Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Awali ya yote, naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa wema wake kuweza kusimama mahali hapa na mimi niwe mmojawapo wa wachangiaji wa hotuba ya Mheshimiwa Rais ya tarehe 13 Novemba, 2020.

Mheshimiwa Spika, hotuba ya Rais imegusia vitu vingi sana lakini kipo kitu kimoja ambacho wenzangu hawajakisema sana, mimi naomba niweke wazi. Nchi yetu kweli kila mmoja anatamani kwamba tuwe mabilionea lakini binafsi ninavyoangalia hatuwezi kuwa mabilionea kwa sababu ya tatizo la rushwa Rushwa imezidi, imepanda bei.

Mheshimiwa Spika, miaka ya 2000 mimi nilikuwa dereva, tulikuwa tunatoa rushwa kwenye mabasi shilingi 2,000, lakini toka mwaka jana mpandishe faini rushwa imepanda sasa hivi kwenye mabasi wanatoa shilingi 10,000 na kuendelea. Nitoe ushauri tu kwa mhusika, kama yupo ama hayupo lakini ananisikia; sioni kama anafanya kazi kumsaidia Rais kwenye upande wa rushwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini vilevile kwenye sekta ya afya hapa kuna tatizo kubwa sana kwenye upande wa afya. Mimi nazunguka sana kwenye mikoa hii ya Tanzania, kila ukipata tatizo ukaingia hospitali hizi dawa zinazosemwa tunazitoa bure hazionekani kiukweli. Naweza nikawa mlalamishi sana lakini ukweli uhalisia ndio huo.

Mheshimiwa Spika, nizungumze kwa ajili ya wananchi wangu wa Jimbo la Mbogwe ambao wengi wao ni kweli ni watu ambao hawajasoma na Wabunge wengi humu tumepigiwa kura na hao watu ambao hawajasoma. Hivyo sasa naishauri Serikali ione jinsi gani hawa wenzetu ambao wameishia darasa la saba, hawana CV, tunashirikiana nao vipi ili kuepusha migongano. Maana nikiangalia kwa hali ya kawaida kama vile wasomi wengi siyo waaminifu. Tukiangalia kwenye halmashauri zetu Serikali inapata hasara nyingi sana. Ukiangalia upande wa watu hao wa rushwa hawashughulikii ipasavyo, utakuta tu watu wanauawa kwa kuiba kuku, wizi wa ng’ombe, wameuliwa na watu wasiojulikana, sijaona Mkurugenzi hata mmoja amefungwa kwa ajili ya kuhujumu miradi ya Serikali. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, naongea haya maneno nikiwa na experience kubwa sana. Leo ni miezi mitatu sasa mimi nikiwa Mbunge na nimejaribu kufanya operesheni kwenye jimbo langu nikaona matatizo yanatokea jimboni. Hivyo sasa nitoe wito tu kwa wahusika; kuna Waziri wa TAMISEMI, hata jana nilimsema lakini na leo naomba tu nirudie ili nishereheshe ili aone kabisa kwamba ni jinsi gani Wabunge wengine tunapata hasira.

Mheshimiwa Spika, Rais anataka tusonge mbele lakini huku sisi tukijitahidi kusimamia kama wasimamizi wakuu wa halmashauri mapato yanayotumwa juu na mapato yale ya ndani hayaonekani yanaenda wapi. Nikiangalia Jimbo langu mimi la Mbogwe ni jimbo lililo na rasilimali nyingi sana, ukiangalia mauzo ya Geita, dhahabu inayotoka Mbogwe ni nyingi sana. Kuna mapato yanayoitwa ya service levy, halmashauri yangu inabaki kuwa maskini na mimi mpaka sasa hivi najiuliza na mwanasheria wangu wa halmashauri, nimemwambia aangalie kifungu, tufuatilie kabisa mapato yetu ili halmashauri yetu iweze kupiga hatua. (Makofi)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge huyo ni Mheshimiwa Nicodemas Henry Maganga, Mbunge wa Mbogwe, mtani wangu. Yeye anatakiwa akimaliza miaka mitano aandikiwe kitabu kwa sababu ni mtu ambaye ameanzia mbali sana kimaisha; ametuambia hapa aliwahi kuendesha mabasi ya abiria hadi Mbunge. Mnaona jinsi nchi hii ilivyo na rasilimali kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Maganga, endelea na mchango wako.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, nilindie muda wangu usinikate, nina vitu vingi vya kuchangia hapa. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukiangalia kwenye miundombinu, barabara mwanzoni zilikuwa zinashughulikiwa na Madiwani, mmekuja mkafanya mabadiliko mkazipeleka TARURA na mimi najitahidi sana kuwasiliana na watu wa TARURA naona jinsi gani hakuna kuwa supported wala kuambiwa kwamba kuna bajeti ya shilingi ngapi zilizopo kwenye akaunti.

