Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi ili nami niweze kuchangia hii hoja iliyoko mbele yetu kwa kujadili hali ya uchumi pamoja na mpango wa maendeleo. Nianze kwa kupongeza sana Waziri wa Fedha, Naibu Waziri na timu nzima kwa kazi nzuri walioifanya ya kutayarisha hii bajeti ya nchi na kufikia hii hatua.

Mheshimiwa Spika, kwa muda huu mfupi nianze moja kwa moja kuchangia baadhi ya maeneo ambayo Waheshimiwa Wabunge walisimama hapa. Wengine walijaribu kuzungumza suala la kwamba tozo nyingi sana kuhusu uvuvi na imeonekana tozo za mifugo peke yake ndizo ambazo zimeweza kushughulikiwa na Serikali lakini tozo za uvuvi hazijaweza kushughulikiwa.

Mheshimiwa Spika, nataka niseme hivi kwa kifupi kwamba, moja tuliamua baada ya kuona changamoto za wavuvi tukaamua kufanya marekebisho ya Sheria ya Kanuni ya Uvuvi ya mwaka 2009 kwa Tangazo la Serikali 383, tukaweza kuondoa kigezo kilichokuwa kinalazimisha Ukanda wa Pwani kuvua dagaa kwa kutumia milimita 10 na badala yake ikiwa ni milimita nane, jambo ambalo lilikuwa ni kilio kikubwa sana kwa wananchi wa maeneo ya Pwani. Hili lilifanyika na tayari kila kitu kiko sawasawa, sasa wanavua kwa milimita nane. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukija kwenye hili eneo hili la kwa nini tozo, ukweli ni kwamba hotuba ya Waziri wa Fedha isingeweza kuchukua mambo yote tuliyoyashughulikia mwaka huu kuyaonesha kwenye taarifa. Nataka niseme kwamba ni kweli kabisa kwamba dagaa walikuwa wanatozwa dola 1.5. Sasa nataka niwaambie hivi, tumerekebisha, Serikali imekubali kilio cha wavuvi na imekubali pia ushauri wa Wabunge, tumepunguza kutoka 0.5 mpaka 0.3 dola za Kimarekani, lakini Ukanda wa Ziwa Nyasa vilevile tumepunguza kutoka 0.5 dola za Kimarekani mpaka 1.3 dola za Kimarekani na Ziwa Tanganyika tumepunguza kutoka dola 1.5 mpaka dola moja.

Mheshimiwa Spika, sababu nyingine ni kwamba kwa nini hizi tozo zinatozwa tofauti tofauti kila eneo; tunatoza tofauti kila eneo kwa sababu Waheshimiwa Wabunge tozo hizi zinapangwa kulingana na thamani ya zao hilo la uvuvi linalozungumziwa. Kwa hiyo dagaa wa Ziwa Tanganyika huwezi kuwalinganisha na dagaa wa Ziwa Victoria, huwezi kuwalinganisha na dagaa wa Pwani.

Mheshimiwa Spika, la pili, ni suala hili la mauzo ya nje; kwamba mauzo ya nje yanaporomoka sana katika sekta hii ya uvuvi kwamba tunauza kidogo. Nataka niseme kwamba ni kweli takwimu zinaonesha na hali ya uchumi katika ukurasa wa kama sikosei wa 72 imeonesha kwamba mauzo yetu ya nje mwaka 2018 yalikuwa dola za Kimarekani milioni 158, lakini mwaka 2017 ilikuwa milioni 193 dola za Kimarekani. Miaka mingine yote kule inacheza kwenye milioni 160, milioni 195, lakini nataka niwaambie Wabunge tumefanya kazi kubwa mambo haya yalisababishwa na vitu vingi. Moja, uvuvi haramu wa kutumia mabomu, wa kutumia nyavu harama ambao tumeushughulikia kwa kiwango kikubwa lakini pia na mambo mengine.

Niwaambie mpaka sasa hivi tunavyozungumza mwaka huu wa fedha 2019, mauzo yetu ya nje mpaka leo hii tunavyozungumza yamefikia milioni 284.7, sawa na bilioni 654, haijawahi kutokea katika awamu nyingine yoyote ile katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna suala hapa Wabunge wamesisitiza sana la uvuvi wa bahari kuu kwamba tuwekeze kwenye bahari kuu. Nataka niwaambie Waheshimiwa Wabunge, Serikali ya Awamu ya Tano imefanya. Moja, mpaka sasa hivi tunavyozungumza consultant wetu anayefanya feasibility study anakabidhi ripoti tarehe 30 Juni, 2019 ya kukamilisha kuanza ujenzi wa bandari yetu ya uvuvi na baada ya tarehe 30 Juni tutaendelea na hatua zinazofuata.

Mheshimiwa Spika, mpaka sasa hivi mazungumzo kati ya Tanzania ya nchi ya Korea kuhusu kujenga hii bandari ya uvuvi yako kwenye hatua nzuri. Kwa hiyo, tunategemea baada tu ya kupata hiyo taarifa ya consultant tutaingia sasa kwenye hatua za ujenzi wa bandari hii ya uvuvi ambayo nayo kwa miaka mingi haikuweza kufanikiwa lakini Serikali hii ya Awamu ya Tano imeweza na hatimaye tunaenda kuwa na bandari yetu ya uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia Wabunge wameshauri Serikali ikubali kununua meli na kuvua majini. Nataka niwape taarifa nzuri kwamba mpaka sasa hivi tumejipanga vizuri kwamba maandalizi mazuri sana yanafanyika ya kununua meli zetu na kuingia kuvua katika ukanda wetu wa bahari kuu. Mwaka huu wa fedha matarajio yetu makubwa tutakuwa tumenunua meli na tumeingia majini. Taasisi zetu zote mbili, TAFICO na ZAFICO ziko kwenye maandalizi mazuri ya kuingia uvuvi wa bahari kuu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hata Wabunge walipochangia wanasema Serikali hii inaenda kutoza wig na kadhalika, Waziri wa Fedha amesema bayana kwa mara ya kwanza tunaenda kuingia kwenye uvuvi wa bahari kuu na mipango yote ile imekaa vizuri na tumejipanga vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la 0.4 zinazotozwa watu wanapovua katika ukanda wetu wa bahari kuu limelalamikiwa na Wabunge, imeonekana ni changamoto. Kesho tunakutana mimi na Waziri mwenzangu wa Zanzibar anayeshughulikia mambo ya uvuvi tuweze kuliamua jambo hili. Kwa hiyo, maamuzi yatakayotoka katika kikao kile yatakuwa ndiyo maamuzi ya Serikali juu ya jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la ngozi limezungumza na Wabunge, kwanza wakiomba asilimia 10 ya export levy kwa ngozi ya wet blue nje ya nchi iondolewe au ipunguzwe. Pia wakaomba asilimia 80 inayotozwa malighafi yetu kuiuza nje ya nchi na yenyewe iondolewe au ipunguzwe.

Mheshimiwa Spika, nataka niseme kifupi kwamba…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, malizia.

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, namalizia kwa kusema kwamba jambo hili Serikali imeshindwa kulifikisha mwisho katika kipindi hiki kwa sababu changamoto za sekta hii ya uvuvi ni nyingi.

Kwa hiyo, nachotaka kuliahidi Bunge lako Tukufu ni kwamba watuachie Serikali tushughulikie hizi changamoto za ngozi hapa nchini kwa kuangalia parameters zote ambazo zinakwamisha biashara hii ambapo tumeshakubaliana Waziri wa Viwanda na Biashara, Waziri wa Fedha na mimi mwenyewe kuhakikisha kwamba hili jambo linafika mwisho sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)