Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Nitumie nafasi hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuweka hai mpaka leo, lakini nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa hotuba zake zote. Ni hotuba ambazo zimeonesha mwelekeo, zimeonesha dira, lakini zinatuonesha dhamira ya msingi aliyonayo Mheshimiwa Rais katika uongozi wakena kulipeleka Taifa hili mahali sahihi, tunakila sababu ya kumpongezea nakumtia moyo.

Mheshimiwa Spika, ukisoma hotuba ya Mheshimiwa Rais, kwanza hotuba ya 2015,halafu ukija kusoma hotuba ya mwaka 2020 inaonesha namna gani mambo mengi makubwa yamefanyika kwenye Taifa hili chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais katika Awamu hii ya Tano. Ukiangalia kwa mfano katika jitihada ambazo Mheshimiwa Rais amezifanya na kusimamia, mapambano dhidi ya rushwa na ndiyo maana utaona kwa mujibu wa Transparency International, katika nchi 35 za Afrika Tanzania imekuwa ya kwanza, lakini hata katika dunia vile vile utaona imekuwa nchi ya 28 katika nchi 136 katika matumizi bora ya rasilimali. Ni jambo jema nakwahiyo tunakila sababu ya kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa sababu mambo mengi yamefanyika kwenye miaka hii mitano.

Mheshimiwa Spika, ukisoma hotuba ya Mheshimiwa Rais inaonesha dira na kimsingi uelekeo ni mzuri, ndiyo maana ukiona kwa mfano uchumi wetu umekuwa mpaka kufikia kukua kwa asilimia saba ni jambo jema, pato ghafilimeongezeka kutoka trilioni 94 point kuelekea 139 ni jambo jema lakini mfumuko wa bei umeshuka, ni jambo jema vile vile katika maendeleo ya kiuchumi. Pia utaona hata mauzo ya nje vile vile yameongezeka kutoka dola bilioni 8.9 mpaka bilioni takribani 9.0,ni jambo jema. Kwa hiyo haishangazi hata mwezi Julai mwaka jana Tanzania ilivyotangwa kuingia sasa kwenye uchumi wa kati.

Mheshimiwa Spika, jukumu tulilonalo sasa ni kuona namna gani kukua kwa uchumi huu tunakuoanisha na maendeleo ya wananchi wa kawaida ili kukua huku kwa uchumi kuwaguse kwenye maisha ya kawaida ya wananchi wetu. Mwananchi aliyepo pale Ukerewe anayeshughulika na uvuvi aone namna gani katika shughuli zake za kujipatia kipato zinaendana na uhalisia wa kukua kwa uchumi. Kwa mawazo yangu, tunasekta za kijumla na ambazo ni muhimu sana ambazo zinagusa sehemu kubwa ya wananchi wetu ambazo Serikali kama itawekeza kwa kiasi kikubwa zitasaidia sana ku-link kukua huku kwa uchumi.

Mheshimiwa Spika, kwa bahati njema sana kwa mujibu wa hotuba ya Mheshimiwa Rais matarajio yake na ambayo ni matarajio yetu sote kwamba, sasa uchumi wetu uweze kukua kwa asilimia nane, ni jambo jema sana, lakini kama tutakuza sekta na kuzisimamia sekta kwa mfano sekta ya kilimo, uvuvi, mifugo, lakini hata nishati ni maeneo ambayo yanaweza kusaidia sana ku-link kukua huku kwa uchumi na maisha ya kawaida ya mwananchi kuwa bora ili mwananchi huyu wa kawaida aweze ku-feel kukua kule kwa uchumi.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, kwenye eneo la kilimo wamezungumza watu wengi hapa, kilimo kinaajiri sehemu kubwa sana wananchi wa Taifa zaidi ya asilimia 70 kwa mujibu wa takwimu, lakini uzalishaji huu wa kilimo bado unachangamoto nyingi, wamesema wachangajiaji waliotangulia kuna matatizo kwenye mbegu, kuna matatizo kwenye utaalam, lakini bado maeneo mengine ambapo uzalishaji umekuwa mkubwa kumekuwa na tatizo kupata masoko hasa masoko ya nje, bado tunachangamoto kubwa.

Mheshimiwa Spika, sasa niishauri Serikali, lakini kwanza niishukuru Serikali angalau kwa taarifa nilizonazo kwa yale makubaliano ambao Serikali ya Tanzania imeingia na Serikali ya Israel ili angalau kila mwaka vijana takribani 100 wawe wanaenda Israel kupata mafunzo ya kilimo, ni jambo jema sana.