Mheshimiwa Spika, mpaka sasa hivi ninavyoongea na wewe hapa ndani ya Bunge lako hili Tukufu barabara zangu zimekatika, Waziri Mkuu ni shahidi, waliwahi mpaka kunidharau sana mimi wakati wa kampeni maana barabara yangu moja ya Budoda ilikuwa haipitiki na mpaka sasa hivi haipitiki, kule kuna wananchi wengi sana na wanajifungua kila siku. Sasa ule mto wakitaka kuvuka waje Masumbwe wanasombwa na vifo vingi vimesababishwa na mto huu. Unaweza ukasema kwamba ni kitu cha kuchekesha lakini ni kweli na uhalisia wa vitu vilivyoko kule Mbogwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile kuna barabara zangu za kutoka Mponda, tumepakana na Mheshimiwa Iddi, Mbunge wa Msalala, barabara zile ni mbaya sana. Kila ukiwafuata TARURA ni watu ambao hawaeleweki kwamba tunazirekebisha au tunafanya nini. Mwishowe nimekuwa kero kwenda kwenye ofisi za TARURA mpaka na mimi naiona hii kazi ya Ubunge ni ngumu sana. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nilindie muda wangu, bado naendelea. Kwa maana hiyo naliomba Bunge Tukufu hizi barabara bora zirudi tu halmashauri ili hawa Madiwani na wao wawe wanawajibika na kutoa go ahead kwamba turekebishe hapa na hapo, kuliko kumleta mtu mwenye degree, engineer ambaye amesoma physically, hajaona practical na hataki kujifunza na wala hayuko tayari kuwasikiliza wananchi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Waziri Mkuu, alikuja akaniombea kura na nimeshinda kwa asilimia…

SPIKA: Katibu, muongezee dakika tatu. (Makofi/ Kicheko)

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Waziri Mkuu alikuja kuniombea kura na nimeshinda kwa asilimia mia moja. Japokuwa siku ile ukiwa kwenye mkutano wangu unaninadi baada ya kusoma yale maelezo nilipingana na wewe maana mimi huwa ninasali, huwa ninajitahidi sana kutembelea kwenye neno la Mungu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo nachotaka niliombe Bunge Tukufu, kwanza sisi Wabunge tuwe na hofu ya Mungu, unajua haya mamlaka tumeyapata kwa nguvu za Mungu. Wapo viongozi kabisa hata hii hotuba wanaipongeza tu na mimi nimekuwa mfuatiliaji mzuri sana wa Rais wetu, watu wale wa karibu yake, ukitaka kumjua mtu angalia kwenye mawasiliano, anajua yule Waziri wa Mawasiliano ni nini huwa wanakifanya ili kumjua mtu mnafiki na mkweli. Wapo watu wakisimama majukwaani ni wazuri, wanampongeza kwa asilimia mia moja, huyu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kafanya mambo makubwa, moja, mbili, tatu, hivi na hivi Dkt. John Pombe Magufuli ni mtu mzuri lakini ukimfuatilia yule mtu unamkuta yuko kwenye connection za wizi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, watu wale kama wananifahamu wakitaka labda wanipeleke mahakamani mimi ushahidi ninao. Hata kama nikipoteza mwingine, Waziri wa Mawasiliano ni rafiki yangu, tutachomoa kwenye simu zao tutaangalia huwa wanaongea nini pale wanapoachana na Rais. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, suala lingine naomba kwenye halmashauri zetu hizi tutengeneze sheria za kuwa-limit Madiwani. Kuna Madiwani ni wazee, ni baba zetu na sisi Wabunge tulioingia awamu hii ni wadogo, wao ni wazoefu wengine wana miaka 20 wamo kwenye game. Walishazoea kuiba, hawapo kwa ajili ya kuwasaidia wananchi.

Sasa sisi tulioisoma hii hotuba ya Mheshimiwa Rais, tunapokwenda na misimamo hii hii tunaonekana wabaya. Naliomba Bunge hili tukufu tutunge sheria ili tuweze kuwa- monitor wale Madiwani.

Mheshimiwa Spika, halafu kuna kauli moja wanaitumia, nilindie muda wangu, bado kama dakika nne. (Kicheko)

SPIKA: Waheshimiwa, namlinda Mheshimiwa, naomba tumpe nafasi. (Kicheko)

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, kuna msemo mmoja hata hapa Bungeni nimeusikia, ukitaka kufuatilia ile miradi iliyotekelezwa na Chama cha Mapinduzi 2015 mpaka 2020 ukitaka kufuatilia kwamba hili jengo limejengwa kwa bei gani wanakwambia wewe usifukue makaburi, subiria zile fedha zinazokuja ili uanze kufuatilia hapo. Mimi naliomba hili Bunge pamoja na wasaidizi wa Mheshimiwa Rais, najua kuna CAG pamoja na watu wengine na Mawaziri wahusika; tufukue makaburi term hii ili tuonekane tunamsaidia Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo mimi namshukuru sana baba yangu mzazi ambaye anaishi kijijini, japokuwa napenda sana aishi na mimi lakini kwa uwezo wa Mungu na mapenzi ya watu wa Mbogwe niko hapa. Nakuomba tu endelea kuniongezea muda hivyo ili niweze kulisaidia taifa langu, hasa watu ambao hawajasoma wakapata vyeti lakini wana akili timamu na wana experience na wana uchungu mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia, namuomba Mheshimiwa Rais apime hata halmashauri 50 tu akiweka hata Wagogo na Wazaramo, sisi Wasukuma akituweka watasema kwamba kwa kuwa ni wa kwetu, aweke tu ninyi watani zetu ambao ni wa darasa la saba waende wakawe Wakurugenzi kwenye halmashauri muone zitakavyopanda hizo halmashauri. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)