Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. SELEMANI M. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kunipa nafasi kuwa miongoni mwa wachangiaji wa hotuba ya Mheshimiwa Rais. Awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo amefanya ndani ya nchi hii. Katika hotuba aliyoitoa yapo mambo ya msingi ambayo aliyasisitiza ambayo na sisi tunahitaji yafanyiwe kazi hasa kwenye maeneo ya watendaji.

Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya vitu vingi na vikubwa katika nchi hii, lakini bado kuna eneo moja la kilimo halijawekewa msukumo mkubwa sana. Hili ni eneo ambalo linawashika Watanzania walio wengi na karibu asilimia kubwa ya ajira za wananchi ziko kwenye eneo hili.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hotuba ya Mheshimiwa Rais, ameelezea zaidi kujikita kwenye kilimo cha umwagiliaji. Miradi mingi ya umwagiliaji haijatendewa haki katika nchi hii na ili tuweze kuwa na uzalishaji mkubwa lazima tuwekeze uwekezaji mkubwa kwenye eneo hili. Nchi hii ina mabonde mengi ambayo hayafanyiwi kazi. Tunaweza tukawa wazalishaji wakubwa na tuchukulie mfano tu Mkoa huu wa Dodoma. Mkoa wa Dodoma ndiyo mkoa ambao una ardhi nzuri yenye rutuba sana, kwa bahati mbaya sana mkoa huu mvua zake ni za shida. Sasa kama tungekuwa tumewekeza kwenye eneo la umwagiliaji karibu kila sehemu ya mkoa wa nchi hii ungekuwa na uzalishaji mkubwa sana. Tunaishauri Serikali…

SPIKA: Mheshimiwa Kakoso, watu wengi hawafahamu hilo kwamba Mkoa wa Dodoma of course that means and Singida and a little bit of Shinyanga ni mkoa wenye ardhi yenye rutuba sana, ni mvua tu! Mvua ikinyesha ukiona hayo mahindi yalivyokaa vizuri utafikiri yamewekewa mbolea ya aina gani.Endelea tu Mheshimiwa Kakoso.

MHE. SELEMANI M. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunaishauri Serikali iwekeze fedha nyingi za kutosha kwenye eneo la Sekta ya Umwagiliaji.

Mheshimiwa Spika, la pili, hata kama wananchi wengi watawekeza kwenye kilimo na kikawa kinalipa, kama hakuna masoko ya msingi, Serikali haijajikita kutafuta masoko ni kazi bure. Mkulima anapozalisha hawezi kusukumwa, kinachomsukuma ni soko, ndiyo maana mnaona mwaka huu watajikita kwenye kilimo cha mpunga, baadaye watahama wataenda kwenye kilimo cha mahindi, ni kubahatisha kutafuta soko.

Tunaiomba Serikali iwekeze kwenye kitengo cha masoko ilikile kinachozalishwa na wakulima kiweze kuwa na uhakika wa kupata masoko yaliyo mazuri.

Mheshimiwa Spika, tunayo mazao makubwa nchini yanayoingiza fedha nyingi za kigeni. Kwa bahati mbaya sana bado Serikali haijawekeza sana. Tukitaka uzalishaji wa tumbaku, mkonge, pamba ni lazima tuwe na uwekezaji mkubwa na ifike mahali Serikali iwekeze na kuweka ruzuku ya kutosha kwenye mazao haya. Naamini tukifanya hivi, Serikali itakuwa inanufaika kwa kiwango kikubwa, mzunguko wa fedha utakuwa mkubwa na wananchi watanufaika sana, ukata hautakuwepo kwa sababu ni eneo ambalo limeshika walio wengi.

Mheshimiwa Spika, nichangie kwenye eneo la miundombinu. Serikali imewekeza fedha nyingi sana kwenye eneo la miundombinu, lakini ushauri wangu naomba nijikite sana kwenye eneo la TARURA.

Mheshimiwa Spika, tulianzisha TARURA lakini haina bajeti. TARURA inategemea fedha za Mfuko wa Barabara ambazo zinakusanywa asilimia 100. Kati ya asilimia 100, asilimia 30 ndizo zinazoenda kwenye eneo la TARURA na asilimia 70 zinaenda kwenye Mfuko wa Barabara kwa ajili ya matengenezo ya TANROADS. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaweza tukawa kituko pale ambapo tulianzisha kitu ambacho hakiwi supported. Tunaomba Serikali kuu itenge fedha za kutosha, nchi yetu imekuwa kubwa, tuna maendeleo ya kila aina, kila sehemu panahitaji miundombinu ya barabara. Hata hayo mazao tunayozalisha yanategemea barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatuna bajeti ya TARURA. Kama nilivyozungumza hapa naelewa mfuko ule unaotumika kwenye bajeti ya TARURA ni Mfuko wa Barabara tu ambao chanzo chake tumekiweka kwenye eneo la mafuta. Sasa niombe Serikali ifanye kama inavyofanya kwenye eneo la barabara kuu zinazohudumiwa na TANROADS ifikie mahali itenge fedha za kutosha ili ziweze kuhudumia barabara. Maeneo haya ni muhimu sana kwa hiyo Serikali iangalie ili tuweze kupata kile ambacho Mheshimiwa Rais anakitarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni mindombinu ya umeme. Serikali imejikita kupeleka umeme vijijini. Tuna mategemeo makubwa na Serikali kwamba itapeleka miundombinu hiyo.

Naomba Serikali ihakikishe kama Mheshimiwa Rais alivyosema tuhakikishe maeneo yote vijijini yanapata umeme. Tukifanya hivyo tutakuwa tunakuza uchumi kwa kiwango kikubwa ambacho kitawasaidia wananchi. Maeneo mengi bado kwenye vijiji hawajapata umeme ambapo malengo ni kusukuma na kuleta mapinduzi ya kiuchumi. Tunaomba eneo hili liangaliwe sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho, nichangie kwenye eneo la sekta ya afya. Hapa bado tuko nyuma sana kwenye bima ya afya. Niiombe sana Serikali katika kipindi hiki cha miaka mitano tuhakikishe Watanzania wote wanapata bima ili waweze kunufaika na Serikali ambayo imefanya mambo makubwa sana.

Mheshimiwa Spika, tunaishukuru sana Serikali, tunampongeza Mheshimiwa Rais, nami naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)