Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Awali ya yote, naomba nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa siku ya leo kunipa afya na kupata uwezo wa kuchangia. Pia nichukue fursa hii kumpongeza Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na timu yake nzima kwa kazi nzuri na ambayo inaonekana. Ndoto za Watanzania sasa zinaendelea kukaribia kutimia na kila sekta imefanya juhudi kubwa. Lengo letu sisi kama Wabunge ni kuendelea kuishauri Serikali na pia kutoa maoni ili yaweze kufanyiwa kazi na tuendelee kuboresha maeneo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii pia kumshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu wetu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa pamoja na Mawaziri wenzake wote kwa kazi kubwa na nzuri wanayofanya kwa kuratibu shughuli zote za uendeshaji mzima wa Serikali, lakini pia shughuli za sera na masuala ya Bungeni.

Mheshimiwa Spika, nikupongeze wewe kwa kutimiza ile ndoto ya kuwa na Bunge mtandao ambayo sasa wote tumeona mafanikio yake. Ingekuwa hiki kipindi ambapo ugonjwa wa Corona umekuja na hatuko katika masuala ya Bunge mtandao naamini Bunge hili lingekuwa limeahirishwa. Hongera sana na pongezi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu moja, tunaomba sasa na Serikali ijitahidi kuweka katika mtandao huu sheria zote ambazo tayari tumezipitishaili tukihitaji kupitia sheria mbalimbali basi tukiingia kwenye tablet zetu tuweze ku- downlod zile sheria tuweze kufanya reference mbalimbali kama kuna kuleta mabadiliko au kuangalia reference mahali ambapo tunahitaji kufanya hivyo. Hiyo itatusaidia sana na itarahisisha mambo mengi ya uendeshaji wa Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia niipongeze timu nzima ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa suala zima hili la Corona na namna wanavyolisimamia. Kuna mengi ambayo yanafanyika, wengi wanaendelea kulaumu lakini mimi najua. Mimi ni Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Kilimo Taifa na tayari sekta ya kilimo inaandaa athari mbalimbali ambazo zinatokana na jambo zima hili kiuchumi kwenye sekta ya kilimo, lakini hivyohivyo kila sekta, ya viwanda na wengine wote wamepewa hayo maagizo. Sekta zote zikishaleta hizo taarifa zao naamini Serikali sasa ndiyo itapata tathmini kamili kutoka kwa wadau wenyewe ndiyo waweze kupanga nini kifanyike ili tuweze kuona hii athari ya kiuchumi na namna ya kusonga mbele, kwa hiyo, hongereni sana.

Mheshimiwa Spika, ombi langu lingine moja kutokana na suala hili la Corona, kama inawezekana Serikali iangalie namna ya kupata vifaa tiba vile ambavyo vinahitajika basi Serikali ingeweza kuondoa kodi ili vifaa hivyo viweze kuingizwa nchini kwa gharama nafuu bila kodi yoyote. Tunajua kabisa Serikali peke yake haitaweza lakini sekta binafsi na wadau mbalimbali wako tayari kusaidia. Kwa hiyo, bidhaa hizi zikiwa zimeondolewa kodi zitakuja kutusaidia hata baada ya janga hili kupita tuna uhakika vifaa hivyo vitaendelea kutumika kwenye shughuli mbalimbali katika sekta nzima ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia niipongeze Serikali kwa ujenzi wa vituo vya afya na zahanati mbalimbali pamoja na hospitali. Nishukuru kwamba sasa hivi tumeona matangazo na madaktari wengi wameomba nafasi zile 1,000; 700 zitakuwa katika ngazi hii ya TAMISEMI lakini 300 zitakuwa ngazi ya Taifa. Tunawapongeza sana, tunaomba hizo ajira mzi-fast track, tunajua wameshaomba ili waende kwa sababu zahanati na vituo vya afya viko tayari ili tuweze kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, pia nilikuwa naomba kwa upande wa TARURA hali ni mbaya, barabara nyingi zimeharibika nchi nzima na siyo jambo la kawaida bali ni kutokana na mvua kubwa zilizojitokeza. Tunaomba mruhusu kwa mwaka huu kwenye fedha zote zitakazoenda TARURA itumike force account ili tuweze kukodisha mitambo kwa gharama nafuu ili angalau tuweze kurekebisha barabara zetu ziweze kupitika wakati wote lakini pia kutengeneza makalvati na madaraja ambayo hayahitaji utaalamu wa hali ya juu ili mawasiliano yaweze kurudi. Pia tuangalie namna ya kuongeza bajeti kwa upande wa TARURA.

