Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. John Peter Kadutu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ulyankulu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa nafasi lakini nianze kukupongeza wewe mwenyewe kwa miaka mitano hii umetuvumilia sehemu kubwa ni kipindi chetu cha kwanza yawezekana mara moja mara mbili labda tulikosea hata kanuni umeendelea kutuvumilia, kwa kweli nafikiria namna ya kuja kukusaidia kampeni kule Kongwa. Pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kuiongoza Serikali hapa Bungeni lakini kwa kuja kututembelea Ulyankulu. Wewe kule ni kwako na tuendelee kukuomba ukipata nafasi uje, bado watu wanakukumbuka sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi hizo nianze na Tume ya Uchaguzi na jambo hili nitaendelea kulisema hata nje ya Bunge mpaka pale tutakapopata ufumbuzi. Mwaka 2015 wakati wa uchaguzi kundi kubwa la watu wetu kule Ulyankulu hawakupiga kura za madiwani na kwa kweli ilileta sintofahamu sana mpaka leo hawajapiga kura kisingizio ni raia wapya lakini kule Katumba na Mishamo ni raia wapya lakini waliweza kupiga kura. Tumefatilia jambo hili kila wakati hatupati majibu na kila wakati nasema hapa na inawezekana Waheshimiwa Wabunge wakawa wanashangaa Kadutu alishang’ang’ania hiyo hoja hapana karibu asilimia 70 ya wapiga kura wa Ulyakulu wanatoka kwenye eneo hili ambalo halikuruhusiwa kupiga kura ya madiwani.

Mheshimiwa Spika, lakini mwaka huu watu hawa hawakuruhusiwa kupiga kura ya Serikali za Mitaa kwa maana ya mwaka jana Novemba hata kuandikishwa na sasa haijajulikana kama watapiga kura au wataendelea tu kukaa kimya au wataendelea kutupigia kura Wabunge na Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nadhani jambo hili lifikie mwisho Kamati yetu ya Bunge ya Mambo ya Nje na Usalama imekuwa inajadili TAMISEMI inajadili na bahati nzuri Mheshimiwa Waziri Mkuu unalifahamu jambo hili hebu huko Serikalini limalizeni ili na wengine tupate hoja zingine kwa sababu kila ukifika kule swali ni hilo, Mheshimiwa Kadutu tutapiga kura au hatupigi kura hawana maswali mengine, je tutaendelea kuishi hapa au tutahamishwa, je wale ambao hawataki uraia wa Tanzania na hawataki kurudi Burundi wataondoka lini? Je, kambi ya wakimbizi na hizo zingine zitafungwa lini? Ni jambo ambalo linawapa shida sana ndugu zangu hawa. Lakini ni lazima tufikirie kama tumewapa narudia tena tuliwapa uraia kwa roho safi basi tuwaruhusu na kama kuna uamuzi tofauti wa Serikali uje badala ya watu kukaa hawajui kinachoendelea hawajengi hawafanyi shughuli kubwa za kiuchumi na mnajua wenzetu wale na sisi wenyewe ni wazalishaji wazuri wa mazao. Tunalisha Kahama, Shinyanga, Mwanza kama mtu anabisha asimame hapa.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie habari ya kilimo, kwenye kilimo nimshukuru tena Waziri Mkuu kwa kushughulikia kero za mazao na hasa tumbaku. Waziri Mkuu alijikita sana kuhakikisha tumbaku inasimama inakaa vizuri, vyama vya ushirika vinakaa vizuri lakini yawezekana Serikalini hamfahamu wiki iliyopita nilikuwepo jimboni nashuhudia kwa macho tumbaku inanunuliwa shilingi 100 mpaka 300 kutoka maalfu ya pesa sasa tumbaku inanunuliwa kwa dharau ile ni dharau. Huwezi kununua tumbaku kwa shilingi 100 kwa shilingi 300 na kama hutaki watu wanasema toa tumbaku ichomwe moto. Hivi kweli mtu msimu mzima masika yote ameshughulika na zao leo anakuja kuwaambiwa shilingi 100 au anaambiwa 300. 300 mtu ana kilo 1000 hakuna kitu pale niiombe sana Serikali isimame iongee nao hawa wenye makampuni wasifanye dharau na ni dhuluma, hii ni dhuluma. Mtu anachukua tumbaku kwa shilingi 300 kwa kweli ni dhuluma.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri Mkuu mimi nikuombe urejee tena uangalie namna ya kuwasaidia wakulima wa tumbaku vinginevyo kilimo cha tumbaku kitakufa na watu wataangalia tena habari ya mazao mengine. Lakini huko nyumba tumbaku ndio ilikuwa zao linaloongoza kwa kuingiza pesa nyingi za kigeni. Leo hii sio kama ilivyokuwa zamani.

Mheshimiwa Spika, linalofanana nalo liko suala la mawakala wa mbolea limechukua muda mrefu toka tumeingia hapa Bungeni mawakala wa Mbolea wamejikusanya wanakuja Dodoma hawajapatiwa majibu. Yaliwahi kutoka majibu kwamba baadhi yao walifanya udanganyifu tukasema sawa lakini wapeni majibu wajue kwamba jambo hili liko mwisho na nani amekosema atolewe ambao hawana makosa wafanye kazi hizo. Kero kama alivyosema mtani wangu mgosi Shangazi suala la NIDA, NIDA hasa vijijini ni tatizo hata huo usajili wa laini za simu umesumbua. Hebu Serikali ihakikishe ifanye tathmini watu wameandikisha na wapya hawajaandikisha waandikishwe lakini Serikali itengeneze mpango mtoto anazaliwa apate usajili wa moja kwa moja tuepukane na jambo hili.

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa kwa sababu mengine tutakutana nayo kwenye Wizara wapo watu wanashangilia ligi ya mpira wetu kusimama. Niwaambie wenzetu wale watoto wa mama mdogo, ligi hata ikisimama bingwa ni Simba.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)