Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, awali ya yote na mimi napenda kuungana na wazungumzaji wa mwanzo pamoja na Mheshimiwa Waziri Mkuu na ninyi nyote kuendelea kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoifanya. Siyo yeye peke yake isipokuwa na wasaidizi wake ambao wameanza kwa spidi kubwa sana. Hongereni sana Mawaziri wangu, hongereni sana viongozi wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimefurahi kupata nafasi ya kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais. Kwangu mimi nikiisoma hotuba ile nzima, ndani yake naweza kusema ni semina elekezi au ni maelekezo yanayotosha kabisa kwa Mawaziri wangu hawa kuanza kufanya kazi kwa spidi kubwa kama ambavyo wameanza. Kwa sababu ndani yake kwa mfano kwenye kila eneo Mheshimiwa Rais amejitahidi kuchambua na kueleza juu ya tamaa yake ya kuona nchi inakwendaje, lakini pili jinsi gani tamaa ile inaweza ikafikiwa ili malengo yale ya kuwasaidia Watanzania walio wanyonge yaweze kufikiwa.

Mheshimiwa Spika, naomba kuongea kidogo katika baadhi ya maeneo ambayo naamini kabisa tunao mchango au kutoa wito kwa Mawaziri wetu ili waweze kufanya kazi nzuri kuweza kumsaidia Mheshimiwa Rais. Kwa mfano, naamini katika eneo la Chalinze na Tanzania ambayo sasa wimbo wetu mkubwa ni maendeleo ya viwanda, viwanda haviwezi kufanikiwa bila kuwepo kwa umeme wa uhakika. Kazi nzuri inafanywa ya kuhakikisha kwamba umeme wetu katika bwawa la Mwalimu Nyerere unakamilika na mimi binafsi yangu nitumie nafasi hii kuipongeza sana Wizara hasa kwa jinsi ambavyo wanaendelea kusimamia ujenzi wa bwawa lile lakini pia kwa ma-engineer wetu ambao hata juzi tulishuhudia wenyewe wakieleza katika vyombo vya habari kwamba hawana shida yoyote na kwamba malipo yanapatikana ndani ya muda. Kwangu mimi hii ni ishara nzuri lakini ni wito wangu kwa Wizara kuhakikisha kwamba wanasimamia ili ule muda ulioelekezwa wa mradi kukamilika uweze kukamilika mapema iwezekanavyo.

Mheshimiwa Spika, kwangu mimi ujenzi wa bwawa hili siyo tu kwamba unaenda kutatua kero nyingi za kimaendeleo za watu, lakini msingi mkubwa ni kwenda kuhakikisha kwamba umeme wa uhakika unapatikana ili ile sera yetu ya viwanda katika Tanzania iweze kufanikiwa. Kwa hiyo, wito wangu narudia tena kwa Waziri husika ajaribu kusimamia vizuri jambo hili ili wale wananchi wetu ambao sasa hivi wameanza kulalamika kupata matatizo ya kukatika umeme mara kwa mara, jambo hilo nalo liweze kuisha.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hilo katika hotuba yake Mheshimiwa Rais alieleza kwa uzuri zaidi jinsi ambavyo anatamani kuona maendeleo ya utalii yanapatikana Tanzania hii. Unakumbuka katika moja ya maeneo ambayo Mheshimiwa Rais aliyagusia ni kutatua migogoro iliyopo baina ya vijiji na hifadhi zetu kwa maana ya kusaidia kuongeza idadi ya watalii kwenye maeneo yetu. Moja ya maeneo hayo ni eneo la Mbiki au Wami Mbiki lakini pia Hifadhi yetu ya Saadani.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Kata ya Mkange kule Chalinze wanalalamika sana juu ya migogoro ambayo inayoendelea lakini ahadi ya Mheshimiwa Rais alipokuja kwenye kampeni alieleza kwamba anatamani sana kuona migogoro hii inakwisha na katika kuhakikisha kwamba migogoro inakwisha, moja ya jambo kubwa ambalo alielekeza ni urasimishwaji wa maeneo ya vijiji hivyo ili sasa wananchi waondoke katika maeneo ya migogoro. Kwa hiyo, wito wangu kwa Mheshimiwa Waziri husika, jambo hili aendelee kuliangalia vizuri kwa sababu sisi ambao tunaamini kwamba Rais wetu ana nia njema ya kusaidia wananchi wake tusije tukamuangusha kwa sisi kushindwa kufikia malengo hayo. Mimi kama Mbunge nikiwa na viongozi wenzangu ndani ya halmashauri yetu, tutakupa ushirikiano mkubwa sana Mheshimiwa Waziri ili kuhakikisha kwamba nia ya Rais inafikiwa katika kiwango kikubwa na ikiwezekana kiwango chenye mafanikio makubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hilo, nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa nia yake nzuri ya kutengeneza reli ya kisasa ya SGR ambayo inatoka Dar es Salaam inakwenda mpaka Kanda ya Magharibi lakini pili inafika mpaka nchi jirani. Kwangu mimi huu ni ukombozi mkubwa sana, kwanza kwa barabara zetu ambazo kwa kipindi kikubwa sana Mawaziri wamekuwa wanalalamika lakini pia wewe mwenyewe unaweza kuwa shuhuda unapotoka kipande cha Chalinze kwenda Mlandizi kimeharibika sana kwa sababu ya uzito mkubwa wa magari yanayopita pale.

