Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya mwanzi kabisa Mungu akubariki na naomba upeleke salamu zangu na shukurani kwa Mheshimiwa Spika kwa kusimamia Bunge letu vizuri na kwa fursa sawa kwetu wote. Ningependa vilevile kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa miaka hii na hii ni Bunge la mwisho kushirikiana kwa pamoja na kila mmoja akafika wakati huu Mungu atubariki wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda vilevile kuchukua fursa hii kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais mwenye Wizara hii. Mheshimiwa Rais amesimamia Wizara hii na akisaidiwa na Waziri wetu na kwa kweli wengine wamesema na mimi nitakuwa nimekosa fadhila kama sitatambua miradi ile ya mkakati ambayo ametuwekea kwa manufaa ya nchi yetu na mikakati hiyo ndio itasaidia maendeleo ya wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kutaja miradi hiyo kama standard Gauge ya railway ambayo itasaidia sana kubeba mizigo na kuongeza uchumi wetu, ufufuaji wa Shirika la Ndege ambayo itachochea sana maendeleo ya Utalii na usafiri wetu sisi wenyewe vilevile. Ya tatu ni ujenzi wa Bwawa la umeme la Mwalimu Julius Nyerere na ninyi mnajua kuwa na umeme wa uhakika maana yake ni kuwa na maendeleo ya hakika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile afya ameichochea sana mpaka leo zahanati 1,198 jamani sio kazi ndogo katika miaka hii minne na miezi, vituo vya afya 487, hospitali 69, hospitali za rufaa 10 na Waziri leo ameelezea vituo vingapi, zahanati ngapi zitaongezeka ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais nina hakika hayo yote yanafanywa kwa ajili yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, umeme vijijini na kuanzisha uwakala jamani kuwa na umeme vijijini maana yake na Miji ni kuletewa maendeleo vilevile, hili ni jambo kubwa kutoka vijiji 2118 leo 9000 na zaidi wana umeme jamani hili si jambo dogo na yote haya ni miradi ya mikakati ambayo ameanzisha Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kubwa zaidi ndugu zangu ni wakala wa maji, wakala wa umeme na wakala wa barabara vijijini, wakala hizi zitasaidia sana barabara, maji ambayo ni jambo muhimu sana zitasaidia sana vilevile na umeme na kuleta maendeleo ya uhakika na ya haraka. Pamoja na hayo bila Mheshimiwa Jafo na Manaibu Waziri pamoja na Mtendaji Mkuu wa Wizara hiyo na watalaam wote nina hakika mengi yasingefanyika kwa hiyo nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Jafo na kila wakati tukiwa na jambo Mheshimiwa Waziri Jafo ukimuendea hajawahi kurudi nyuma ahsante sana wakisaidia na Manaibu Waziri pamoja na wataalam wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba niseme kwamba jamani ningependa kusema machache ambayo yatasaidia sana vijiji vyetu na wilaya yangu. Kwanza ni sera ya barabara vijijini. Sera inasema kukarabati barabara ijijini haiongei kufungua barabara, ninaomba hii sera tuiangalie ili tuwe na kufungua na kukarabati barabara ambazo zipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa sababu tuna wakala wa TARURA ingawa wanapata fedha kidogo lakini tusibakie tu kukarabati kuna Wilaya ambazo hazina barabara nyingi, kuna Wilaya ambazo zina barabara nyingi lakini tukifungua tutawapa kipaumbele wale ambao hawana barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningeomba mimi kwa wakala wa barabara, barabara ya kutoka Gisambarang kupitia Masusu, Milongori, Biroda mpaka Lalaji jamani ni mpakani halafu kuna msitu na kuna watu wengi sana, vilevile barabara nyingine ya kufungua ingekuwa barabara kutoka Mascaroda kwenda Ng’arda, Lambo na kwenda Dareda ambako kuna hospitali kubwa pamoja na kwamba iko Babati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile ningependa kujiekeleza kwenye elimu ni muhimu sana na sasa elimu ya sayansi ndio muhimu nimefurahi, ninashukuru na ninampongeza Waziri kusema kwamba kila Wilaya zitajengwa barabara kwenye shule za sekondari, maabara zimeshajengwa zimefika mbali ninaomba sana tukamilishe ili watoto wetu wasome sayansi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kuongea juu ya Watendaji wa vijiji na Kata. Kule kuna kata na vijiji ambavyo havina watendaji. Maana yake ni kwamba maendeleo na hata huduma za wananchi zinaomba muangalie umuhimu wa kuazisha ya kupeleka na kuajiri watendaji ili vijiji vyetu na kata zetu ziweze kuongozwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile ningependa kuongea kuongea habari ya TASAF ninajua itakuwa kwingine lakini ndio iko vijijini. Ninaishukuru Serikali namshukuru sana Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Jafo na wengine wote kwamba sasa TASAF inaenda kwenye vijiji vyote TASAF ilikuwa inaenda kwenye vijiji vichache ikienda kwenye vijiji vyote wale masikini watapata namna ya kuweza kutoka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ninapenda niseme kwamba kuhusu vituo vya afya niliomba kituo kwa ajili ya Basotu na Endasack lakini mmenipa vituo vya pembezoni ya Hilbadau au pamoja na Simbay sasa mmeniletea fedha kwa ajili ya Mogitu. Ninaomba usisahau kata hizo pamoja na kata zingine nakushukuru umesema kila kata, kila wilaya itapata vituo vitatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na vilevile nisipoongea juu ya mkopo ule wa asilimia 10 nitakuwa sijatenda haki. Jamani mikopo hii inainua wanawake, vijana na walemavu. Naishukuru na wilaya yangu kwamba wanatoa ingawa kuna deni ambalo huko nyuma hawakutoa ninaomba kupitia msukumo wako madeni yale yaliyobaki wapewa wananchi lakini vilevile wanawake waendelee sasa hivi naona msukumo umeongezeka tutaondoa umasikini wakisadiana na TASAF nina hakika tutakwenda mbali sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Wizara hii ni Wizara muhimu sana ni cross cutting ni ya TAMISEMI ina maji na maji ni kitu muhimu sana. Wilaya kama ya Hanang iko kwenye lift valley hamna maji ninaomba jamani mshirikiane na Wizara ya Maji najua Wizara sasa hivi huu ni wakala hauko chini ya TAMISEMI lakini tuweze kuomba vijiji na kata zipate maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana naomba niongee juu ya Corona, ni ugonjwa mbaya kuliko magonjwa mengine yote…(Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa kengele ya pili imeshagonga.

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)