISEMI, wanatakiwa kuziangalia Halmashauri kwa jicho la pili.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumefanya vizuri sana kwenye sekta ya kilimo kufufua ushirika na mambo mengine, lakini bado kuna mambo ya kufanya kwenye ushirika. Naweza nikakupa mfano, katika Wilaya yetu ya Kwimba kuna shida kubwa sana sasa hivi inaendelea. Kuna mazao ambayo Serikali imeyaweka kusimamiwa na ushirika ambayo kiuhalisia hayakupaswa kusimamiwa na ushirika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna zao la choroko na mazao mengine kama ufuta, yamewekwa kwenye ushirika lakini mazao haya siyo kama mazao mengine yaliyoko kwenye ushirika kama pamba. Mazao haya ni ya chakula, ni mazao ambayo uuzaji na usimamizi wake unapaswa uwe wa kawaida na usitegemee AMCOS na ushirika. Katika Wilaya Kwimba, moja ya jambo ambalo linatutesa sasa hivi ni mazao yetu ya choroko kupelekwa kwenye ushirika na tunalazimishwa mazao ambayo ni ya chakula, mazao ambayo sisi muda wote tunayategemea, tukitaka kuuziana ni lazima twende kwenye AMCOS.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niiombe Serikali kwamba umefika wakati wa kuangalia ushirika wetu. Tumeuimarisha ushirika, unafanya vizuri lakini tunauongezea majukumu ambayo ni magumu kuyafanya. Moja ya jukumu ambalo ushirika unapata shida kulifanya ni hili la ununuzi wa choroko, dengu na mazao mengine ambayo ni mazao yetu ya chakula na biashara, kuna wakati tunahitaji kuyatumia kama mazao ya chakula. Mimi siwezi kuhitaji kununua choroko ikabidi niende kununua AMCOS, nitanunua kwa mtu mwenye choroko. Naomba sana katika suala hili Serikali kupitia Wizara ya Kilimo ione namna ya kuhakikisha mazao yaliyoongezwa kwenye ushirika yanarudishwa, tunaanza kuyanunua kwa njia zetu za kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na naomba niunge mkono hoja ya Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)