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwamba amezungumzia suala la kilimo na hilo nitalizungumza wakati wa bajeti ya Wizara ya Kilimo kwa mapana yake lakini niongelee suala la lishe. Siku zote naamini kwamba kinga ni bora kuliko tiba. Tungewekeza zaidi kwenye upande wa sekta hii ya kilimo kwa mapana yake na watu wakaendelea kupata elimu juu ya lishe hata hili gonjwa la Corona tusingekuwa tunaliogopa sana kwa sababu miili yetu ingekuwa na kinga na hata yale magonjwa mengine, miili ikiwa na kinga nzuri hii gharama tutayotumia kwenye dawa za kutibu itapungua. Kwa hiyo, tuwekeze zaidi huko kwenye sekta ya kilimo kwa mapana yake ili tuweze kujenga afya zetu wenyewe.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo kwenye Sekta ya Ajira na Vijana, naomba kwenye Sekta ya Kukuza Ujuzi tungeendelea kuwekeza. Ile asilimia mbili tuliyopitisha kwenye sheria wakati wa dharura ambayo inakwenda Bodi ya Mikopo, nashauri irudi kwenye VETA (Skills Development) ili vijana wote sasa waweze kuboreshwa kwenye ujuzi kwa kupitia VETA.

Mheshimiwa Spika, kwenye VETA nashauri twende na mfumo wa Builder Apprenticeship Painting System (BAPS) ambapo Mkoa wa Manyarara pale Babati ndiyo ya kwanza Tanzania tumeanza kufanya majaribio. Ni mfumo ambao mwanafunzi anasoma miezi miwili au mitatu, anaenda kutekeleza yale ambayo amefundishwa katika viwanda au katika karakana mbalimbali. Akitoka pale baada ya miaka miwili ni fundi kamili ambaye ni hands on.

Mheshimiwa Spika, Watanzania wengi sasa hivi wanahitaji blue collar jobs, siyo white collar jobs ambapo ana degree yake haimsaidii, hapati ajira. Ingewezekana tungebadilisha sheria kama nchi nyingine, badala ya kwenda JKT ukimaliza Form Four, kila mtu apitie kwenye mfumo huu wa VETA wa kupata skills za aina fulani ili katika maisha kama huna ajira, angalau unajua kitu kingine cha kufanya ambacho kitakupa ajira kwa wakati huo.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nashauri, nashukuru kwamba Ofisi ya Uwekezaji sasa iko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, wanaendelea kuratibu vizuri sana. Tunaomba suala zima kwa kupitia ile road map tumepata hii blue print, tunaomba sasa sheria ile ya blue print ije kwa haraka zaidi ili itekelezwe kusudi gharama za uzalishaji hapa nchini ziteremke, bidhaa zetu ziweze kushindana kwenye soko la ndani na la nje kwa gharama. Hiyo inawezekana kwa kupitia hiyo sheria ya blue print kutekeleza yale yote ambayo yako kwenye blue print.

Mheshimiwa Spika, pia ombi lingine ambalo ni muhimu sana lifanyiwe kazi kwa kupitia uwekezaji, ni suala hili la BRELA, kampuni nyingi zinadaiwa penalty na interest kutokana na kutokuwasilisha returns kwa miaka mingi. Naomba kama mlivyofanya kwenye Kodi ya Mapato, mngewapa msamaha ili tuanze moja. Kwa sababu zile penalty kwa tozo za shilingi 14,000/=, yaani hakuwasilisha kipindi kile, leo ni shilingi milioni 10. Sasa mtu anaona kuanzisha kampuni ni shilingi 300,000/= kwa nini nifufue ile kampuni inadaiwa shilingi milioni 10? Ni vizuri tukafuta yale madeni tuanze fresh…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Jitu Soni. Malizia.

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naunga mkono hoja. (Makofi)