Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja ya hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, kwanza napenda nianze kwa kusema naunga mkono hoja kwa sababu hotuba hii imeeleza kwa ufasaha mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Tano na imeainisha kazi ambayo inakwenda kufanyika katika mwaka 2020/2021. Nampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa ambayo amekuwa akiifanya katika Serikali hii.

Pia napenda kuwapongeza Mawaziri katika Ofisi yake, Dada yangu Mheshimiwa Jenista Mhagama na Mheshimiwa Angellah Kairuki, hakika wanaonyesha mfano namna ambavyo wanawake wanafanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia napenda kutumia nafasi hii kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamechangia katika Sekta ya Elimu na niseme kwamba michango yote tumeipokea. Kwa sababu ya muda na kwa kuzingatia kwamba ndiyo mara yangu ya kwanza kuongea Bungeni tangu Benki ya Dunia ilipopitisha mkopo wa shilingi milioni 500, nitumie nafasi hii kutoa shukurani za dhati kwa Benki ya Dunia kwa kuidhinisha mkopo huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unafahamu namna ambavyo mkopo huu ulileta sintofahamu na hata kuna kipindi ambapo katika Bunge lako kulikuwa na mjadala kuhusu suala hili. Tunashukuru kwamba baada ya majadiliano wameweza kuzipitisha. Niseme kwamba fedha hizi zinakwenda kuimarisha elimu ya sekondari, zinakwenda kuondoa vikwazo na hasa kwa watoto wa kike kuhakikisha kwamba wanapata elimu iliyo bora. Mradi huu utakwenda kunufaisha watoto wasiopungua 6,500,000 na utatoa kwa elimu kwa watoto wote wa kike na wa kiume bila ubaguzi wowote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi huu utasimamiwa na Wizara ya Elimu ambayo ndiyo ina dhamana ya kusimamia elimu hapa nchini na tutahakikisha kwamba tunasimamia mradi huu kwa kushirikiana na wadau wote muhimu.

Kwa hiyo, niwahakikishie Watanzania kwamba Serikali iliomba huu mkopo kwa sababu ina dhamira ya dhati ya kuboresha elimu. Kwa sababu sasa mkopo umeidhinishwa, Serikali inakwenda kuutekeleza kama ambavyo tumekubaliana na Benki ya Dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama unavyofahamu na wakati mwingine huwa unakemea hizi tabia; yapo mambo ambayo yameshaanza kuleta majadiliano kuhusiana na huu mkopo na ndiyo maana nimeona mimi mchango wangu niutumie katika kuleta ufafanuzi. Mradi huu unatekelezwa katika mfumo wa “Lipa Kulingana na Matokeo” kama ambavyo Wabunge wote mnafahamu mradi wa Lipa Kulingana na Matokeo tulionao. Tunao uzoefu, tunayo dhamira, tunao uwezo wa kuhakikisha kwamba tutatekeleza mradi huu kulingana na mipango ambayo tumeiweka ili tuweze kufikia malengo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwahakikishie Watanzania, nia yetu iko pale pale, uwezo wetu uko pale pale, tunakwenda kuimarisha elimu yetu na tutahakikisha kwamba tunawashirikisha wadau wote katika hatua zote ili kuhakikisha tunafanikiwa.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuzungumzia mradi huu ambao utakuwa na mazingira ambayo ni jumuishi na rafiki kwa watoto wetu wote, nizungumzie na mimi janga ambalo liko kwenye nchi yetu na dunia kwa ujumla, suala la virusi vya Corona.

Mheshimiwa Spika, tunafahamu shule zetu zimefungwa, wanafunzi wako nyumbani. Hivyo basi, imekuwa kwa kweli ni jambo ambalo kidogo linaathiri hali yetu ya elimu kama ambavyo linaathiri sekta nyingine. Kwa hiyo, nitumie nafasi hii kuendelea kusisitiza na katika mchango wa Wabunge, kuna suala ambalo lilijitokeza kwamba kuna baadhi ya wazazi ambao watoto wao wanaendelea kwenda tuition.

Mheshimiwa Spika, Serikali imekataza mikusanyiko isiyokuwa ya lazima na Serikali ilifunga shule kwa sababu ya kuwaweka watoto katika mazingira salama ili wasiwe na mikusanyiko. Kwa hiyo, natumia nafasi hii kusema kwamba tuition zote zinazofanyika sasa hivi ni batili. Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya wahakikishe kwamba wanasimamia maelekezo ya Serikali. Mtu yeyote anayeendesha tuition, ni batili, achukuliwe hatua inayotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara yangu kwa kutambua kwamba Wanafunzi wako nyumbani na wanahitaji kuendelea kuwa wanapata elimu hata wakiwa nyumbani, tunayo huduma ya maktaba ambayo inatolewa na Taasisi ya Elimu Tanzania ambayo kiutaratibu ili uweze kupata vitabu katika huduma hiyo ilikuwa unapaswa kulipa. Sasa kwa kutambua kwamba wanafunzi wamefunga shule, Serikali inatoa huduma ya upatikanaji wa vitabu vyote kuanzia Elimu ya Awali, vya Shule ya Msingi, Shule ya Sekondari kuanzia O- level na A-level bila malipo yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwasihi sana wanafunzi wote, huko waliko majumbani kwao watumie muda wao kusoma vitabu ambavyo Serikali inawapa access bila gharama yoyote badala ya kwenda kuzurura mitaani na kujiweka katika hatari ya kuweza kupata maambukizi ya virusi vya corona. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, narudia kukushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja hii.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)