Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hoja iliyopo mezani. Kwanza na mimi nianze kutoa pongezi kwa kazi kubwa ambayo ni dhahiri ambayo imefanywa na Serikali ya Awamu ya Tano. Sisi sote ni mashahidi kwa kiasi gani miaka hii mitano imekuwa ni ya utekelezaji wa yale yote yaliyoainishwa katika Ilani ya Uchaguzi, Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa mwaka 2015/ 2020. Kwa sababu ni dhahiri hata sisi huwa tukizungumza na marafiki zetu wengine hususan hawa ambao wamekaa upande wetu wa kulia, tukiongea kiurafiki huwa wanakiri jitihada kubwa ambazo zimefanyika katika utekelezaji wa Ilani.

Mheshimiwa Spika, aidha, niendelee kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa anayoifanya katika kuhakikisha utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi, lakini kwa hotuba yake hii ambayo tunachangia leo. Nafahamu kwamba ana wasaidizi wake Waziri, Manaibu Waziri, Makatibu Wakuu na watumishi wote wa Serikali ambao wanafanya kazi hii kubwa, kwa hiyo nipongeze jitihada hizo.

Mheshimiwa Spika, napenda kuchangia katika masuala ya vijana na kabla ya kuchangia katika masuala ya vijana ningependa na mimi nigusie changomoto hii au janga hili la kidunia na hasa katika sekta ya afya, la ugonjwa wa SARS-Cov2 au tuseme COVID 19. Ugonjwa huu kama wote tunavyofahamu ni janga la dunia, janga la kiafya ya kidunia na sisi Tanzania ni nchi mojawapo ambayo imekutwa na ugongwa huu. Nafahamu kuna jitihada kubwa sana na sisi wote ni mashahidi, ambazo zimefanywa na Serikali katika kuhakikisha kwamba tunautokomeza ugonjwa huu.

Mheshimiwa Spika, kuna wazo ambalo lipo katika jamii ambalo naona halijatolewa ufafanuzi. Kuna mawazo (misconception) kwamba ugonjwa huu hauathiri watu wenye ngozi nyeusi kama unavyoathiri watu wa mabara mengine, yaani kwamba Bara la Afrika sisi tuna upekee ambao unatupa nafuu katika kudhurika na ugonjwa huu. Mawazo hayo sidhani kama ni mazuri sana kwa sababu pia yanafanya wananchi wanaweza wakazembea katika kujikinga kwa kuamini kwamba wao wakiwa wana ngozi nyeusi watakuwa wana nafasi kubwa zaidi ya kupambana na ugonjwa huu, hiyo ni moja.

Mheshimiwa Spika, lakini kitu kingine, tunafahamu kwamba ugonjwa huu unaleta athari za kiuchumi. Bila shaka Serikali itakuwa ina mkakati wa kuona ni namna gani inachukua hatua za kifedha ili kupunguza madhara ya kiuchumi yanayotokana na janga hili. Kwa hiyo, naomba Serikali na yenyewe iangalie kuona kwamba watachukua hatua gani ambayo itasaidia kuokoa sekta zile ambazo zimeathirika kiuchumi na janga hili la ugonjwa huu

Mheshimiwa Spika, kwenye hotuba ya bajeti ya Waziri Mkuu wamezungumzia na wametoa maelezo yanayojitosheleza kwa namna gani masuala ya ajira na uwezeshaji yamefanyiwa kazi na mikakati ya kusonga mbele. Mimi nina ushauri katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza, ni kuhusiana na mfuko kutengwa kwa asilimia kumi ya mapato ya ndani ya kila Halmashauri kwa ajili ya kuwezesha makundi maalum ikiwa ni pamoja na vijana, wanawake na kundi la ulemavu. Tumeona katika kipindi hiki cha miaka mitano kwenye Bunge hili tulifanya marekebisho ya sheria na sasa tumehakikisha kwamba fedha hizi zinatengwa. Ushauri wangu ni kwamba Serikali ione ni namna gani itatengeneza mfumo wa kielektroniki ambao utaweza kusaidia kufanya michakato yote ya uombaji na utoaji mikopo hii.

