Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze Rais wetu Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya. Pia nimpongeze Waziri Mkuu pamoja na timu yake kwa kuwasilisha hutuba yake nzuri iliyogusa kila mahitaji ya Watanzania.

Mheshima Spika, naomba nianze kuchangia suala zima la afya na niendelee kuipongeza Serikali yangu tukufu kwa kujenga vituo vya afya zaidi ya 350 na zaidi pamoja na Hospitali za Wilaya, pamoja na hayo kuna maeneo mengine wananchi wamejitolea kujenga vituo vya afya kwa nguvu zao pamoja na zahanati na wamefikia hatua nguvu zimewaishia, hivyo wanahitaji Serikali yao tukufu iwaunge mkono kama maeneo mengine walivyopewa fedha kwa ajili ya kujenga majengo ya kisasa.

Kwa hiyo, niiombe Serikali yangu iwapatie wananchi wa Jimbo la Lushoto fedha kwa ajili ya kumalizia vituo viwili vya afya ambavyo kimoja kipo Kata ya Gare na cha pili kipo Kata ya Ngwelo, kwani vituo hivi vikimalizika, vitapunguza usumbufu wanaoendelea kuupata kwa kutembea zaidi ya kilometa 50 mpaka 60 kufuata huduma za afya Wilayani.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo kuna zahanati nyingi zimejengwa kwa nguvu za wananchi na zimeisha lakini hazina vifaa tiba pamoja na watumishi, kwa hiyo niiombe Serikali yangu itenge fedha za kutosha katika bajeti hii ili zahanati zile ambazo zimejengwa kwa nguvu za wananchi zianze kutoa huduma kwa wananchi wetu pamoja na nyumba za watumishi.

Mheshimiwa Spika, nichangie suala la elimu, niipongeze Serikali kwa kujenga madarasa mengi ya sekondari na msingi, kwakweli madarasa yale yameleta tija na ufanisi mkubwa hasa kwa wananchi, kwa jitihada hizi naomba niishauri Serikali yangu tukufu kwa nini isitumie mfumo huu huu kumalizia maabara zilizojengwa kwa nguvu za wananchi, pamoja na kujenga hosteli katika mashule yetu ya sekondali ili wanafunzi wetu wa kike kuepuka kupata mimba za utotoni na zisizokuwa za lazima na watoto hawa kutimiza ndoto zao.

Kwa kuwa Jimbo la Lushoto lina shule za sekondari zaidi ya 30 na zenye hosteli ni sekondari tatu tu na hosteli hizo hazina ubora. Kwa hiyo niiombe Serikali yangu iweze kunipatia fedha ili tuweze kujenga hosteli angalau katika sekondari zifuatazo Malimbwi Sekondari, Mariam Mshangama Sekondari, Kwai Sekondari, Ubiri Sekondari, Claus Sekondari na Ngwelo Sekondari.

Mheshimiwa Spika, tutakapojenga hosteli katika shule hizi tutakuwa tumewaokoa watoto hasa wa kike katika janga hili la kupata mimba na pia ufaulu utaongezeka katika mashule yetu hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, kuhusu barabara zetu hasa za TARURA kwa kweli chombo hiki kinafanya vizuri ila kina changamoto ya rasilimali fedha na ukizingatia chombo hiki kina barabara nyingi za vijijini ambazo ndizo zinazotoa mazao kutoka kwa wakulima, hivyo basi niishauri Serikali yangu iongeze asilimia kumi ili jumla wapewe asilimia 40 angalau wataweza kukabiliana na changamoto hizi za barabara kuliko ilivyo kuwa sasa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la umeme, niendelee kuipongeza Serikali yangu tukufu kwa kusambaza zaidi ya vijiji 9000 mpaka sasa, kwa kweli ni kazi kubwa sana imefanyika, ushauri wangu niiombe Serikali yangu itenge bajeti ya kumalizia vijiji vilivyobaki ili kuondoa manung’uniko kwa wale ambao bado hawajapata umeme,hasa katika Jimbo la Lushoto lenye vijiji 62 lakini vilivyopata umeme ni vijiji 30 tu.

Kwa hiyo bado vijiji 32 na hii imeleta malalamiko ya kila siku na sisi Wabunge kuulizwa maswali ya kila siku na kukosa majibu yake, pamoja na haya Waziri wa Nishati alitoa waraka wa gharama za umeme zisizidi shilingi 27,000 lakini maagizo hayo hayafuatwi, wananchi bado wanalalamika, kwani wanapofika TANESCO wanaambiwa hakuna kitu kama hicho.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu naomba Waziri atoe tamko tena na ufuatiliaji ufanyike pamoja na kutoa onyo kali kwa Mameneja wa Wilaya.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono bajeti ya Waziri Mkuu kwa asilimia mia moja.