Mheshimiwa Spika, sasa niishauri Serikali, iweze kuwalea vijana hawa,iweze kuwawezesha iliwanapokuwa wamemaliza mafunzo yale wakirudi nchini watusaidie kufikia kwenye malengo yetu ya kufanya mapinduzi ya kilimo kwenye Taifa hili; kwa sababu kama kila mwaka vijana 100 wakienda wakarudi wakawezeshwa, wakaweza kutusaidia kitaalam ni kweli tutafikia mapinduzi haya tunayotarajia kwenye eneo la kilimo.

Mheshimiwa Spika, niipongenze Wizara ya Mambo ya Nje inafanya kazi kubwa sana kutafuta wawekezaji, lakini vile vile katika kutafuta masoko kwa ajili ya bidhaa zetu tunazozalisha hapa nchini. Hata hivyo, bado naona kuna ombwe ambapo niishauri Serikali, iweze kuimarisha mahusiano kati ya Wizara ya Mambo ya Nje, Wizara ya Kilimo na Wizara ya Uwekezaji ili angalau wakulima wetu wanapolima mazao yao, basi yaweze kupata masoko ya uhakika nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika,eneo lingine kama nilivyosema ni eneo la uvuvi; kama ilivyokwenye kilimo, uvuvi unaajiri sehemu kubwa sana ya wananchi wa Taifa hili. Kwa mfano kwenye eneo letu la Kanda ya Ziwa, mimi natoka Ukerewe, katika kilometa za mraba 6,400 za Ukerewe, asilimia 90 ni maji, kwa hiyo utaona wananchi wengi wa Ukerewe wanashughulika na uvuvi na hivyo uvuvi unaajiri vijana wengi Ukerewe, Kanda ya Ziwa lakini hata maeneo mengine. Hata hivyo, kama Serikali itawekeza katika uvuvi huu inaweza ikasaidia sana kuboresha uchumi wa mtu mmoja mmoja. Bahati mbaya sana bado hatujaweza kufanya vizuri kwenye eneo hili la uvuvi.

Mheshimiwa Spika, alisema mchangiaji mmoja asubuhi hapa miaka miwili iliyopita kulikuwa na operesheni zile za kuzuia uvuvi haramu haisaidii sana, wavuvi wetu wadogowadogo hawa ambao tunahangaika kuwatafutia mikopo ili wajiimarishe kiuchumi hata kama kafanya kosa unakwenda unavunja mtumbwi wake, unachoma nyavu zake, haimsaidii sana. Nishauri Serikali iwekeze zaidi kwenye kutoa elimu. Bahati nzuri wananchi wetu ni wasikivu sana; kama wanashirikishwa, wanapata elimu, ni walinzi wazuri sana wa rasilimali zetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niiombe Serikali, kwenye eneo hili la uvuvi kwa mfano, ili tuweze kuufanya kwa tija na uweze kuwasaidia wananchi wetu kuweza kuimarisha uchumi wao kwa mwananchi mmoja mmoja na katika uchumi jumuishi, basi Serikali iwekeze kwenye kutoa elimu. Vilevile kama ambavyo tumekwishaanza tayari kwa ajili ya kuwasaidia kuwawezesha ili kuimarisha mitaji yao, jambo ambalo naamini litasaidia sana sehemu kubwa ya jamii yetu kuweza kuimarika kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ingawa kumekuwa na changamoto vilevile kwenye sekta hii ya uvuvi; wavuvi wetu wanakabiliana na changamoto nyingi sana lakini ninahisi kunakosa kiunganishi kati ya wavuvi na Serikali; chombo ambacho kinaweza kikawatetea, kikawasemea na wakati mwingine kikashauri Serikali namna gani ya ku-deal na masuala ya uvuvi ili sekta hii ya uvuvi iweze kuwa na manufaa kwenye taifa letu. Kwa hiyo, nishauri Serikali iweze kuliangalia jambo hili.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo linaweza kusaidia sana kufanya uchumi wa mwananchi mmoja mmoja uweze kuimarika ni kwenye eneo la nishati. Nishukuru sana, kwa mujibu wa hotuba ya Mheshimiwa Rais, mwaka 2015 wakati anahutubia Bunge, katika vijiji 12,000 ni vijiji karibu 2,000 tu ndiyo vilivyokuwa na umemeā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ni kengele ya pili Mheshimiwa Michael Mkundi, Mbunge wa Ukerewe.

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru, naunga mkono hoja. (Makofi)