Mheshimiwa Spika, pia mikopo hii kuwe na formula kwa sababu jinsi ilivyo sasa hivi kila Halmashauri inakaa vikao vyao kuangalia ni kiwango gani cha chini au cha juu kitatolewa kwa ajili ya mikopo. Kwa hiyo, kuna mbinu tofautitofauti zinazotumika katika maeneo tofauti. Kwa hiyo, katika siku za mbele tuone ni namna gani tunakuwa na mfumo wa kielektoniki ambao utasaidia kusimamia na kuratibu mfuko huu kwa ajili ya kuwezesha vijana, wanawake pamoja na kundi la watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Spika, pia tukiangalia kuna Sheria hii ya Manunuzi ya Umma, Sura 410, kwenye kifungu cha 64(2) kimetoa masharti ya kwamba taasisi au tuseme mashiriika ya umma yatenge asilimia 30 ya manunuzi yake kwa ajili ya kuwezesha vikundi vya vijana, wanawake na watu wenye ulemavu. Naiomba Serikali iweke mkazo na msisitizo kuona kwamba kifungu hiki cha sheria ikiwa ni pamoja na Kanuni zake kinazingatiwa kwa sababu ni eneo pia la vijana wetu, wanawake pamoja makundi ya watu wenye ulemavu kujipatia nafasi ya kutengeneza kipato na kutatua changamoto ya ukosefu wa ajira.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kutoa maoni yangu kwenye suala zima la elimu. Sisi sote ni mashahidi ni kwa kiasi gani jitihada zinafanyika kuhakikisha sekta ya elimu inaboreshwa Tanzania. Tumeona kuna mkakati wa elimu bure, lakini tunaona Bodi ya Mikopo imeongezewa bajeti kwa ajili ya kutoa mikopo kwa vijana wengi zaidi.

Mheshimiwa Spika, nachoomba, kwa sababu sote tunafahamu tuko katika harakati za kuhahakisha tunatengeneza vizuri uchumi wa viwandana tunajua uchumi wa viwanda unahitaji zaidi kada ya kati, kwa hiyo, kuna kila haja pia tuwekeze kwa hali inayotosheleza katika kada ya kati. Tunaona kuna jitihada tofauti tofauti lakini tujiulize ni kwa kiasi gani hawa wanafunzi tuseme wanaosoma masuala ya ufundi, hawa technicians, wale wenye uhitaji kwa mfano wa kupatiwa mikopo kwa ajili ya kuwezeshwa wao kupata taaluma hizo umewekwa kwenye utaratibu kama vile tunavyoona kwenye Bodi ya Mkopo.

Mheshimiwa Spika, hawa graduates, unaweza ukawa na Mhandisi mmoja akasimamia Mafundi Mchundo 20 au Mafundi Sanifu hata 60 lakini hawa Mafundi Mchundo pamoja na mafundi Sanifu wanahitajika wengi zaidi. Sasa itakuwa vizuri zaidi kama pia tukijielekeza katika kuhakikisha tunatengeneza mazingira wezeshi zaidi kwa ajili ya kada ya kati kwa sababu yenyewe ndiyo itakayohitajika zaidi katika uchumi wa viwanda tofauti na hizi ngazi zingine za elimu ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia katika suala zima la elimu tufanye maboresho ya mitaala ya elimu ili iweze kumuandaa mhitimu kuweza kuwa na uwezo wa kutengeneza pesa. Nina maana kwamba mitaala yetu ya elimu iwe inampa mhitimu financial literacy, kwamba akishamaliza kusoma, je, ana uwezo wa kutengeneza pesa? Kwa sababu hiyo ndiyo hoja ya msingi. Unaweza ukawa na degree hata nne lakini kama zile degree zako hujaweza kuzibadilisha katika uzalishaji na kujitengenezea kipato ina maana zinakuwa hazijasaidia. Kwa hiyo, tuone ni namna gani tunaboresha mitaala ya elimu ili iweze kuwaandaa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika, kuwaandaa wahitimu kuwa na uwezo wa kuzalisha pesa.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)