Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Tabasamu Hamisi Hussein Mwagao

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sengerema

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. HAMIS H. T. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Sengerema, naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Spika, hotuba hii ya Mheshimiwa Rais ni miongoni mwa hotuba tamu sana katika nchi hii. Hizi hotuba za kishujaa hazitakiwi kuachwa bila kujadiliwa wala kusifiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais ameonesha ushujaa mkubwa sana ndani ya miaka mitano. Nimeangalia hotuba ya miaka mitano, nikaangalia na hotuba hii aliyoitoa juzi anafungua Bunge la Kumi na Mbili, mimi binafsi naunga mkono hoja kwa asilimia 100. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie kuhusiana na suala la mifugo. Katika mifugo Mheshimiwa Rais amesema kwamba wafugaji katika nchi hii sasa wana nafasi kubwa ya kupewa maeneo ya kupata vitalu, lakini waandaliwe sera nzuri kwa ajili ya kuacha kwenda kuchunga mifugo kwa aina ya zamani sana. Leo wafugaji wanatembea kuchunga wakati tunayo ardhi kubwa ya kutosha tungeweza kuzalisha nyasi, tunayo mabua ya mahindi yanapatikana kila mkoa, kwa nini wasitengeneze sera nzuri kwa ajili ya mifugo yetu?

Mheshimiwa Spika, leo wafugaji wanahamishwa kama hawapo kwenye nchi yao. Kila siku kesi zinakuwa nyingi, ukiangalia taarifa ya habari ni migogoro mikubwa ya wafugaji. Katika hili kama utaandaliwa mfumo mzuri sisi pamoja na kuwa nchi ya pili kwa ufugaji katika Afrika, tutakuwa nchi ya kwanza.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili kwenye hili suala la nyama, wananchi wa Tanzania hawajahamasishwa kula nyama. Mwananchi mmoja anatakiwa kwa kiwango cha chini ale kilo, ana hali mbaya nusu kilo, lakini akila hata robo kilo tu soko la nyama peke yake halitoshi katika nchi hii. Sisi wenyewe tunakuwa ni soko kubwa sana la nyama, kwanza tuanze kula sisi nyama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la maeneo haya ya malisho. Ni kwamba wakikata vitalu na hawa wafugaji wakapewa maeneo ya kwenda kuchunga kwanza ni walipaji wazuri kwa wakati. Leo katika nchi hii mifugo imeenea nchi nzima na miongoni mwa wafugaji ambao wanapata tabu, lazima tuwe wakweli, ni Wasukuma na Wamasai. Tumekuwa tunakwenda kila kona unahamishwa unaondoka, sasa hii imekuwa ni hatari. Kwenye hotuba hii tunakwenda katika uchumi wa kati, nafikiri Waziri wa Mifugo na Waziri wa Sheria waliangalie jambo hili tuwe huru katika nchi yetu katika suala la mifugo.

Mheshimiwa Spika, sasa niende upande wa kilimo cha pamba. Nchi hii pamba inalimwa katika mikoa 11. Katika Ilani yetu ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi na Mheshimiwa Rais ametembea nayo katika kampeni, anasema tunahitaji kuzalisha tani milioni moja, tuna uhakika wa kuzalisha zaidi ya tani milioni tatu lakini ni kama pamba itaokolewa na Serikali kwa dhamira ya kweli.

Mheshimiwa Spika, Kwa mfano, kama tumeweza kuokoa Shirika letu la Ndege leo liko hai kwa nini tusiokoe pamba yetu ya Tanzania kwa mambo matatu tu? Jambo la kwanza ni kwamba pamba hii ya nchi yetu itumike kwenye kuzalisha nyuzi na kutengeneza nguo katika nchi hii. Serikali inunue viwanda vya nyuzi na nguo halafu uone kama kilo moja ya pamba haitauzwa Sh.2,000 mpaka Sh.5,000 kwa kilo. Hii nguo niliyovaa mimi leo inauzwa Sh.170,000 au Sh.150,000 ukipata kwa gharama nafuu wakati haina robo kilo ya pamba. Sasa tunaonekana watu wa ajabu, ni lazima tumsaidie Mheshimiwa Rais na tuweke dhamira ya kweli, hilo ni la kwanza.

Mheshimiwa Spika, la pili, ni kupiga marufuku kuuza pamba kwa robota, kwa sababu uuzaji huu wa pamba wa robota unaifanya nchi hii inakuwa mtumwa, wanatuchezea katika maeneo makuu. Wanatuchezea katika mbegu, tunazo nchi zinazolima pamba katika Afrika; Burkina Faso ukiangalia Mali, Sudan, Misri, Zimbabwe na ukiwaona wenzetu Waganda leo wanakwenda kuchukua pamba ya Msumbiji wanasema ni miongoni mwa pamba bora katika Bara la Afrika hii yote ni kutuchezea akili, lakini kama tutakuwa tuna viwanda vyetu hatuwezi kuulizwa hilo jambo kwasababu pamba ni kilimo cha mabepari.

Mheshimiwa Spika, mbegu katika nchi hii hivi viwanda vya pamba vilivyopo huwezi ukailinda mbegu, unaweza ukatoa maelekezo kwamba mbegu ya kupandwa katika nchi hii inalimwa Igunga…

(Hapa kengele ya kwanza ililia)

MHE. HAMIS H. T. MWAGAO: Hii kengele na yenyewe tena, basi bwana.

SPIKA: Ya kwanza hiyo.

MHE. HAMIS H. T. MWAGAO: Sawa. Hapa nipo mahali patamu sana basi tu.

Mheshimiwa Spika,suala la mbegu haliwezi kulindwa na wafanyabiashara, suala la mbegu litalindwa na Serikali, lakini suala la pembejeo, mbegu na dawa na pamba ina muda ina timeframe, mwisho wa kupanda mbegu ni tarehe 15 mwezi 12, lakini mbegu inafika Januari, hizi dawa baada ya kupulizia, roho inaniuma muda unakuwa ni mdogo, sijui nifanyeje kuhusiana na suala la pamba. Serikali imerudisha viwanda vyetu vya Nyanza, SHIRECU, halafu tunashindwa kuiokoa pamba, zaidi ya wananchi milioni 16 ndiyo roho yetu.Mheshimiwa Rais tutamsaidiaje katika hili maana yake roho inatuuma, tuokoleeni pamba.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.