Mheshimiwa Spika, mimi naamini kwa kufanikiwa kukamilisha SGR hii maana yake mizigo mizito yote itaingia kwenye treni na itakwenda katika maeneo husika na hasa yale maeneo ambayo tumetengeza miradi ya kimkakati hasa ule mradi wa dry port wa pale Kwala na mwingine ule wa Kahama, maana yake ni kwamba tunakwenda kutatua tatizo kubwa ambalo linaendelea kukabili Watanzania wetu. Hivyo basi zile pesa ambazo zinatumika wakati mwingine kutengeneza barabara ambazo zinaharibika ndani ya muda ambapo hazipaswi kuharibika, kwa kweli nalo tutaliondoa tatizo hilo. Kwa hiyo, kwangu mimi ni kumpongeza pia Mheshimiwa Rais na kumuahidi kwamba tuko naye bega kwa bega kuhakikisha kwamba mradi huu unakamilika mapema iwezekanavyo na Watanzania waendelee kupata mafanikio ambayo yeye ameyakusudia.

Mheshimiwa Spika, pia Mheshimiwa Rais alieleza juu ya nia yake nzuri ya kuona jinsi gani tunaweza tukachukua hii idadi kubwa ya mifugo tuliyonayo ambayo inatupa nafasi ya pili kwa idadi ya mifugo Tanzania kuwa ni sehemu ya uchumi kuwawezesha wananchi wetu. Katika eneo letu sisi la Chalinze lakini pia katika maeneo ya Pwani ya Tanzania, wanyama kwa maana ya mifugo, mbuzi na kondoo ni wengi sana.

Mheshimiwa Spika, naamini nia hii ya dhati ya Mheshimiwa Rais ambayo ameeleza kwenye hotuba yake ambapo analenga kuhakikisha miaka mitano itakapomilika zaidi ya machinjio tisa za kisasa zitakuwa zimejengwa, kwa kweli naamini machinjio haya yatakapokamilika tutakuwa tumesaidia sana kuondoa migogoro ya wakulima na wafugaji inayoendelea. Naamini wafugaji wetu wanahitaji kupewa elimu na siyo kugeuzwa maadui katika maeneo yao ili waonekane kwamba ni wakosefu. Pamoja na hilo ni muhimu pia kwa Wizara kuhakikisha kwamba wanawapelekea wafugaji hawa huduma muhimu zinazotakiwa katika maeneo yale. Kwa mfano, ujenzi wa mabwawa makubwa ili waache kusafiri na mifugo kwa umbali mrefu kwenda kutafuta huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, mwisho, lakini siyo kwa umuhimu, naomba kugusia kwenye eneo la elimu. Asubuhi hapa umeibuka mjadala mkubwa sana juu ya Bodi ya Mikopo na mikopo inayotolewa kwa vijana wetu. Nikupongeze wewe pia kwa kuliona jambo hili lakini kwa kweli sisi kama Wabunge sijui kama wenzangu wanaliona hili lakini vijana wetu wengi wanakosa fursa ya kusoma vizuri kwa sababu ya kukosa mikopo ya Bodi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, shida kubwa ambayo mimi naiona binafsi ni kwamba katika maeneo mengi sana, vijana hawa wanapokuwa katika level za chini, sisi Wabunge au kupitia wahisani mbalimbali tumekuwa tunawasaidia kuwasomesha katika shule zilizo nzuri. Kwa mfano, wako vijana ambao wamesoma katika shule hizi ambazo tunasema ni private schools katika level ya form one mpaka form four lakini vijana wale baada ya kufika chuo kikuu either wazazi wale wamekosa uwezo au wale sponsor wamefariki au wale wanaowawezesha nao hawana uwezo huo, kwa hiyo, wale vijana wanajikuta kwamba wananyimwa mikopo kwa sababu ya kukosa vigezo. Wito wangu kwa Wizara iangalie historia ya mwanafunzi huyu. Kigezo kisiwe amesoma wapi, kigezo kisiwe kwamba amewezeshwa na nani, waangalie kama uwezo huo anao ili kuweza kufikia malengo mazuri aliyoyaainisha Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa nitumie nafasi hii kumpongeza sana ndugu yangu Bwana Aweso, Waziri wa Maji kwa kazi nzuri sana anayoifanya. Wana wa Chalinze wanakushukuru na wanaendelea kushukuru katika kazi kubwa unayoendelea kuifanya. Wito wao mmoja tu ni kwamba zile pampu zinazojengwa pale Msoga na Chamakweza hebu hakikisheni kwamba zinakamilika mapema iwezekanavyo ili lile tatizo la maji linalowakabili wananchi wale liweze kuisha na liwe hadithi ambayo imepita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, naunga mkono hotuba zote za Mheshimiwa Rais, napenda kusema kwamba tuko pamoja naye na ajue kabisa kwamba anao vijana ambao wanamtakia mema. Ahsante sana. (Makofi)